Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Hon. Daimu Iddi Mpakate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduru Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

MHE. DAIMU I. MPAKATE: Mheshimiwa Mwenyeiti, ninapenda kuchangia hotuba ya Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia kama ifauatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jimbo la Tunduru Kusini kuna shule za Kata nane na tunategemea kuongeza shule mbili za sekondari ya Misechela na Tuwemacho jumla 10 katika kata 15. Changamoto kubwa ya shule hizo ni za kutwa tunalazimika wanafunzi kuwalaza madarasani kutokana na umbali wa vijiji wanavyotoka watoto hai hivyo madarasa haya mchana na usiku mabweni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo basi, tunaomba Serikali kutusaidia kujenga mabweni katika shule hizo ili kupunguza kero za wanafunzi hao kutembea kilomita nyingi kufuata shule na uwezo mdogo wa wazazi kuwapangia watoto wao nyumba za kuishi. Changamoto nyingine ni upungufu wa madarasa kutokana na idadi kubwa ya watoto wanaofaulu kwenda kidato cha kwanza kipindi cha sera ya elimu bila malipo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto nyingine ni upungufu wa maabara ya sayansi. Tunashukuru Serikali na wananchi kwa kujitolea kujenga maabara ya masomo ya sayansi. Lakini pamoja na jitihada hizo bado majengo hayo hayajakamilika kwa kupewa vifaa vya maabara. Kwa hiyo tunaomba Serikali kutoa vifaa vya maabara ili kuzifanya maabara zile zifanye kazi ipasavyo sambamba na upungufu wa maabara kuna upungufu mkubwa wa walimu wa sayansi kwa masomo ya fizikia, kemia, biolojia na hesabu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba Serikali iendelee na jitihada za kuajiri walimu wa sayansi angalau kila somo apatikane mwalimu mmoja ili kuweza kuwafundisha watoto wetu katika teknolojia mpya ya sayansi na teknolojia. Changamoto nyingine ni kwamba katika shule hizo zote hamna shule yoyote ya high school jambo ambalo linalozimisha wanafunzi wengi kukosa kuendelea na masomo ya high school. Hivyo ninaomba angalau tupate high school mbili kwa kuanzia shule ya sekondari Semeni na shule za sekondari Mchoteka ili kuongeza idadi ya wanafunzi wanaokwenda high school.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changanoto nyingine ni kutokuwa na chuo cha ufundi kwa ajili ya kuendeleza vipaji vya wanafunzi. Hivyo ninaomba fursa itakayopatikana chuo cha ufundi kijengwe katika Jimbo la Tunduru Kusini hususani katika Kata ya Mtina ambako mahitaji makubwa muhimu na ya kutosha yapo, kama vile ardhi, maji safi na barabara inayopatikana wakati wote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, VETA ni muhimu sana ili kuendeleza vijana wetu wanaomaliza darasa la saba na kidato cha nne na cha sita ambao wanakosa nafasi za kuendelea mbele kimasomo. Changamoto nyingine ni la nyumba za walimu ambapo walimu wengi wanakaa kwenye nyumba za kupanga vijijini. Tukumbuke kwamba shule zote hizi zipo vijini ambapo huduma ya nyumba za kupanga si nzuri sana wanalazimika kupanga ili waishi. Ni vyema Serikali kuona umuhimu wa kujenga nyumba za walimu ili kupunguza kero.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho ni mikopo kwa walimu. Kwa kuwa kipato cha walimu ni kidogo ninaomba Serikali kuona namna ya kuwakopesha usafiri hasa pikipiki ili waweze kujikimu pindi wanapotaka kusafiri kwenda mjini kufuata mahitaji pamoja na mishahara. Walimu wengi wana madai mengi kwenye mabeuli SACCOS jambo ambalo linawafanya waishi katika mazingira magumu sana na kushindwa kufanya kazi vizuri. Hivyo ninaomba mishahara ya walimu iongezwe pamoja na kupewa fursa ya kukopeshwa na Serikali kwa riba nafuu kama zile za vijana akinamama na walemavu ili kuwapunguzia mzigo wa kukopa kwa riba kubwa.