Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Hon. Amb Dr. Diodorus Buberwa Kamala

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nkenge

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

MHE. BALOZI DKT. DIODORUS B. KAMALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa fursa hii ninayo mambo machache ambayo ningependa kuchangia naomba nianze kwa kusema naunga mkono hoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza ambalo ningependa kulichangia, sote tunafahamu kwamba hivi sasa tunajenga Tanzania ya viwanda lakini ili tuweze kujenga Tanzania ya viwanda kada muhimu sana inayoweza kutusaidia kujenga Tanzania ya viwanda ni vyuo vya ufundi (Technical Colleges) hivi sasa tunazo Technical Colleges nadhani tatu, tuna Arusha Technical College, tuna kule Mbeya halafu tuna Dar Technical.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nashauri Mheshimiwa Waziri, aje na mpango wa makusudi na wa dharura ili tuanzishe vyuo vyote kama hivyo kwa ajili ya Kanda ya Kusini, Kanda ya Ziwa na Kanda ya Magharibi rafiki yangu hapa nyuma anasema Kanda ya Kati nilikuwa sijalipanga, naomba niongeze pia na Kanda ya Kati. (Makofi)

Mheshimiwa Waziri tukifanya hivyo tutaweza kujenga Tanzania ya viwanda kwa spidi kubwa zaidi. Uwezekano wa kufanya hivyo upo, na uwezekano wa kupata fedha za kutekeleza jambo hilo upo na Waheshimiwa Wabunge tupo hapo tutakushauri zaidi hizo fedha utazipata namna gani. Jambo muhimu ni kuja na mpango na huo mpango upate baraka za Bunge zima na tutafanya hivyo, tutaweza kujenga Tanzania ya viwanda kwa kasi zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, nimeangalia bajeti ya Mheshimiwa Waziri, kitu kimoja kilichokuja kwenye kichwa changu ni kwamba shule hizi za msingi na shule za sekondari ni shule ambazo zipo lakini hazina mwenyewe. Kwa sababu unakuta Wizara ya Elimu ndiyo inapanga sera na viwango na kila kitu, lakini inapokuja kwenye kugawa walimu, ukimwambia Mheshimiwa Waziri hapa, shule yangu fulani haina walimu, atakwambia hilo jambo linashughulikiwa na Wizara nyingine. Ukimwambia kuna tatizo la madarasa sehemu fulani, ataniambia jambo hilo linashughulikiwa na Wizara nyingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nami naona hizi shule za msingi na sekondari zipo lakini hazina mwenyewe; na mwenyewe ni Wizara ya Elimu. Kwa hiyo, nashauri kwamba wakati umefika Serikali ifikirie kurejesha utaratibu wa zamani, mambo ya elimu yote yasimamiwe na Wizara ya Elimu ili ziwe na mwenyewe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivyo kwa sababu kuna shule moja inaitwa Shule ya Msingi Kajunguti, iko kilomita 10 kutoka Makao Makuu ya Wilaya ya Misenye. Shule hii ina walimu wawili tu, walimu wote wawili hawakai pale. Hii shule haina mwenyewe, maana wakati fulani ilitolewa na KKKT, lakini ukiwauliza KKKT shule hii mlitoaje? Mlitoa nyaraka zinazosema mmeitoa? Wanasema hawakutoa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ni shule ambayo haina mwenyewe. Sasa nikagundua kwamba siyo hiyo tu, ni shule zote za Tanzania zipo, lakini hazina mwenyewe na mwenyewe ni wewe, ndiyo maana nashauri leo hii utaratibu wa zamani urejeshwe ili kuweza kuweka sawa utaratibu wa elimu hapa Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna jambo moja ambalo nimekuwa nikisikia muda mrefu kwamba Waheshimiwa hawa walimu wanaofundisha kwenye shule za msingi, siku moja nilikuta Afisa Elimu mmoja wa Wilaya, aliita Walimu wa Shule za Msingi ofisini kwake, akawa anawakemea, anawatukana kama watoto wadogo. Nikaangalia nikasema aah, huyu Afisa Elimu, hawa walimu nao si wamesoma kama yeye! Unakuta kwamba akishakuwa Afisa Elimu anaona walimu kama watoto wadogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili nilipojaribu kufuatilia zaidi nikakuta na lenyewe halina mwenyewe, kwa sababu mwisho wa siku kumbe wanaosimamia maadili ni watu wengine. Sasa hizi ni vurugu. Ndiyo maana nasema turejeshe ule utaratibu wa zamani na walimu tuwanyime kila kitu ambacho hatuwezi kuwapa, lakini tuwape heshima wanayostahili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna jambo lingine niliseme, tuna uhaba wa walimu tunakubali, lakini uhaba huo wa walimu sawa, lakini wale wachache waliopo tuwagawe sawa. Haina sababu unasema kuna uhaba wa walimu lakini unakuta shule nyingi zina walimu 20, shule nyingie 10, shule nyingine ina wawili, shule nyingine ina mmoja tu, hii sio sawa sawa. Hao wachache waliopo tuwagawe sawa. Sasa hilo nitaliletea hoja maalum kuonyesha ni jinsi gani wale wachache waliopo tuwagawe sawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja ya mwisho ningependa kuisisitiza, namshukuru Mheshimiwa Waziri kwa kazi nzuri aliyoifanya kule Jimboni kwangu kwa kukarabati Chuo cha Maendeleo ya Wananchi. Natambua mwanzoni fedha hazikutumika vizuri, baadaye alikuwa mkali akaelekeza kwa karibu, akafuatilia, sasa naona kazi imefanyika vizuri. Nakushukuru Mheshimiwa Waziri kwa kunisaidia na chuo hicho sasa kimekarabatiwa vizuri na mambo yanaendelea vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa nirudie kusisitiza, turejee kwenye utaratibu wetu wa zamani wa kusimamia elimu. Tukiendelea kama tunavyoendelea sasa, hizi shule zote, sekondari na kila kitu zitakuwepo lakini zitakuwa hazina mwenyewe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukisoma hii hotuba ya Mheshimiwa Waziri, utakuta sehemu kubwa amejikita zaidi kwenye Vyuo vya Elimu ya Juu na Vyuo vikubwa vikubwa lakini kitu ambacho ni cha msingi kabisa walimu, wanafunzi unatakiwa uwaandae tokea kule chini waliko. Sasa Mheshimiwa Waziri anasubiri waje mpaka huku juu, anawapokea kwenye vyuo vikuu na kuendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani kuna haja ya kulitafakari hili jambo na kuja na mpango mbadala wa kurejea kwenye utaratibu wetu wa zamani. Bila kufanya hivyo, tutaendelea kuwa tunafikiri tunaendelea mbele lakini kumbe tuko pale pale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. (Makofi)