Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Hon. Joseph Michael Mkundi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ukerewe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, mahitaji ya Chuo cha Ufundi Stadi Mkoani Ukerewe, ongezeko kubwa la vijana wanaomaliza elimu ya msingi na sekondari usioendana na uwepo wa miundombinu wezeshi kwenye taasisi za elimu umeathiri sana ufaulu wa vijana wetu. Hivyo ukichangiwa na jiografia ya Visiwa vya Ukerewe vijana wengi wamekuwa wanaona kuwa uvuvi ndiyo suluhisho lao kimaisha, hali hii imepekelekea uharibifu wa mazingira na uvuvi usio endelevu kwa sababu tu ya kukosa njia mbadala ya kuwawezesha kukabiliana na changamoto za maisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hali hii uwepo wa Chuo cha Ufundi Stadi (VETA) katika Visiwa vya Ukerewe kutasaidia kwanza kuandaa vijana wetu kuelekea kwenye nchi ya viwanda, kuwaandaa vijana kuwa na fikra za kujiajiri kiufundi zaidi badala ya fikira za kuajiriwa hali ambayo imekuwa inapelekea kutumia muda mwingi kutafuta kazi badala ya kujiajiri na kupunguza uvuvi haramu unaotokana na wimbi kubwa la vijana kuamini katika uvuvi tu, kumbe kupitia ufundi wangeweza kufanya shughuli nyingine za uzalishaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, umuhimu wa kuruhusu vijana kurudia shule hasa elimu ya msingi. Maeneo ya vijijini ambapo kutokana na mazingira, vijana wengi wamekuwa wanamaliza elimu ya msingi katika umri mdogo lakini pia wakiwa na uwezo mdogo kitaaluma hali ambayo huwapa mazingira magumu sana wazazi au walezi wa watoto hawa. Hivyo, iwapo Wizara itaruhusu watoto hawa kurudia shule, itawasaidia kuimarika kitaaluma na kukomaa kiakili kabla ya kuingia katika hatua inayofuata ya elimu ya sekondari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, umuhimu wa washauri kwa watoto pale wanapohitaji kuchagua masomo (mchepuo). Vijana wengi wamekuwa wanachagua masomo kwa mkumbo tu ama fasheni na baadaye hugundua kuwa hawakuwa wamefanya chagua sahihi. Hii ni kutokana na kukosa ushauri wakati wa uchaguzi wa masomo. Hivyo, ni muhimu Serikali kupitia Wizara kuhakikisha kunakuwa na Walimu washauri kwenye mashule yote ili kusaidia kuwashauri vijana pale ambapo wanahitaji kufanya uchaguzi wa masomo ya kitaaluma.