Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Hon. Joseph Leonard Haule

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Mikumi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

MHE. JOSEPH L. HAULE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa nafasi ili na mimi niweze kuchangia kwenye Wizara hii muhimu kwa ustawi wa Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, elimu bure (bila malipo). Kumekuwa na ongezeko kubwa sana la wanafunzi katika kujiandikisha kujiunga na shule mbalimbali lakini kuna tatizo kubwa sana la miundombinu kwani miundombinu imezidiwa na idadi kubwa ya wanafunzi wanaojiunga na elimu msingi, mfano, vyoo, madarasa, ofisi za walimu na nyumba za walimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia pamoja na idadi ya wanafunzi kuongezeka lakini kuna uhaba mkubwa sana wa walimu kwani uwiano wa wanafunzi na walimu kwenye shule zetu haulingani kabisa. Hivyo basi inapelekea ile dhamira njema ya kukuza na kusaidia kila mwenye uwezo wa kwenda shule aende shule isiwe na tija kwa maana uchache wa walimu unadumaza hiyo nia njema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, upatikanaji wa fedha za miradi na maendeleo. Tumekuwa tukipitisha fedha na bajeti mara kwa mara lakini cha kusikitisha ni kwamba fedha za kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo zimekuwa zinatolewa kwa asilimia ndogo sana. Niiombe sana Serikali iwe inatoa fedha zinazopitishwa na Bunge lako Tukufu ili kuweza kufikia yale malengo ambayo Wizara na Serikali kwa ujumla zinakuwa zimejiwekea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, uhaba wa walimu. Tumekuwa na upungufu mkubwa sana wa walimu nchini. Mfano kwa wilaya ya Kilosa peke yake, kwenye upande wa shule za msingi, tuna wanafunzi 107,000 lakini tuna walimu 2,393 kwa hiyo tuna upungufu wa walimu 929. Nitumie nafasi hii kuiomba sana Serikali itusaidie kwa kutuongezea walimu zaidi kwenye shule za msingi Wilayani Kilosa. Pia ituongezee walimu wa sayansi kwenye Wilaya yetu ya Kilosa kwani napo tuna upungufu mkubwa sana wa walimu wa sayansi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH). Ni vyema sana Serikali ikaona umuhimu wa COSTECH ili tuweze kusaidia Taifa letu kwenye masuala ya ubunifu wa mambo mbalimbali kwenye nchi yetu. Tanzania tumebarikiwa sana kuwa na watu mbalimbali wanaovumbua vitu vingi lakini tuna tatizo kwa COSTECH kushindwa kuwafikia na kuwasaidia kutokana na ufinyu wa bajeti. Bila bajeti ya kueleweka COSTECH haiwezi kuvumbua, kubuni na kusaidia vipaji mblimbali ambavyo kama vingeweza kusimamiwa ipasavyo vingeweza kutuletea maendeleo makubwa sana na kututoa kimasomaso kama Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.