Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Hon. Shabani Omari Shekilindi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lushoto

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

MHE. SHAABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa, nampongeza Mheshimiwa Waziri pamoja na timu yake kwa kazi kubwa wanayoifanya katika kuwatumikia Watanzania. Ninaishukuru Serikali yangu Tukufu kwa kupata mgao wa walimu katika Halmashauri ya Wilaya ya Lushoto. Kama ujuavyo, Lushoto ni eneo lenye milima na mabonde na miundombinu yake siyo rafiki. Kwa hiyo, zipo changamoto nyingi mno za kielimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja, walimu waliopangiwa Wilaya ya Lushoto katika Halmashauri ya Lushoto ni wachache sana kwani hawaendani na shule zilizopo katika Halmashauri ya Lushoto. Ukizingatia Lushoto kuna shule nyingi za msingi na sekondari zaidi ya 100 na zaidi. Kwa hiyo, naisihi Serikali yangu sikivu ituongezee walimu ili kuondoa zero katika shule zetu, kwani Lushoto tumekuwa hatufanyi vizuri lakini sababu kubwa ni ukosefu wa walimu. Kwa hiyo, kutotupa walimu wa kutosha ni kufanya watoto wetu waendelee kufeli. Naomba Lushoto iangaliwe kwa jicho la huruma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wa Lushoto ni watu wanaojituma sana katika msaragambo, hasa wa kujenga maboma ya shule za msingi pamoja na sekondari. Wananchi wale wanakata tamaa kwani majengo mengi yamejengwa na kufikia usawa wa lenta lakini majengo yale mpaka sasa hivi hayajaezekwa na nguvu za wananchi kuharibika bure. Hii inawakatisha tamaa wananchi wetu. Kwa hiyo, naiomba Serikali ipeleke fedha kwa ajili ya kumaliza maboma yale yanayotokana na nguvu za wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo, kuna changamoto za mabweni katika sekondari zetu. Lushoto kuna sekondari zaidi ya 20 hazina mabweni na hii pia inachangia sana watoto wetu kufeli, hasa kwa hawa watoto wetu wa kike kupata ujauzito na kushindwa kuendelea na masomo yao. Kwa hiyo, naiomba Serikali yangu itujengee mabweni hasa katika shule za Gare Secondary, Mgambo Secondary, Malibwi Secondary, Kwemashai Secondary, Balozi Mshangama Secondary, Mdando Secondary, Mkunzi Juu Secondary; Prince Clous Secondary, Lushoto Secondary, Kitala Secondary, Ngwelo Secondary na Mariam Mshangama Secondary. Shule zote hizi hazina mabweni. Kwa hiyo, naiomba Serikali yangu ilione hili ili tuweze kuboresha elimu katika Jimbo la Lushoto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto nyingine ni kupandisha madaraja walimu wetu pamoja na kuwapa motisha, kwani walimu wanafanya kazi kubwa sana. Pia waboreshewe miundombinu ya nyumba zao, hasa ukizingatia Wilaya ya Lushoto shule nyingi zipo vijijini sana ambako hakuna mazingira rafiki ya kuishi watumishi wetu hawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Lushoto ni Wilaya kongwe, kwani wilaya hii ni ya tangu Mkoloni, lakini mpaka sasa hakuna Chuo cha VETA. Kwa hiyo, hii imechangia kurudisha watoto wetu nyuma, hasa wale wanaomaliza Darasa la Saba pamoja na wale wanaomaliza Kidato cha Nne. Hili limekuwa ni kundi kubwa linaloongezeka siku hadi siku. Kwa hiyo, naiomba Serikali yangu sikivu itujengee Chuo cha VETA katika Jimbo la Lushoto ili watoto wetu waweze kupata stadi za maisha. Sambamba na hilo, nimependekeza Jimbo la Lushoto kijengwe Chuo cha VETA kwani ndiyo katikati ya majimbo yote matatu ya Wilaya ya Lushoto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna hizi shule shikizi, naiomba Serikali yangu sikivu iweze kusajili shule hizi, hata kama ina vyumba vinne. Nayasema hayo kwa kuwa wananchi wakiamua kuanzisha jambo lao huwa halirudi nyuma. Mfano, katika Jimbo la Lushoto nina shule shikizi mbili; Mgambo Primary School na Kaghambe Primary School. Shule hizi mpaka sasa zina vyumba sita, kwa hiyo, niombe shule hizi zisajiliwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja kwa asilimia 100.