Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Hon. Dr. Stephen Lemomo Kiruswa Mamasita

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Longido

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote natoa pongezi kwa Waziri Mheshimiwa Profesa Joyce Ndalichako, Naibu Waziri Mheshimiwa William Ole Nasha, Katibu Mkuu na timu nzima ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kwa kazi nzuri na kwa hotuba hii nzuri iliyosheheni miradi mingi iliyotekelezwa mwaka huu 2018/2019. Baada ya pongezi hizi naomba sasa nichangie hoja kwa kutoa maoni na ushauri wangu kwa Serikali, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Miundombinu; ukarabati wa Taasisi za Elimu; naishauri Serikali isiishie kukarabati vyuo na shule kongwe tu bali itenge fedha za ukarabati wa shule zake zote kila mwaka wa fedha. Kwa suala la shule kongwe, Wilayani Longido sisi tuna shule kongwe za msingi zilizojengwa tangu enzi ya ukoloni. Kwa mfano tuna shule ya bweni ya msingi ya Longido ambayo ilijengwa mwaka 1947 na majengo yake yamekuwa chakavu, hivyo inastahili kukarabatiwa na Serikali. Hii ndiyo shule ya msingi aliyosoma hayati Edward Moringe Sokoine, aliyekuwa Waziri Mkuu wa Tanzania wakati wa Serikali ya Awamu ya Kwanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mitaala; Taasisi ya Elimu Tanzania; suala la Mitaala, Miongozo na Vitabu; Serikali ijumuishe shule za awali katika mipango yake ya kuandaa mitaala, miongozo na kuchapa vitabu vya kiada na rejea. Msingi wa elimu bora huanzia ngazi ya elimu ya awali na si darasa la kwanza na kuendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mamlaka ya Elimu ya Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA); nashauri Serikali iongeze kasi ya kuanzisha VETA katika kila wilaya nchini. Kwa kuwa, Wilaya ya Longido hakuna chuo chochote cha Serikali na tuna ardhi ya kutosha na kwa sasa tuna maji safi na salama ya kutosha pamoja na umeme Makao Makuu ya Wilaya na vijiji jirani, naikaribisha Wizara watujengee VETA ya Taifa inayolenga fani zifuatazo: Mifugo (livestock production & livestock products), wanyamapori (wildlife nature conservation & tourism), madini (small scale mining skills), huduma za kitalii (Hospitality & Hotel Management), Uashi na useremala, TEHAMA na kadhalika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na uanzishwaji VETA kila wilaya, nashauri Serikali ianzishe chuo mahsusi cha Walimu wa sayansi, ili kuziba pengo la uhaba mkubwa tulionao wa Walimu wa sayansi katika shule zetu za sekondari na vyuo. Kwa kuwa, sisi Longido tuna ardhi, maji na umeme naikaribisha Serikali ijenge chuo hicho Wilayani Longido na kiitwe Tanzania Science Teachers’ College. Chuo hiki kitakuwa ndio kiwanda cha kuzalisha Walimu wa fani zote za sayansi kwa ajili ya mahitaji ya nchi yetu katika ngazi zote husika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu; naipongeza Serikali kwa ongezeko la wanafunzi wanaopewa mikopo ya elimu ya juu. Naomba kuishauri Serikali itoe elimu ya jinsi ya kuzaja fomu kwa usahihi katika kila shule yenye wanafunzi wanaostahili kupewa mkopo ili kuondoa tatizo lililopo la baadhi ya wanafunzi wenye sifa kukosa mikopo kwa sababu ya kutojua jinsi ya kujaza fomu za maombi kwenye mitandao kwa usahihi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, naomba niiangalize Serikali kuhusu suala la uwepo wa vijiji vichanga nchini ambavyo bado havina shule za msingi sambamba na huduma zingine muhimu za kijamii kama zahanati, barabara, mawasiliano ya simu, maji na umeme. Kwa mfano, katika Wilaya ya Longido yenye jumla ya vijiji 49, tuna vijiji kadhaa ambavyo havina shule na hivyo, kuna idadi kubwa ya watoto ambao hawaendi shule. Baadhi ya Vijiji hivyo katika Wilaya ya Longido ni pamoja na Engusero (Kata ya Naondoto), Nadaare (Kata ya Iloirienito), Wosiwosi (Kata ya Gelei Lumbwa), Leremeta (Kata ya Sinya) na Loondolwo (Kata ya Meinigoi). Naiomba Serikali itenge fedha za kuwaunga mkono wananchi kwa kuwachochea kuanzisha shule za awali na msingi katika vijiji hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja.