Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maji na Umwagiliaji

Hon. Dr. Stephen Lemomo Kiruswa Mamasita

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Longido

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maji na Umwagiliaji

MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa fursa na mimi niweze kuchangia kwenye hoja hii ya Wizara ya Maji. Kwanza nitangulize shukrani za pekee kwa Mheshimiwa Waziri na kwa timu yake yote kwa kazi nzuri wanayoifanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Nitumie fursa hii kuishukuru Serikali ya Awamu ya Tano kwa sababu kati ya watu ambao wameguswa na kujaribu kutatua tatizo la maji nchini ni pamoja na Wilaya yangu ya Longido baada ya ule mradi mkubwa wa maji kutoka Mto Simba kwenye Nyanda za juu za Mlima Kilimanjaro kufikisha yale maji Longido na watu wamefurahia na maji yale kwa kweli yamekuwa ukombozi maana kiangazi ambacho kimekuwa kinaendelea kilipelekea watu wanunue maji mpaka Sh. 1,500 kwa ndoo kutoka katika vyanzo mmbalimbali. Tunaishukuru sana Serikali kwa hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na mawazo mazuri yaliyojitokeza katika hotuba hii na nimeona mambo mengi mazuri yanayofanyika, mimi kwanza niwaunge mkono Waheshimiwa Wabunge wanaosema kwamba tuweke miguuu chini leo mpaka Wizara ya Maji watenge fedha za kutosha kuhakikisha kwamba maji yanamfikia kila Mtanzania ili azma yetu ya kumtua mama ndoo kichwani iweze kutimizwa kweli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishukuru Serikali kwa sababu hii fedha ya Mfuko wa Maji ambayo asilimia 70 imepatikana ikaenda kwenye maji na asilimia 17 tu ndiyo imepatikana kwenye vyanzo vingine, imeonesha kwamba kumbe tungetenga fedha nyingi zaidi kwa vyanzo mbalimbali vya Serikali tungeweza kufikia malengo. Ninaiomba Serikali izingatie suala hili la kuongeza hiyo tozo kwenye mafuta ifike shilingi 100, lakini pia ikamue percent fulani katika kila aina ya tozo inayotozwa kwa huduma mbalimbali katika vyanzo mbalimbali ambavyo Serikali inatoza kodi katika nchi hii. Iwe ni katika Sekta ya Utalii, iwe ni katika Sekta ya madini; sekta zote ambazo Serikali huchukua tozo wekeni percent kidogo iende kwenye kuboresha Mfuko wa Maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na tuzingatie kwamba sasa hivi tuna RUWASA, sasa RUWASA kama ni taasisi iliyoundwa ya kuhakikisha kwamba kuna wataalam wa kutosha, kuna vifaa vya kutosha, watapataje kuendesha kwa ufanisi kama hawana fedha?

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ninaomba kwanza kodi zinazokera, za kuumiza hizi tasisi za maji, ziondolewe, kama mitambo ya maji ifutiwe kodi, vifaa vya kuchimba mabwawa vifutiwe kodi na kila namna ifanyike ili kuhakikisha kwamba tunauinua huu mfuko ili tumtoe mama ndoo kichwani na kweli tufikishe huu uhai ambao tunasema maji ni uhai kwa kila Mtanzania. Tukipata maji safi na salama katika nchi hii miradi mingine yote ya maendeleo itawezekana. Afya ya watu itaboreka, muda wa kuwekeza kwenye shughuli nyingine za uchumi utaimarika maana muda mwingi hupotea katika kutafuta maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuunga mkono hiyo hoja na kutoa dukuduku langu la kutamani Wizara iongeze bajeti yake, naomba nijielekeze katika masuala mahususi ambayo yamejitokeza katika hii hotuba, na imegusa miradi ambayo inagusa sana maisha ya wananchi wa Jimbo langu la Longido. Katika ukurasa wa 119 kuna kiambatisho namba 2 kinachoongelea kiwango cha maji katika maziwa, mito mabwawa na vyanzo mbalimbali vya maji nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna Mto unaitwa Mto Ngarenanyuki, huu mto unatiririsha maji kutoka Arusha National Park unapitia Arumeru unakuja mpaka Longido, Kijiji cha Ngereiyani. Maji yake yana fluoride nyingi, sio mazuri kwa binadamu, lakini yanafaa sana kwa kilimo cha nyanya. Wakulima wengi wamegundua kwamba hayo maji yanaotesha nyanya ya ubora wa kimataifa, nyanya zinauzwa kila mahali nchi hii, Dar es Salaam, mpaka nchi za nje, Mombasa na zinakwenda mpaka Nchi za Uarabuni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini sasa kwa matumizi holela ya huo mto mifereji imepasuliwa kila mahali, nyanda za mto zimeharibiwa, huo mto unakwenda kupoteza hadhi yake na mazingira yanaharibika na maji hayafiki tena kwenye nyanda za chini, wananchi wa Ngereiyani hawapati tena yale maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba Serikali pia iweke usanifu wapime kiwango cha hayo maji na ikiwezekana wajenge matenki maji yapitie kwenye matenki ndiyo kutoka kwenye mabomba yaende kwenye mashamba ya wakulima wadogo wadogo ili tuhifadhi mto na watu wengi waweze kufikiwa na hayo maji, tuboreshe kilimo cha umwagiliaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, kwa sababu maji ya Mto Simba yanakwenda kusuluhisha tatizo la maji kwa wakazi ambao kwa sasa hivi, hii awamu ikikamilika ni watu kama 18,000 tu wa Kata ya Longido na Kata ya Engikaret na kwa sababu tumetengewa bilioni 2.9 na ninaishukuru Serikali sana kwa sababu ya usambazaji wa hayo maji. Basi huu mradi utakapokuwa umesambaza hayo maji yakatimiza ahadi ya viongozi wakuu wa Serikali akiwepo Rais ya kupeleka hayo maji mpaka Namanga, Kimokowa na kusambaza kule Kiserian, tutakuwa tumetatua kero ya maji kwa wananchi wasiopungua 30,000 wa Longido, lakini bado kuna watu zaidi ya 100,000 ambao hawana chanzo cha uhakika cha maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilishawahi kusema katika Bunge hili kwamba maji ya mafuriko ya mwaka jana yalitupasulia mabwawa ambayo ndiyo yalikuwa yanategemewa na jamii ya wafugaji katika wilaya yangu. Kuna mabwawa yamefukiwa kabisa, kuna mabwawa yamepasiuka, nilitegemea kwenye bajeti hii kwenye ile miradi mingine ambayo Waziri ametaja katika hotuba yake, kuona kuna miradi mingine ya maji ukiacha haya maji ya mito; ningetegemea mabwawa yale yaliyopasuka na yaliyojaa udongo yangetengewa bajeti maana sisi mabwawa hayohayo ndiyo maji ya binadamu ndiyo hayohayo ya mifugo; Bwawa na Kimokowa, Bwawa la Tinga Lesing’ita, Bwawa la Sinoniki, Bwawa la kule Muriatata na mabwawa mengine mengi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na kuna ahadi za Serikali za kuchimba pia mabwawa mengine ambayo yatafaa kwa hata umwagiliaji pale katika Kata ya Tingatinga. Kuna ahadi ya Serikali ya kuchimba bwawa la umwagiliaji ili haya maji yanayotiririka ya msimu wa mvua kutoka Kilimajaro yatekwe wananchi wa Tingatinga waweze kuendesha kilimo cha umwagiliaji na maji hayohayo yatafaa kwa mifugo na watu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na kule Wosiwosi, mwisho wa Wilaya hii ya Longido katika Ukanda unaopakana na Kenya na Wilaya ya Ngorongoro kuna Kijiji kinachoitwa Wosiwosi, wao maji ya kunywa binadamu hakuna kabisa mpaka wanakwenda Kenya kutafuta maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuliomba pia bwawa na nilitegemea bwawa hilo lingewekwa kwenye ile miradi mingine ili wananchi wa Longido ambao wako mbali na haya maji ya Mto Simba waweze nao kufarijika na kuona kwamba Serikali ya Awamu ya Tano inawajali kwa suala la maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nitumie fursa hii kuwashukuru baadhi ya wadau ambao wametuunga mkono katika kutatua kero za maji Longido; tuna Shirika la Maisha Bora, wamekuwa wakitusaidia katika miradi ya kuchimba visima virefu katika Kata ya Matale; kuna taasisi ya kiwindaji inaitwa Kilombero Safaris wakishirikiana na Shirika linaitwa World Self International, wamekuwa wakitusaidia kupima maeneo mbalimbali kubainisha maeneo yenye maji ya chini pamoja na wengineo kama Friends for African Development, marafiki zetu kutoka Chuo Kikuu kimoja cha Marekani ambao wametuchimbia visima vitatu. Naomba Serikali itambue juhudi zao na iendelee kututengea fedha za kuchimba visima virefu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la mwisho ambalo ninapenda kuchangia ni suala la umuhimu wa kuvuna maji ya mvua katika nchi yetu. Maji ya mvua yakivunwa, na sheria ipitishwe – maana kabla sijawa Mbunge ilishatengeneza sheria lakini sidhani kama inafanyiwa kazi – na iwekwe kwamba ni kampeni ya kitaifa; kila kaya wahimizwe wawe na mfumo wa kuvuna maji ya mvua, iwe ni sehemu ya requirement katika kusimamia utekelezaji wa ujenzi wa nyumba za makazi ya watu na taasisi mbalimbali nchi hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maji ya mvua yatatuondolea kero ya maji kwa asilimia kubwa. Inaponyesha hata katika maeneo kame maji mengi yanapotea kwa sababu hatuvuni maji ya mvua na nimeenda katika nchi zingine, kama Jimbo la California kule Marekani, wao hawana mto wowote lakini maji yote ya mvua yanavunwa na wanalimia mpaka wanauza mazao ya matunda nchi za nje; kwa nini sisi Tanzania wenye maji mengi ya mvua ambayo yanafurika kila wakati inaponyesaha, hata katika maeneo kame tusiige huo mfano tukahimiza uvunaji wa maji ya mvua katika mabonde, tuhimize uvunaji wa maji ya mvua katika nyumba zetu za bati kila kaya ihimizwe iwe na mfumo na wataalam wa Serikali wasimamie hiyo kama kampeni mahususi katika shule, katika hospitali, katika taasisi za dini na nyumba za makazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa lakini sio kwa umuhimu, nipende pia kutumia fursa hii kuishukuru Serikali kwa sababu sisi katika Wilaya ya Longido ambayo ni wilaya ya wafugaji kwa asilimia 95, na ni wilaya ya uhifadhi pia wa mazingira ya wanyamapori kwa asilimia hiyohiyo 95, tumeendelea kuona mkono wa Serikali kupitia kile chakula tulichopewa wakati wa ukame. Wananchi wa Longido wamefarijika na wamesema kila wakati ukisimama Bungeni mshukuru Rais kwa sababu tulipolia njaa kwa sababu ya ukame tulipewa chakula, tulitengewa chakula tani 10,000 za mahindi na tani 1,000 ndiyo zinazoendelea kuwalisha watu katika mwezi huu wote tunavyoangalia hali ya hewa itakavyokuwa. Na tumshukuru Mungu mvua imenyesha lakini haitoshelezi.

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa.

MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja, ahsante sana kwa kunipa nafasi.