Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maji na Umwagiliaji

Hon. Anthony Calist Komu

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Moshi Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maji na Umwagiliaji

MHE. ANTONY C. KOMU: Mheshimiwa Mwenyekiti, Nakushukuru kunipa nafasi kuchangia hii Wizara, ambayo kwa kweli ni Wizara nyeti, ni Wizara muhimu sana, ni Wizara ambayo kwa kweli inasimamia uhai wetu. Maana yake hali ya maji, isipokuwa nzuri hatuwezi kuwa na Kilimo kizuri, hatuwezi kuwa na hali nzuri ya hewa, hatuwezi kuwa na mazingira mazuri na kwa kweli hatuwezi kuendelea. Kwa hiyo, ni jambo la muhimu sana sana kuzungumza haya mambo ya maji na kuyazungumza katika hali ya umakini wa hali ya juu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme kwamba nimemsikiliza Waziri vizuri, nimesikiliza Kamati na bahati nzuri niko kwenye Kamati ya Kilimo, Mifugo na Maji, kwa hiyo nafahamu vizuri, niseme kwa kweli, kwamba bado hatujawa serious vya kutosha katika kuwekeza katika maji, kwa sababu ukiangalia tu kitakwimu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hizi asilimia 51 ambazo tunazizungumza, tunazungumza bilioni 106 ambazo ni fedha zinatokana na ule mfuko wa maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini katika fedha za ndani, za vyanzo vingine ambazo ni bilioni 284, tumetoa bilioni 48 tu sawa na asilimia saba. Sasa ni vizuri Wabunge wakaelewa, na mtu mwingine yoyote anayeona kwamba tuna tatizo kubwa la maji, akaelewa kwamba hatuko serious kiasi hicho. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu kama tumetenga pesa, halafu tunatoa asilimia saba, tunataka tufanye maendeleo ambapo viwanda vyetu vinategemea maji. Chakula chetu kinategemea maji, mazingira yetu yanategemea maji, hali ya hewa inategemea maji, halafu tunatoa asilimia saba we are not serious. Kwa hiyo nafikiri tuna tatizo hapa la vipaumbele vyetu, kupanga ni kuchagua najua kuna matatizo makubwa mengi, ambayo tunataka kufanya, lakini tunalinganisha maji na nini? Katika nchi hii? Ni kwa nini hatuwekezi kwenye maji vya kutosha? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niombe sana, kwamba Waziri akija hapa na kwenye ukurasa wa 22 wa kitabu chetu hiki cha Kambi Rasmi ya Upinzani, tumesema fedha ya nje imetoka asilimia nne, ni kwa sababu randama inasema hivyo. Kwa hiyo, na Waziri akija hapa tumuombe, hizo bilioni 188 za nje, hata kwenye Kamati, kwa kweli hazikuletwa wakati huo. Kwa hiyo, aje atuambie zimetoka wapi? Na zimekwenda kufanya nini kwenye hiyo miradi ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikitoka hapo na mbaya zaidi, leo pamoja na kwamba changamoto za maji zimeongezeka, lakini bajeti ya maji inapungua. Mwaka jana kwenye hii bajeti tunayoimaliza sasa hivi, tulikuwa na bilioni 673 kwa ajili ya maendeleo, safari hii ni bilioni 610 zaidi ya asilimia nane drop kwa hiyo unaweza ukaona, kwamba ni tatizo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa takwimu zenyewe za Waziri hapo, inaonyesha kwamba nchi yetu sasa hivi iko kweye red line, kwenda kwenye nchi ambazo zina uhaba mkubwa wa maji duniani. Kwa sababu kiwango cha chini, ni meta za ujazo, 1,700 kwa mtu mmoja kwa mwaka. Leo sisi tuko kwenye 1,952 ukilinganisha na mwaka wa 1962 tulivyopata uhuru, tulikuwa 7,000 na kitu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, unaweza kuona ni namna gani, tunaenda kwenye danger zone kwa hiyo nilikuwa naomba sana, kwamba tuendelee kufanya jitihada. Sasa watu wamezungumza hapa, kwamba miradi inaenda kwa kusuasua na Serikali inachangia sana, wakati tunafanya ziara, tulikuta miradi haitekelezwi kwa sababu unakuta mahali ambapo kuna mradi unatekelezwa, mradi mkubwa mzuri unaohitajika sana lakini unaambiwa kwamba vifaa viko bandarini toka mwezi wa kumi na mbili mpaka mwezi huo wa nne ambapo tulikuwa tunapita kwenye hizo ziara havijatoka, kwa sababu msamaha wa kodi haujatolewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini waliosaini Mkataba na wakasema kwamba kutakuwepo na msamaha wa kodi ni Serikali yenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo Serikali saa nyingine inajishika mashati, tunaomba wafanye coordination na Mheshimiwa Jenista yuko hapa, awaratibu hao watu wake, ili tusije tukakutana kutana na hivyo vitu vya aina hiyo kwa sababu implication zake ni kubwa, miradi inachelewa na gharama zinapanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo naomba sana, hilo lizingatiwe, niende Moshi, kule kwenye Halmashauri ya Moshi, tunaambiwa kwamba hali yetu ya maji ni nzuri, nataka niseme hali si nzuri, kwa sababu hiki kinachosemwa ni pamoja na miradi ambayo ilijengwa miaka ya sabini wakati wa Lucy Lameck wanasema bado inafanya kazi. Ukienda kule kwenye Kata kadhaa, Kata ya Kimochi, ukienda kule old Moshi, ukienda kule uru, (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo vyanzo vyenyewe vya maji vilishakauka. Kuna mito ambayo ndiyo ilikuwa ina kuwa source ya maji ilishakauka, kuna chemchem nyingine hazipo tena, mabomba yamechakaa, kwa hiyo, niombe sana, kwamba kama alivyozungumza, Mbunge mmoja hapa ifanyike review tuweze kujua hali halisi ya upatikanaji wa maji ukoje na tusipofanya hivyo tunajivuna leo kwamba tuna bajeti kubwa ya afya ni kwa sababu watu wanaugua sana, na magonjwa mengine yanasababishwa na kutokuwa na maji salama. (Makofi)

MHE. JOHN W. HECHE: Sixty percent ya …

MHE. ANTONY C. KOMU: Mheshimiwa Mwenyekiti, kule Moshi, kuna, na nitoe pongezi sana kwa Mamlaka ya maji pale Moshi, inaitwa MUWASA, inafanya kazi nzuri. Lakini niwaombe sana Wizara, kwamba kuna madeni makubwa wanadai, Majeshi yetu, Chuo cha Polisi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wanadai Magereza zaidi ya bilioni mbili, walipwe hizi fedha. Ili waweze kufanya huu ukarabati ninao uzungumza, waweze kupanua maeneo mengine kupeleka maji. Tunao mradi mmoja sasa hivi ambao unatekelezwa kule, Kata ya mabogini, tunahitajia kama bilioni 1.8. Waziri ameshaniahidi kwamba wanapeleka hizo hela. Nakuomba sana Mheshimiwa Waziri, hizo fedha ziende na tusingekuwa na tatizo kiasi hicho kama hizi fedha zetu ambazo Mamlaka yetu imeshatoa service kwa Serikali yenu halafu hamlipi? Kwa hiyo niwaombe sana kwamba mpeleke hizi fedha ili hiyo miradi iweze kutekelezwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie kwa kusema kwamba Kamati imeshauri, Kamati yetu ya Kilimo, Mifugo na Maji imeshauri kwamba ni usanifu wa miradi inavyofanyika iwe comprehensive iwe inazingatia mambo yote ya muhimu kuwepo na provision kwa ajili ya maji taka. Kuwepo na provision kwa ajili ya fidia, kuwepo na provision kule maji yanakopita. Wale, hata kama haijengwi sasa hivi, lakini designing izingatie hilo. Ili kule maji yanakopita, kwa mfano tumeenda kule Arusha, kuna mradi ambao unatoka Jimbo la Siha kilomita 64 kwenda Jimbo la Longido, hapo katikati kuna watu wana uhitaji mkubwa wa maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini hakukuwepo na provision yoyote kwa ajili ya kuwapa maji kwa ajili ya mifugo, na kwa ajili ya matumizi ya binadamu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, matokeo yake ni kwamba huu mradi utakuwa hatarini siku zote, lakini ukienda pale Arusha Mjini kuna mradi mkubwa unatekelezwa, lakini ukienda kuangalia ni namna gani, design imezingatia land acquisition na kule mabomba ya maji taka yatakapopita unaona bado kwamba watu wana jikanyaga kanyaga. Ndiyo maana unakuta kwamba miradi mingi inaanza, lakini kwenye process unaambiwa kwamba usanifu ulikosewa na sasa mradi umepanda kutoka bilioni fulani mpaka bilioni fulani, sasa ili tuondokane na hilo nafikiri ushauri wa Kamati uzingatiwe. Lingine ambalo tuliliona ni Kampuni moja kupewa miradi mingi kwa wakati mmoja, na matokeo yake, kunakuwepo na visingizio mbalimbali katika kuitimisha hiyo miradi na hili tatizo tuliliona pale Arusha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kwa hiyo tuwaombe sana Mheshimiwa Waziri na watu wake, wafuatilie mambo kama hayo na wahakikishe kwamba hayajirudii. Nakushukuru sana.