Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Hon. Eng. Edwin Amandus Ngonyani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Namtumbo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

MHE. ENG. EDWIN A. NGONYANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja ikiwa ni pamoja na zifuatazo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsanteni sana na kwa kumwalika Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kuja kukifungua Chuo cha VETA cha Namtumbo na hivyo kukipandisha hadhi. Nawaomba mkamilishe nyumba za walimu na mabweni ya wanafunzi ili chuo kianze kutoa mafunzo bila kusahau vifaa vya kufundishia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, fedha mlizotoa kuunga mkono ujenzi wa Shule ya Msingi ya Miembeni katika Kijiji cha Likuyu Mandela ni shilingi milioni 180 na shule ya kisasa kabisa imekamilika kujengwa na imeanza kutumika. Ahsanteni sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu usimamizi thabiti wa Sera ya kila Kata kuwa na Sekondari moja ya kutwa, sera hii imewezesha Wilaya ya Namtumbo kuwa na Sekondari 23 katika Kata 20. Ni Kata moja tu haina Sekondari kutokana na kuanzishwa hivi karibuni (Kata ya Msisima). Tuombe tu, shule hizi za kutwa zinahudumia Vijiji na Vitongoji vilivyosambaa kwa zaidi ya kilometa 5 - 26 na hivyo kulazimika wanafunzi kupanga ama kuwa na mabweni katika shule hizo kinyume na madhumuni ya kuanzishwa kwa shule hizo za kutwa. Mazingira hayo tuomba yavumiliwe badala ya kupigwa vita na Idara ya udhibiti ubora wa elimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Bodi ya Mikopo imeundwa na inafanya kazi vizuri. Hongereni sana, maana Bodi hii imefanikiwa kuwahudumia baadhi ya wanachuo wenye uhitaji. Katika eneo hili nampongeza sana Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Mheshimiwa William Tate Olenasha, kwa kazi kubwa anayoifanya ya kufuatilia wanachuo wenye uhitaji mkubwa wa mikopo katika Wilaya ya Namtumbo na nchi nzima kwa ujumla ambao kwa namna moja ama nyingine vigezo vilivyowekwa na Bodi na njia inayotumika, uthibitishaji wa vigezo hivyo vinaifanya Bodi kuwakosa wenye uhitaji na kuwapa wasio nao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Naibu Waziri anatusikia Wabunge na ni mwepesi wa kufuatilia taarifa tunazompa na pale inapothibitika kuwa haki haikutendeka, huirejesha haki kwa mhusika. Hakika unaye msaidizi mwenye hekima ya Mfalme Suleiman anayetajwa katika Biblia na anaitendea haki taaluma yake ya Sheria. Hongera sana Profesa Joyce Lazaro Ndalichako na kupitia kwako tumshukuru sana Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kukuibua wewe na Naibu wako na kuwakabidhi uongozi wa Wizara hii nyeti ya Elimu, Sayansi na Teknolojia katika kipindi hiki muhimu cha mustakabali wa Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ziko sababu nyingi, itoshe kuishia hapa, naomba sana Mheshimiwa Waziri atusaidie katika haya yetu wana-Namtumbo:-

(a) Tukamilishiwe ujenzi wa Chuo cha VETA cha Wilaya ya Namtumbo;

(b) Tuondolewe waraka unaozuia ujenzi wa mabweni katika shule zetu za Sekondari za kutwa;

(c) Turekebishiwe mfumo unaotumika katika kuwapa wahitaji wa mikopo kutoka HESLB ili wahitaji halisi wasiachwe solemba na kukatisha ndoto zao za kutaka kujiendeleza kielimu;

(d) Naomba Chuo cha Ualimu kinachomilikiwa na SONAMCU kilichoko katika Kijiji cha Nahoro kiwezeshwe kuendelea kutoa huduma; na

(e) Naomba ukarabati wa Chuo cha Maendeleo ya Jamii cha Mputa ufanyike kwa wakati uliopangwa ili u- yatima wa chuo kile ufutike mioyoni mwa wanafunzi na Walimu wa chuo hicho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawasilisha. Naunga mkono hoja hii ya Mheshimiwa Waziri, Prof. Joyce Lazaro Ndalichako, Mbunge kwa asilimia mia moja.