Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Hon. Susan Anselm Jerome Lyimo

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

MHE. SUSAN A. J. LYIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa nafasi. Leo nitachangia kwa masikitiko makubwa sana hasa nikikumbuka kwamba mwaka jana wakati kama huu nilikuwa na Naibu wangu Mheshimiwa Mwalimu Bilago, lakini leo hatunaye, kwa hiyo napenda tu niseme kwamba nina masikitiko makubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kunukuu Mwanasayansi maarufu wa Kijerumani Bwana Albert Eisten, ambaye alisema:

“Dunia itaharibiwa sio na watenda mabaya bali kwa ukimya wa watu wema wakati maovu yanatendeka.” (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara ya Elimu ina wasomi wengi kuliko Wizara zote Tanzania. Kwenye Kamati yetu ambayo mimi ni mjumbe imejaa Maprofesa ambao ndiyo ambao wanakaa kimya wakati wanaona mfumo wetu wa elimu unaharibika. Vilevile Maprofesa hao wanaongozwa na Profesa Ndalichako ambaye naamini ni msomi mzuri lakini hatuoni mfumo wa elimu ukibadilika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, elimu ni kama kiwanda, hauwezi ukapeleka muwa kiwandani ukatoka muwa lazima utoke sukari. Leo hii wanafunzi wanaanza nursery mpaka anamaliza darasa la saba hajui kusoma wala kuandika, amepoteza miaka yote saba. Ndiyo sababu naunga mkono alichokisema mzee Kishimba pale kwamba sasa hivi elimu badala ya kuwa ufunguo wa maisha umekuwa kifungo cha maisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, tunapoongelea elimu lazima tuongelee ubora wa elimu. Leo ambapo Sera ya Elimu ya mwaka 1995 ambayo ndiyo inatuongoza inatoa mitaala na vitabu tumeipigia kelele kwamba imepitwa na wakati lakini imekuja Sera ya mwaka 2014 ambayo hata miaka minne (4) haijaisha tayari inaanza kufanyiwa maboresho. Waziri anatumbia kwamba inafanyiwa maboresho kwa sababu haikupita kwa wadau, haiingii kichwani kwa sababu gani haikupitishwa kwa wadau?

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado tunatumia sheria ya mwaka 1978 ambayo ilitumika kwenye Sera ya mwaka 1995 na inaendelea kutumika kwenye Sera ya 2014. Mimi binafsi najua kwamba huwezi kuwa na sheria bila kuwa na sera na kwa maana hiyo sera inapotengenezwa ndiyo unakuja kutengeneza sheria.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Sera ya mwaka 2014 imesema bayana kwamba watoto watasoma mpaka darasa la sita halafu baada ya hapo wote wataenda sekondari, ndiyo tunaita elimu msingi lakini leo hawaitekelezi. Waziri ukimuuliza atakwambia kwa sababu sheria haijabadilika then tunauliza which come first sheria au policy? Kwa hiyo, wakubali kwamba walizembea na hayo mabilioni ya pesa yaliyotumika kutengeneza hiyo Sera ya 2014 watuambie kodi za wananchi kwa nini zinatumika bila wao kuwa na mkakati maalum wa kuhakikisha wanapotengeneza sera wanaenda kwanza kuijaribisha halafu baadaye ndiyo inakuwa sera kamili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukizungumzia suala la ubora wa elimu, baada ya hiyo Sera sasa kuwa na matatizo, wamekuwa na miongozo na mambo mengi sana. Kwa mfano, ukisikiliza Waraka Na. 5 na wakati huo nadhani Kamishna wa Elimu alikuwa Profesa, nimesahau jina lake alikuwa Profesa Balalusesa. Unaposema mwanafunzi hawezi kufukuzwa shule mpaka amekuwa mtoro kwa siku 90 mfululizo siku za week days, hii ina maana miezi minne kamili kwa sababu kama ni mwezi mmoja una siku 22 za kwenda shule times 4 yaani miezi minne huyu mtoto akienda kwa mfano siku ya 86 bado hafukuzwi. Halafu Waraka huu uwe applicable pia kwenye shule za private, haiwezekani. Hakuna mwalimu mwenye shule yake ya private atakayeruhusu upuuzi wa namna hii. Haya mambo ndiyo sababu tunasema Tanzania mimi huwa sielewi tunaelekea wapi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine wanasema kwamba mwanafunzi hawezi kufukuzwa mwaka anaofanya mtihani wa kumaliza shule. Ina maana kama uko darasa la saba, form four, form six huwezi kufukuzwa. Sasa na hii imepelekea kuporomoka kwa maadili kwa sababu mwanafunzi wa form four au form six akijua anafanya mitihani anaweza hata akaamua kumpiga mwalimu kwa sababu anajua hatafukuzwa mpaka Mahakama ithibitishe, hiyo Mahakama inathibitisha saa ngapi. Kwa hiyo, kuna mambo ambayo tunadhani hayajakaa sawasawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikitoka hapo nije sasa kwenye matatizo makubwa ya walimu. Hapa nina barua ya mmoja wa walimu hajapandishwa daraja toka mwaka 2003 amekuja kupandishwa juzi yaani mwezi huu wa nne ndiyo amekuja kulipwa mshahara wa kwanza kwa kupandishwa cheo toka 2003 anapokea Sh.140,000 mpaka juzi amekuja kupokea shilingi milioni moja sijui na laki ngapi, barua ziko hapa na ameendika several times. Sasa wako walimu wa namna hii wangapi? Kwa hiyo, nitampa Waziri husika atuambie ni kwa sababu gani wanawadhalilisha walimu kiasi hiki. Walimu ndiyo kila kitu kwa hiyo niombe sana Serikali iache kuwadhalilisha walimu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo nataka kuzungumzia ni suala zima la Bodi ya Mikopo ya Juu. Tumelizungumza jana kwenye hotuba na hata Kamati, Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu inapata fedha nyingi sana which is very good lakini fedha hizi takribani zaidi ya asilimia 52 kwa mwaka huu zinaenda kwenye Bodi ya Mikopo, ile miradi halisi ya maendeleo kuanzia shule za msingi mpaka elimu ya juu, ndiyo sababu unaona majengo mengi ya vyuo vya elimu ya juu pamoja na vyuo vya ualimu haitekelezwi kwa sababu fedha zinaenda kwenye Bodi ya Mikopo. Kwa hiyo, ni ombi langu kwamba vote ya Bodi ya Mikopo iwe peke yake ili irahisishe kwanza ufuatiliaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wala haiingii akilini kwa sababu gani Tume ya UNESCO ambayo iko chini ya Wizara hii ina vote yake na inapokea shilingi bilioni 2 tu lakini Bodi ya Mikopo inapokea takribani shilingi bilioni 500 kwa nini isiwe na vote yake. Kikubwa zaidi tunachozungumza hii Bodi ni lazima iwekewe vote yake peke yake ili irahisishe ufuatiliaji wa fedha zinazorejeshwa na ambazo zinatoka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, natambua kwamba kuna miradi ya maendeleo mingi sana yaani kwa hiyo shilingi bilioni 863, shilingi bilioni takribani 400 ndiyo zinabaki. Jambo la kusikitisha miradi muhimu kama ya vyoo na usafi fedha za nje tu ndiyo zinahudumia. Kwa hiyo, leo tunahitaji wahisani watuchimbie vyoo, haiwezekani. Kwa hiyo, hili ni jambo muhimu sana lizingatiwe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni TET. Wengi wameongelea kuhusu vitabu, mtakuwa mnawafukuza tu Wakurugenzi lakini sawasawa, haiwezekani TET wawe ndiyo wachapishaji, editors, evaluators na wana approve, haiwezekani na haiko mahali popote. Kwa hiyo, ombi langu ni kwamba lazima kuwe na independent organ ambayo itakuwa inapitia vitabu hivyo. Pia editor atakayejulikana amehariri vibaya huyo ndiye achukuliwe hatua. Kwa mfano, haiwezekani SUMATRA yenyewe iwe inamiliki mabasi, kwa hiyo na huku haiwezekani hao TET watunge vitabu, wasambaze na ndiyo sababu tunapata matatizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho naomba sana Wizara sasa hivi wanataka kupeleka vitabu mpaka China wakati humu ndani hamjapeleka vitabu kwenye shule za private, mnaendaje China?

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)