Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Hon. Nuru Awadh Bafadhili

Sex

Female

Party

CUF

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

MHE. NURU A. BAFADHILI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimshukuru Mungu kwa kuniwezesha kuchangia hotuba iliyopo mbele yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuzungumzia kuhusu walimu. Zamani unapoingia chuoni unaambiwa ualimu ni wito kama Padre, Askofu au Shekhe. Hii iliwafanya wote wanaochukua mafunzo ya ualimu kuwa na nidhamu katika kazi yao. Sasa hivi tuna walimu ambao wengine hawastahili kuitwa au kuwa walimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwalimu anatoka shuleni badala ya kurudi kule anakoishi moja kwa moja anakwenda kwenye vilabu vya pombe. Kule analewa kiasi kwamba anakuwa hajitambui hususan walimu wa kiume. Anapita mitaani anayumba watoto ambao wengine ni wanafunzi wake wanamsindikiza kwa kumzomea. Hii inashusha hadhi ya mwalimu na ualimu kwa ujumla.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nielezee kuhusu walimu kupata mafunzo ya mara kwa mara (refresher courses) wakati wanapokuwa likizo. Hii itawasaidia walimu kwenda na wakati uliopo kwa maana pengine kuna mabadiliko ya mitaala.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuzungumzia kuhusu utoro wa watoto kwa baadhi ya shule. Kuna sababu mbalimbali zinazosababisha utoro kwenye shule zetu. Moja, ni ukosefu wa walimu. Kuna baadhi ya shule hususan shule za vijijini utakuta kuna madarasa saba lakini walimu wanne tu, pale lazima kuwepo na utoro. Pili, watoto kwenda shuleni wakiwa na njaa kwani mtoto mwenye njaa hafundishiki. Tatu, ukosefu wa uzio katika shule kadhaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nini kifanyike? Nashauri shule ziwe na walimu wa kutosha katika madarasa. Pia shule ziwe na utaratibu wa kuwapikia wanafunzi angalau uji ili waweze kukaa madarasani na kusikiliza mafundisho wanayopewa. Shule nyingi hazina wigo ni rahisi wanafunzi kutoroka na kupotea mitaani kwenda kuungana na wale ambao wana tabia mbaya. Kwa hiyo, Serikali ione umuhimu wa kujenga uzio katika shule zetu hapa nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, nashauri shule za msingi zifundishe masomo ya ufundi kama useremala, uashi, ushonaji, upakaji nyumba rangi na kadhalika. Serikali ianzishe karakana za kufundishia ufundi huo ili kuwaandaa wanafunzi wale wanaokosa nafasi ya kujiunga na elimu ya sekondari waweze kujiajiri au kujiendeleza katika vyuo vya VETA na kupata ujuzi mzuri na kujiajiri ili kupunguza wimbi la wazururaji.