Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Hon. Prof. Joyce Lazaro Ndalichako

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Kasulu Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, kwanza kabisa sina budi kumshukuru Mwenyezi Mungu kuniwezesha kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu kwa ajili ya kuhitimisha hoja ambayo niliiwasilisha mbele ya Bunge lako mnamo tarehe 29 Aprili, 2019.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee kabisa naomba nikushukuru wewe kwa kuuongoza vyema mjadala wa hoja yangu, lakini pia niwashukuru Waheshimiwa Wabunge wote ambao wametoa michango mizuri katika bajeti ambayo nimewasilisha leo kuhusu Fungu Namba 46 pamoja na Fungu Namba 18.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nitoe shukurani za kipekee kwa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kwa ushirikiano mkubwa ambao wameendelea kuutoa katika Wizara yangu na kwa kweli kwa mara nyingine nishukuru sana Uongozi wa Bunge kwa kuisuka vyema Kamati ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii ambayo hakika imesheheni Wajumbe ambao wanaifahamu vyema sekta ya elimu. Kwa hiyo wamekuwa na michango mizuri ambayo hakika inachangia sana katika kuboresha elimu katika nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia nishukuru sana Waheshimiwa Wabunge wote ambao wamechangia hoja hii. Tumepokea michango mingi sana na michango mizuri ambayo yote ilikuwa na lengo moja na kuhakikisha tunaimarisha na kuboresha elimu katika nchi yetu na kuweka mazingira rafiki kwa vijana wa Kitanzania ili waweze kujifunza vizuri. Kwa hiyo, nianze kusema tu kwamba kwa moyo mkunjufu, Wizara imepokea michango yote ambayo imetolewa na Waheshimiwa Wabunge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jumla ya Waheshimiwa Wabunge 114 walichangia hoja yangu na kati yao, Waheshimiwa Wabunge 63 wamechangia kwa maandishi na Wabunge 51 wamechangia kwa kuongea. Naomba kwa sababu ya muda siwezi kuwataja lakini naomba orodha yao iingie kwenye Hansard waweze kutambulika.

Waheshimiwa Wabunge waliochangia kwa maandishi ni pamoja na Mheshimiwa Sophia Mwakagenda, Mheshimiwa Omari M. Kigua, Mheshimiwa Amina N. Makilagi, Mheshimiwa Husna S. K. Mwilima, Mheshimiwa Richard M. Ndassa, Mheshimiwa George M. Lubeleje, Mheshimiwa Rhoda E. Kunchela, Mheshimiwa Joseph L. Haule, Mheshimiwa Joseph M. Mkundi, Mheshimiwa Aida Joseph Kheneni, Mheshimiwa Nuru A. Bafadhili, Mheshimiwa Mbaraka Kitwana, Mheshimiwa Shaabani O. Shekilindi, Mheshimiwa Daimu Iddi Mpakate, Mheshimiwa Zuberi M. Kuchauka, Mheshimiwa Engineer Gerson H. Lwenge, Mheshimiwa Hamidu H. Bobali, Mheshimiwa Ally M. Kessy, Mheshimiwa Margaret Sitta, Mheshimiwa Ruth H. Mollel, Mheshimiwa Esther N. Matiko, Mheshimiwa Dkt Chrestine G. Ishengoma, Mheshimiwa Dkt. Steven Kiruswa, Mheshimiwa Suzana C. Mgonukulima, Mheshimiwa Ignas A. Malocha, Mheshimiwa Flatei G. Massay, Mheshimiwa Engineer Edwin A. Ngonyani, Mheshimiwa Lucia U. M. Mlowe, Mheshimiwa Zainabu M. Amiri, Mheshimiwa Lucy S. Magereli, Mheshimiwa Ritta E. Kabati, Mheshimiwa William V. Lukuvi, Mheshimiwa Mgeni J. Kadika, Mheshimiwa Abdallah D. Chikota, Mheshimiwa Kiza
H. Mayeye, Mheshimiwa Mary D. Muro, Mheshimiwa Anatropia L. Theonest, Mheshimiwa Dkt. Pudenciana Kikwembe, Mheshimiwa Sonia J. Magogo, Mheshimiwa Zainab M. Bakar, Mheshimiwa Silafu J. Maufi, Mheshimiwa Mussa B. Mbarouk, Mheshimiwa Cosato D. Chumi, Mheshimiwa Timotheo P. Mnzava, Mheshimiwa Joyce B. Sokombi, Mheshimiwa Lolesia J. Bukwimba, Mheshimiwa Shally J. Raymond, Mheshimiwa Marwa R. Chacha, Mheshimiwa Juma O. Hija, Mheshimiwa Omari A. Kigoda, Mheshimiwa Mashimba M. Ndaki, Mheshimiwa Qambalo W. Qulwi, Mheshimiwa Mahmoud H. Mgimwa, Mheshimiwa Elibariki I. Kingu, Mheshimiwa Jitu V. Soni, Mheshimiwa Devotha M. Minja, Mheshimiwa Rev. Dkt. Getrude P. Rwakatare, Mheshimiwa Maria N. Kangoye, Mheshimiwa Salma R. Kikwete, Mheshimiwa Catherine N. Ruge, Mheshimiwa Zainabu N. Mwamwindi, Mheshimiwa Khadija N. Ali, Mheshimiwa Dkt. Dalaly P. Kafumu na Mheshimiwa Richard P. Mbogo.

Aidha, Waheshimiwa Wabunge waliochangangia hotuba ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia ya mwaka wa fedha 2019/2020 kwa kuzungumza ni pamoja na Mheshimiwa Yosepher F. Komba, Mheshimiwa Rashid Abdallah Shangazi, Mheshimiwa Mendrad L. Kigola, Mheshimiwa Joram I. Hongoli, Mheshimiwa Aida Joseph Khenani, Mheshimiwa Almas Athuman Maige, Mheshimiwa Joseph Leonard Haule, Mheshimiwa Pascal Y. Haonga, Mheshimiwa Hasna Mwilima, Mheshimiwa Phillipo A. Mulugo, Mheshimiwa Joseph M. Mkundi, Mheshimiwa Sikudhani Y. Chikambo, Mheshimiwa Mendrad Lutengano Kigola, Mheshimiwa Abdallah D. Chikota, Mheshimiwa Amina N. Makilagi, Mheshimiwa Edward F. Mwalongo, Mheshimiwa Shaaban O. Shekilindi, Mheshimiwa Daimu I. Mpakate, Mheshimiwa Esther N. Matiko, Mheshimiwa Engineer Edwin A. Ngonyani, Mheshimiwa Aida Joseph Khenani, Mheshimiwa Angelina A. Malembeka, Mheshimiwa Vedasto E. Ngombale, Mheshimiwa Salma R. Kikwete, Mheshimiwa Jumanne K. Kishimba, Mheshimiwa Sixtus R Mapunda, Mheshimiwa Zainab
M. Bakar, Mheshimiwa Dkt. Immaculate S. Semesi, Mheshimiwa Profesa Jumanne A. Maghembe, Mheshimiwa Dkt. Jasmine T. Bunga, Mheshimiwa Rashid M. Chuachua, Mheshimiwa Balozi Dkt. Diodorus B. Kamala, Mheshimiwa Joseph K. Mhagama, Mheshimiwa Tauhida C. G. Nyimbo, Mheshimiwa James F. Mbatia, Mheshimiwa Hamidu H. Bobali, Mheshimiwa Susan A. J. Lyimo, Mheshimiwa Marwa R. Chacha, Mheshimiwa Maria N. Kangoye, Mheshimiwa Fatma H. Toufiq, Mheshimiwa Kemilembe J. Lwota, Mheshimiwa Dkt. Charles J. Tizeba, Mheshimiwa Masoud A. Salim, Mheshimiwa Khadija N. Ali, Mheshimiwa Sebastian S. Kapufi, Mheshimiwa Goodluck A. Mlinga na Mheshimiwa Mwita M. Waitara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia niwashukuru Waheshimiwa Mawaziri ambao wamechangia hoja yangu. Kwa namna ya kipekee nimshukuru sana Kaka yangu Waziri wa Fedha amejibu vizuri na kitaalam hoja zinazohusu masuala ya fedha lakini pia nimshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri, TAMISEMI na yeye kwa ufafanuzi wa hoja ambao ameutoa. Kwa ujumla kwa kweli Wabunge wote kwa umoja wenu michango yenu imekuwa ni mizuri na kipekee kabisa nimshukuru Waziri Kivuli Mheshimiwa Susana Lyimo hakika safari hii umekuja kivingine na hotuba yako imesheheni ushauri. Kwa hiyo tunashukuru sana na kwa mara ya kwanza, Mheshimiwa Susan Lyimo ameipongeza Taasisi ya Elimu Tanzania, nashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli niwaahidi Waheshimiwa Wabunge kwamba sitaweza kwa muda niliopewa kujibu hoja zao zote lakini hoja zote zitajibiwa kwa maandishi na tutahakikisha kwamba kabla ya kumaliza Bunge hili basi tutaweza kukabidhi majibu yetu kwa Waheshimiwa Wabunge wote. Kwa hiyo, naomba sasa nizungumzie tu hoja ambazo nitaweza kuzizungumza kutokana na muda nilionao na nitaanza na masuala ambayo yamezungumzwa na Waheshimiwa Wabunge wengi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa kuanza na suala la uchapaji wa vitabu; suala la uchapaji wa vitabu limejitokeza na hii ninaamini ni kwa sababu Waheshimiwa Wabunge wanatambua kwamba vitabu na Taasisi ya Elimu ndiyo moyo wa sekta ya elimu. Kwa hiyo Taasisi ya Elimu ispofanya vizuri ni dhahiri kwamba elimu yetu itakuwa haiko vizuri. Baadhi ya hoja ambazo Waheshimiwa Wabunge wamezizungumzia ni kutokuwepo kwa vitabu vya baadhi ya masomo na kutokuwepo kwa vitabu vya elimu ya msingi, vya darasa la Tano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kwanza kabisa nianze kuwashukuru Wabunge wote waliochangia kuhusiana na suala la vitabu kwa sababu suala la ufundishaji na ujifunzaji haliwezi kwenda vizuri kama hatuna vitabu ambavyo ni vizuri kwa hiyo maoni yao na msisitizo ambao wanauweka unaendana pia na namna ambavyo Serikali imekuwa ikiisimamia Taasisi hii ya Elimu na ndiyo maana hata katika Bunge hili nadhani ni kwa mara ya kwanza ambapo tunazungumzia Bajeti ya Wizara ya Elimu na hakuna vitabu vibovu ambavyo vimeletwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakumbuka ilikuwa mwaka 2013 Mheshimiwa Mbatia aliingia na sanduku la vitabu ambavyo vimejaa makosa na ndiyo maana Serikali ikaamua, wakati huo hivyo vitabu vilikuwa vinachapwa na Kampuni binafsi Serikali ikaamua sasa hilo jukumu kurudisha Taasisi ya Elimu Tanzania. Lakini bahati mbaya Taasisi ya Elimu Tanzania na yenyewe ilipoanza wanasema Waswahili “mwanzo ni mgumu” haikufanya vizuri katika baadhi ya maeneo lakini, Serikali tulikuwa wakali kweli kweli na vile vitabu vyote vyenye makosa tuliviondoa shuleni na sasa hivi Taasisi ya Elimu imesimama vizuri na kazi yao imetukuka kwa hiyo tunakwenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwahiyo napenda kuliarifu Bunge lako Tukufu vitabu vya darasa la Tano vilishasambazwa shuleni nakala milioni 2,867,400 waliochelewa kupata walipata Mwezi Februari, na kwa sababu kuna tabia ya baadhi ya watu kufungia vitabu, tunapeleka shuleni lakini havifiki kwa walengwa, kwa hiyo, nilivyosikia tu Waheshimiwa Wabunge wanachangia nilifuatilia hata kwenye hizo halmashauri kuuliza kulikoni wakati tunajua vitabu vimepelekwa inakuaje Waheshimiwa Wabunge wanakuja kuuliza huku Bungeni? Kwa hiyo, nimejiridhisha na hata sehemu ambazo waliuliza maswali vitabu vilivyochelewa kufika vilikuwa ni Mwezi wa Pili kwa hiyo vitabu viko shuleni na wanafunzi wanavisoma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja nyingine ilihusu kutokuwepo kwa mtaala na mihtasari kwa shule zinazotumia lugha ya Kingereza; naomba niliarifu Bunge lako Tukufu, mitaala kwa lugha ya Kingereza ilishaandaliwa tangu Mwaka 2016 na inapatikana katika duka la vitabu la Taasisi ya Elimu Tanzania na Maduka ya Mawakala wa Taasisi ya Elimu Tanzania ambayo yanapatikana katika Mikoa yote nchi nzima.

Mheshimiwa Mweyekiti, aidha, Wizara kupitia Taasisi ya Elimu Tanzania imekamilisha kazi ya kuandaa vitabu vya kiada kwa shule zinazotumia lugha ya Kingereza kama lugha ya kufundishia kwa Darasa la Kwanza, la Pili na la Tatu na vitabu hivyo nilisema katika hotuba yangu, kwamba tumeanzisha Maktaba ya Mtandao. Kwa hiyo, vitabu hivi ambavyo nimekuja na sampuli kuwaonyesha Waheshimiwa Wabunge vinapatikana katika Maktaba mtandao kwa hiyo vitabu vya lugha ya Kingereza vipo hivi hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwaombe Waheshimiwa Wabunge watembelee tovuti yetu kama inavyoonekana pale ambayo ni www.tie.go.tz ili waweze kujipatia kwa urahisi vitabu ambavyo tayari Serikali imekwisha viandaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja nyingine ambayo ilizungumzwa na Mheshimiwa Ndugu yangu na rafiki yangu kabisa Mheshimiwa Phillipo Mulugo kuhusiana na suala la vitabu ambavyo vilikuwa na dosari. Baada ya marekebisho ambayo Serikali imefanya, amesema kwamba kuna baadhi ya wadau wetu ambao walikuwa wamevinunua na hivyo wamepata hasara kubwa sana kwa sababu vitabu vilivyokuwa Serikalini vimeondolewa lakini wale wadau wengine ambao walikuwa wamenunua nje ya mfumo wa Serikali wao wamepata hasara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa taarifa ambazo tunazo, Serikali haikuwa imeuza kitabu chochote kwa mtu yoyote kwa sababu makosa yalibainika mara tu baada ya kusambaza hivyo vitabu. Kwa hiyo, naomba niseme mbele ya Bunge lako tukufu, kama kuna mtu wa yoyote ambaye alikuwa amenunua vitabu ambavyo vina makosa ninaomba awasilishe vilelezo (receipt) yake na vitabu ambavyo vina makosa na Serikali itambadilishia kwa sababu tayari Serikali imetoa tamko la kuviondoa vitabu hivyo shuleni na havitakiwi kutumika mahali popote na havitakiwi kuwa kwenye circulation kwa sababu watoto wadogo wanaweza wakakutana nacho wakakitumia. Kwa hiyo, ni msimamo wa Serikali vile vitabu ni marufuku kutumika mahali popote. Kwa hiyo, kama kuna mtu ana kitabu na alikuwa amekinunua akirudishe na atapewa kitabu kingine ambacho ni kizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine limezungumzwa na Ndugu yangu Mheshimiwa Esther Mahawe ambaye ni Rais wa TAPIE (Wamiliki wa Shule Binafsi) na alikuwa anazungumzia suala la gharama za mafunzo kwa ajili ya walimu wa shule binafsi. Nimesikia hapa lugha zinazungumzwa kwamba utoaji wa elimu bure kwamba kunakuwa na ubaguzi kwenye shule za Serikali wanafanya mitihani bure au wanakuwa wanafanya mafunzo bure.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme hakuna kitu cha bure, shule za Serikali zinalipiwa na Serikali ndiyo maana Waziri wa Fedha kila mwezi anatoa bilioni 23.8 kwa hiyo hakuna cha bure, inategemea tu kwamba gharama inalipwa na nani. Kwa hiyo, Serikali inalipia Walimu wanapokuwa wanakwenda mafunzo kazini, Serikali inawalipia wanafunzi wanapokuwa wanafanya mitihani. Na shule binafsi tungeziomba zichangie katika grarama za mafunzo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, suala la gharama ya mafunzo ambayo iliwekwa, kwa taarifa nilizonazo ni kwamba walikaa kikao wakawa wameshauriana Wamiliki wa Shule Binafsi na Taasisi ya Elimu Tanzania na niwaombe kwa sababu kwa kweli tunafanyakazi vizuri na shule binafsi, kama hizo fedha ambazo mlikuwa mmekubaliana baadaye mmeziona kwamba ni kubwa, rudini tu mkakae kwenye mazungumzo. Nia yetu ni moja kuhakikisha kwamba tunaendeleza elimu yetu, sidhani kama tunaweza tukashindwa kuelewana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo limezungumzwa sana na Waheshimiwa Wabunge wengi ni malalamiko kuhusiana na kubadilika kwa mtaala mara kwa mara. Napenda kulijulisha Bunge lako Tukufu kwamba tangu tumepata uhuru mwaka 1961 mtaala umebadilika mara nne tu. Tangu tumepata uhuru mwaka 1961 mitaala ya elimu imebadilika mara nne tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mara ya kwanza ni mara baada ya kupata uhuru, mara ya pili ni baada ya Azimio la Arusha mwaka 1967, mara ya tatu ulibadilika mwaka 1979 kuingiza masomo ya michepuo na mara ya nne ulibadilika mwaka 1997 baada ya mfumo wa vyama vingi vya siasa kwa hiyo kulikuwa na context ambazo zilibadilika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati mwingine tunakuwa tunafanya maboresho ya mtaala. Nitatoa mfano, kwa mfano, mwaka 2005 kumezaliwa Nchi ya Sudan Kusini ni lazima tufanye maboresho haya siyo mabadiliko. Ni maboresho katika mtaala kuonyesha kwamba nchi za Afrika idadi imeongezeka kwa sababu kuna nchi mpya imezaliwa, haya hauwezi ukasema ni mabadiliko. Kwa hiyo, kumekuwa na maboresho ambayo yanafanyika madogo madogo ya kawaida, maboresho yanayozingatia mabadiliko ya Sayansi na Teknolojia, lakini mabadiliko makubwa yamefanyika mara nne tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na suala hilo, watu wamezungumzia sana mfumo wa elimu yetu na vilevile wamzungumzia sana hata suala la kwamba sasa hivi elimu yetu inakuwa inakwenda ndivyo sivyo na nilikuwa natafuta hapa quotation ya Mheshimiwa Susan Lyimo aliyoanzanayo. Katika kitabu chake alianza na quotation ya kuonyesha kwamba “ukitaka kuangamiza nchi yetu basi uchezee mfumo wa elimu na kwamba ukiwa na watu wenye vyeti feki, ukiwa na watu ambao wamekaa wanafanya kazi mahali ambapo sipo basi itakuwa ni silaha kubwa ya kuangamiza nchi yetu”.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikuhakikishie kwamba Serikali ya Awamu ya Tano iko makini sana na inatambua kwamba bila mfumo imara wa elimu basi mambo hayawezi kwenda vizuri na ndiyo maana Serikali ilifanya uhakiki wa watu wenye vyeti feki. Jumla ya watumishi 15336 wameondolewa kwenye Utumishi lakini pia Serikali kwa kutambua kwamba ukimuweka mtu mahali ambapo hana sifa nazo hawezi kufanya vizuri. Zaidi ya watumishi 5300 ambao walikuwa wameajiriwa katika fani ambazo hawana ujuzi nazo wameondolewa. Wanataka Serikali ifanye nini zaidi ya hapo kuonyesha kwamba inatambua na kujali umuhimu wa elimu katika nchi yetu ya Tanzania? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo limezungumziwa, nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango amejibu vizuri na kitaalam masuala ambayo yanahusiana na masuala ya fedha. Lakini naomba tu nifafanue moja. Kuna suala moja ambalo kwa kweli niseme hapa na Ndugu zetu Washirika wa maendeleo wako pamoja na mimi walikuja hapa jana na Kiti kiliwatambulisha na hata sasa wanafuatilia mjadala wetu. Haipendezi hata kidogo kwa mtu ambaye ni mstaarabu, mtu ambae ni muungwana, mtu ambae anashirikiana na wewe katika maendeleo tunatumia maneno ya ajabu ajabu kuwasema Washirika wetu wa maendeleo, siyo jambo jema hata kidogo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme kwanza hii dhana ya kusema kwamba Serikali imekuwa tegemezi sana siyo sawa. Ukiangalia bajeti ya Wizara kwa miaka mitatu iliyopita; Mwaka 2017/2018, mchango wa Serikali ulikuwa ni asilimia 66.2 na mchango wa Wafadhili ulikuwa ni asilimia 33.8 lakini katika Mwaka huu wa fedha wa Bajeti hii ambayo Waheshimiwa Wabunge, ninawaomba kwa unyenyekevu kabisa muidhinishe mchango wa Serikali ni asilimia 67.6 na mchango wa Wafadhili ni asilimia 32.4, kwa hiyo, Serikali imeendelea kuwa inapunguza utegemezi. Lakini Waheshimiwa Wabunge naomba niwaulize swali; hivi kama Serikali ina mahusiano mazuri na wafadhili, ina marafiki kutokana na Utawala Bora, wako tayari kuja kutoa misaada katika nchi yetu, kuna kosa gani Ndugu zangu? Kwa sababu inakuwa kama vile ni dhambi. Kwa nini inakuwa kama vile ni dhambi Serikali ikipata misaada kutoka nje? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa nafikiri mngeipongeza Serikali, haiwezekani mtu aje akuletee fedha zake kama wewe huna usimamizi mzuri, kama wewe huna Utawala Bora, kama wewe husimamii vizuri zile fedha ambazo zinaletwa. Kwa hiyo, Ndugu zangu sioni kama kuna sababu yoyote ya kuhangaika na nitoe tu taarifa kwamba hata sasa hivi tunapoongea Serikali ya Uswisi imetoa msaada wa jumla ya shilingi bilioni 14,900,000,000 kwa ajili ya kuendeleza ujuzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na hizi hata kwenye kitabu chako hazionekani kwa sababu ni makubaliano ambayo tumeingia hivi karibuni na tarehe 31 Mei tutazindua rasmi huu mpango. Lakini nitoe taarifa zaidi kwamba kupitia Global Partnership in Education, mfuko huu umetoa Dola milioni 90 kwa Tanzania mwanzoni mwa Mwezi huu wa Nne ambao ni sawa na bilioni 200 za Kitanzania na huo ni msaada kutokana na Utawala Bora katika nchi yetu ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho kuhusiana na fedha maana mengi Mheshimiwa Waziri ameyajibu; kumekuwa pia na dhana kwamba bajeti ya Wizara imepungua, mwaka uliopita ilikuwa trilioni 1,407,000,000,000 na Mwaka huu ni trilioni 1,388,000,000,000. Waheshimiwa Wabunge naomba niwahakikishie Serikali hii ya Awamu ya Tano iko makini sana na Bajeti ya Wizara ya Elimu ndiyo maana mmeona kuna mambo mengi mazuri yamefanyika. Naomba niwaambie kwamba fedha za elimu hazijapungua isipokuwa tumekuwa na mabadiliko kidogo katika program yetu ya lipa kulingana na matokeo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kiasi cha shilingi bilioni 90,088,000,340 za Lipa Kulingana na Matokeo tumezipeleka katika Fungu Namba 56-Ofisi ya Rais, TAMISEMI. Kwa hiyo, kama zingebaki katika Fungu Namba 46 kama ambavyo ilikuwa katika bajeti ya 2018/2019, bajeti yetu ingesomeka trilioni 1,478,000,000,000. Kwa hiyo, endeleeni kumuamini Mheshimiwa Rais wetu Dkt. John Pombe Magufuli yuko makini sana katika maeneo ambayo ni muhimu katika Taifa hili, na kamwe hawezi kuchezea mfumo wa elimu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa nizungumzie suala ambalo limekuwa likijitokeza ambalo Waheshimiwa Wajumbe wa Kamati yetu wamekuwa wakitushauri kama Serikali. Kwa kweli kama nilivyosema tunaheshimu sana na kuthamini michango ambayo inatolewa na Kamati yetu ya Huduma na Maendeleo ya Jamii lakini nikiri tu kwamba wakati mwingine siyo kila ushauri unaweza ukafanyika au ukatekelezeka kwa mara moja na haina maana kwamba usipotekeleza umepuuza. Kwa hiyo, naomba Waheshimiwa Wabunge tunaposema Serikali imepokea ushauri mtuelewe hivyo kwamba kuna mambo mengine ambayo tunapaswa kama Serikali kuyazingatia na kujiridhisha kabla ya kutekeleza moja kwa moja ushauri ambao umetolewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna ushauri ambao umetolewa kwamba tuvipange Vyuo vyetu Vikuu katika madaraja mbalimbali. Mifano imetolewa kwamba tuangalie nchi kama Marekani; ukiangalia Nchi ya Marekani, ukiangalia Nchi za Ulaya zenyewe zimeendelea sana katika mifumo yao ya elimu. Sisi katika Elimu ya Juu vyuo vyetu vingi bado ni vichanga na kwa maana hiyo Serikali ina wajibu wa kuvilea na kuhakikisha kwamba vinakuwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii tukianza kuweka madaraja ukasema kwamba Chuo Kikuu cha Dar es Salaam Daraja la Kwanza, ukasema labda kwa mfano, Chuo Kikuu cha Mzumbe sijui Daraja la Tatu, tayari utakuwa unawapa picha Watanzania kwamba hapa siyo mahali pazuri pakwenda; na ukianza kuangalia kwamba Serikali ina vyuo, sasa Serikali yenyewe ikianza kupanga vyuo na ni ukweli usiofichika kwamba tukipanga vyuo vya Seriakli ndiyo vitakuwa katika madaraja mazuri. Sasa kesho mtarudi hapa na kusema kwamba Serikali inanyanyapaa vyuo binafsi. Tuache Watanzania wenyewe wataamua kwamba waende wapi na ndiyo maana Serikali imetoa uhuru, hatuwapangii wanafunzi mahali pakwenda kusoma. Kila mwanafunzi yuko huru kuchangua Chuo anachotaka kwenda kusoma mwenyewe. Lakini tumeshuhudia vipo vyuo ambavyo vinapata tabu sana kupata Wanafunzi. Kwa hiyo tayari madaraja yamejipanga miongoni mwa Watanzania wanafahamu wapi wakienda watapata elimu iliyo bora.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia tumejaribu kuangalia uzoefu katika Nchi za wenzetu ambao wanapanga hayo madaraja. Kunakuwa na changamoto kwa sababu unapoweka madaraja kunakuwa na changamoto kama vile kuwepo kwa malengo na vigezo tofauti na vinavyotumika katika ushindani au kunakuwa na vyuo vinajikita zaidi katika yale maeneo ambayo yanajua kwamba ndiyo haya yanayotumika katika kuwapanga katika madaraja. Lakini pia katika Nchi za wenzetu, jukumu la kuvipanga vyuo katika ubora halifanywi na Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia katika nchi za wenzetu jukumu la kuvipanga vyuo katika ubora halifanywi na Serikali. Kwa hiyo, pia nishauri kwamba Kamati ya Makamu Wakuu wa Vyuo na Wakuu wa Vyuo Vishiriki hapa nchini wanaweza wakalichukua hilo jambo wakaliangalia lisiwe jambo la Serikali. Kama wataona inafaa, sisi Serikali hatuna tatizo lolote, lakini upande wa Serikali tukianza kupanga Vyuo vya Serikali vipo daraja la juu, vyuo vingine vinaweza vikafa ikaonekana kama vile kuna namna ambayo Serikali inasema kwamba huku hakufai.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jukumu la Serikali, tutaendelea kuhakikisha kwamba tunakagua na kujiridhisha kwamba vyuo vyote nchini vinazo sifa stahiki ambazo zinaruhusiwa kwa mujibu wa taratibu zilizowekwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo napenda kulizungumzia ni suala la Chuo Kikuu cha Mwalimu Julius Kambarage Nyerere ambacho Mheshimiwa Amina Makilagi alizungumzia, lakini na ndugu yangu Mheshimiwa Getere akampa taarifa ambayo alikuwa anachomekea, kweli ali shindilia, kwa hiyo, nimepokea maoni yenu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu, Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere na mwaka huu tunatimiza miaka 20 tangu ameondoka duniani, Serikali inamthamini sana na Serikali ina dhamira ya kumuenzi kwa kuanzisha Chuo cha Mwalimu Nyerere cha Kilimo kama ambavyo hata imeonesha katika Ilani ya Chama cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu sasa kwa sababu limeulizwa hapa Bungeni, ni bahati mbaya kwamba hiki chuo pamoja na kwamba kuna majengo ambayo yalitolewa, lakini yalitolewa kwa maneno, kama Serikali hatujapata hati za kukabidhi na Serikali imekuwa ikifanya kazi kubwa sana kufuatailia, lakini mpaka leo ninavyozungumza, hati miliki hazijapatikana. Kwa hiyo, nisingependa kulizungumza sana, lakini naomba wanaohusika nitoe wito wakamilishe taratibu haraka kwa sababu dhamira ya Serikali ya kuanzisha chuo hiki iko pale pale kama ambavyo imeainishwa katika ilani ya Chama cha Mapinduzi ya mwaka 2015/2020.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa noamba nizungumzie uimarishaji wa mazingira ya wanafunzi wenye mahitaji maalum. Suala la wanafunzi wenye mahitaji maalum Serikali inalichukulia kwa uzito mkubwa sana. Kwa kutambua matatizo makubwa ambayo yapo katika shule hizi na Waheshimiwa Wabunge wengi sana wamelizungumzia, Serikali imetenga kiasi cha shilingi bilioni 11.2 katika bajeti hii kwa ajili ya kununua vifaa visaidizi kwa ajili ya wanafunzi wenye mahitaji maalum.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kwa kutambua changamoto za ufundishaji, Serikali katika mwaka wa fedha 2018/2019 imeanzisha kozi ya stashahada katika Chuo cha Ualimu Patandi kwa ajili ya walimu wanafunzi wenye mahitaji maalum. Pia Serikali imejenga Shule Maalum ya Sekondari katika Chuo cha Walimu Patandi ambayo inaweza kuchukua wanafunzi 640.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine la kuhusiana na Wanafunzi Wenye Mahitaji Maalum ni kuhusu muda wa kufanya mtihani, kwamba ule muda wanaopewa hautoshelezi. Naomba niliarifu Bunge lako Tukufu kwamba Baraza la Mitihani la Tanzania huwa linatoa muda wa nyongeza kwa wanafunzi wenye mahitaji maalum na huwa linatoa dakika 10 za ziada kwa mitihani ya sanaa za jamii na dakika 20 za ziada kwa kila saa kwa somo la hisabati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ina maana kama ni mtihani wa masaa matatu, mwanafunzi mwenye mahitaji maalum atapewa masaa manne ya kuyafanya kwa sababu anaongezewa dakika 20 kwa kila saa ya mtihani na kwa masomo ya Arts anaongezewa dakika 10 kwa kila saa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme kwamba Serikali inawathamini sana watoto wenye mahitaji maalum. Kama muda huu ambao tunaongeza dakika 20 kwa kila saa, utaonekana hautoshi, sisi tuko tayari kufanya review, lakini kwa sasa naomba tutambue kwamba Serikali inaongeza muda kwa wanafunzi wenye mahitaji maalum, lakini hata mwaka 2017 Baraza la Mitihani lilifanya mapitio ya muundo wa mitihani kwa ajili ya wanafunzi wenye mahitaji maalum ili kuzingatia namna ya maswali ambayo yanaweza yakaulizwa kulingana na mahitaji maalum waliyonayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala la Sera ya Elimu na Mafunzo ambalo pia limezungumzwa na Waheshimiwa Wabunge wengi; na hususan ni suala la muda wa elimu kwamba je, elimu yetu ni miaka sita au saba?

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme kwamba nilishawahi kujibu katika Bunge lako Tukufu, naomba nirudie kusema tena. Muda wa Elimu ya Msingi ni miaka saba, haujabadilika. Kwa sasa hivi Serikali haina mpango wowote wa kubadilisha muda huo kwa sababu Serikali imejikita zaidi katika kutatua changamoto ambazo Waheshimiwa Wabunge mmezizungumzia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwamba mitaala yetu inaishia Darasa la Sita, siyo kweli. Mtaala wa Elimu ya Msingi ambao taasisi ya elimu imeutoa uko mpaka Darasa la Saba. Kwa hiyo, niwatoe hofu Waheshimiwa Wabunge kwamba watoto mwaka ule wa saba wataenda kucheza. Hakuna muda wa mchezo, hii ni Serikali ya kauli mbiu ya Hapa Kazi Tu; na kazi ya mwanafunzi ni kusoma. Kwa hiyo, hata wanafunzi nao watasoma darasa la saba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala la Vyuo vya Ufundi Stadi (VETA). Nikiri kwamba katika vyuo hivi kumekuwa na ahadi za muda mrefu na hata imekuwa kero kwa baadhi ya Waheshimiwa Wabunge kila siku wanakuja kuuliza maswali Bungeni kuhusiana na vyuo vyao. Wanahoji kwamba sasa je, Serikali ina dhamira kweli ya kujenga Vyuo vya Ufundi Stadi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niseme kwamba dhamira ya Serikali iko pale pale na sasa hivi dhamira iko kubwa zaidi kwa sababu tunajenga uchumi wa viwanda. Tunapojenga uchumi wa viwanda tunahitaji mafundi stadi na mafundi mchundo wengi zaidi. Kwa hiyo, dhamira ya Serikali ya kutekeleza sera ya kujenga VETA katika mikoa na Wilaya iko pale pale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ambavyo nimesema, kupitia fedha ambazo nasikitika sana kwamba wengine wanatumia maneno mabaya ya kuzungumzia kwa Washirika wetu wa Maendeleo, Serikali imeamua na inakwenda kufanya. Kwanza sasa hivi tunaendelea na ujenzi wa VETA Mkoa wa Rukwa na Geita, tunakamilisha maandalizi ya ujenzi wa VETA kwa Mikoa ya Njombe, Simiyu na Kagera. Pia Serikali imekamilisha VETA ya Wilaya ya Namtumbo; na sasa hivi tuko katika hatua za ukamilishaji na usimikaji wa vifaa katika Wilaya ya Ileje, Nkasi, Urambo, Newala, Muleba na Simanjiro.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Serikali inaendelea kukamilisha matayarisho ya VETA Wilaya ya Itilima, Kasulu Halmashauri ya Wilaya, Babati na Ngorongoro. Pia Serikali inakamilisha kupata wataalam elekezi kwa ajili ya kujenga VETA katika Wilaya ya Ruwangwa, Kongwa, Halmashauri ya Mji wa Kasulu na Nyasa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumaeamua katika bajeti yetu ya mwaka 2019/2020 Serikali imetenga jumla ya shilingi bilioni 40 na tunakwenda kujenga VETA katika Wilaya zifuatazo: Chunya, Kilindi, Korogwe, Ukerewe, Chemba, Igunga, Pangani, Kishapu, Rufiji, Uyui, Kwimba, Bahi, Mafia, Longido, Mkinga, Uvinza, Ikungi, Iringa Vijijini, Lushoto, Mbarali, Monduli, Buhigwe, Ulanga, Masasi na Butiama.

Waheshimiwa Wabunge, mnataka nini tena ndugu zangu? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niseme tu kwa kweli kwa sababu ya muda kama nilivyosema, nisingependa unifukuze kwa kengele, lakini niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge wote kwamba sisi tumepokea maoni yenu lakini labda sambamba na hili la Vyuo vya Mafunzo ya Ufundi Stadi kumekuwa na maombi ya Waheshimiwa Wabunge kubadilisha Vyuo vya Maendeleo ya Wananchi kuzifanya ziwe VETA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwaombe tu Waheshimiwa Wabunge kwamba Vyuo vya Maendeleo ya Wananchi vimeanzishwa kwa malengo mahususi, kwa hiyo, Serikali isingependa kuvibadilisha. Tutashirikiana na Wajumbe katika maeneo husika, kama kutakuwa na fedha, kwa sababu hata hizi Wilaya ni kwa kuanzia, lakini zoezi la kuendelea kujenga VETA katika Wilaya litakuwa endelevu. Kwa hiyo, tutaweza kuwasiliana na katika maeneo ambayo tutakuwa tumeyafanyia tathimini kwa kuangalia taratibu ambazo tunazitumia, basi hakuna dhambi yoyote ukiwa na Chuo cha Maendeleo ya Wananchi na ukawa pia na vhuo cha VETA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tutakarabati Vyuo vyote vya Maendeleo ya Wananchi na pia tutaboresha mafunzo yake lakini suala la VETA na Vyuo vya Maendeleo ya Wananchi ningeomba sana Waheshimiwa Wabunge tuache kama vitu viwili tofauti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimalizie tena kwa kuwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge wote kwa kweli kwa michango mizuri ambayo wameitoa. Niwahakikishie kwamba Serikali hii katika mambo ya elimu, kama kuna vitu ambavyo Mheshimiwa Rais ameviweka katika kipaumbele, ni elimu. Mumsikilize, mahali popote anapoongea, hawezi akamaliza kuzungumza bila kuzungumzia masuala ya elimu. Hazungumzi maneno tu, lakini hata fedha tunapata.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, katika mwaka kwa fedha ulioisha 2017/2018, mpaka kufika Juni, 2018 tulipata bajeti ya maendeleo kwa asilimia 86 na tulipata bajeti ya matumizi mengineyo kwa asilimia 107, yaani tulipata zaidi ya kile kiasi ambacho kimetengwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kama alivyosema Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango, ninayo imani kubwa sana na Serikali kwamba katika kipindi hiki cha miezi miwili iliyobaki, Wizara ya Fedha itaendelea kutoa fedha kwa miradi ambayo ilitengewa fedha lakini mpaka sasa haijapata ili kuhakikisha kwamba tunaweza kufikia malengo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nimalizie pia kwa kuishukuru familia yangu kwa kuendelea kuniunga mkono; nimshukuru mwanangu Dajosi ambaye yuko hapa pamoja na mdogo wangu Benjamini Ndalichako. Nawashukuru sana Washirika wetu wa Maendeleo ambao wamekuwa nasi katika Bunge hili tangu jana tulipowasilisha hoja hii. Naomba tu waelewe kwamba kuna lugha za Kibunge. Kwa hiyo, Waheshimiwa Wabunge wote wanathamini michango yao na ninaomba waendelee kushirikiana na Serikali kuiunga mkono nchi yetu katika sekta ya elimu ili iweze kusonga mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nitoe shukurani za dhati sana kwa Watanzania wote wenye mapenzi na mema na Sekta ya Elimu ambao wamekuwa wakinipa maoni na ushauri mbalimbali ambayo yamekuwa chachu ya kuboresha elimu yetu. Niwahakikishie kwamba nitaendelea kuwa napokea maoni yenu na mnivumile wakati mwingine unakuta una message zaidi ya 350, siyo rahisi kuyapokea kwa wakati mmoja, lakini huwa najitahidi kusoma na kufanyia kazi kile ambacho mnanishauri kwa maslahi ya nchi yetu. Kwa hiyo, naomba msichoke kutoa ushauri na Wizara yangu itaendelea kulipokea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge wamezungumzia sana suala la mfumo wa elimu na kuwa na mjadala. Kama ambavyo wenzetu wa madini wamefanya kwa kukutana na wadau wao, naomba nimwagize Katibu Mkuu wangu aangalie uwezekano wa kuwa na mkutano mkubwa wa wadau wa Sekta ya Elimu ili tuweze kupata mawazo yao. Hakuna tatizo lolote. Serikali ipo tayari kusikiliza na iko tayari kufanyia kazi mawazo ya Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nawashukuru sana ndugu zangu wa Mkoa wa Kigoma, ndugu zangu wa Wilaya ya Kasulu ambao wamekuwa wakinitia moyo katika jukumu langu la Kitaifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa, nawaomba Waheshimiwa Wabunge wote waunge mkono bajeti hii ili tuweze kwenda mbele, tuweze kuchapa kazi, tuweze kuendeleza elimu katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya maelezo hayo, naamini kwamba Waheshimiwa Wabunge wote wataunga mkono bajeti hii kwa sababu elimu haina itikadi, watoto wote wa Kitanzania wanastahili kupata elimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya maelezo hayo, naomba kutoa hoja. (Makofi)

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naafiki.