Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Hon. Eng. Edwin Amandus Ngonyani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Namtumbo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

MHE. ENG. EDWIN A. NGONYANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa fursa hii ya kuongea leo, pili nikushukuru wewe kwa kunipa hii fursa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara hii, inayoongozwa na Mheshimiwa Prof. Joyce Ndalichako, kwa kweli sina maneno ya kusema, na wana Namtumbo wote hawana maneno ya kusema, ni furaha tu kwao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kwa mara ya kwanza, Tanzania inajenga vituo vya VETA katika ngazi ya wilaya na wameanzia Namtumbo, nawashukuruni sana. Nashukuru sana Mheshimiwa Rais amekuja na kukipa heshima kubwa zaidi kile kituo cha VETA cha Namtumbo kwa kukifungua, nashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikuombe sana Mheshimiwa Waziri, hakikisha kwamba yale yaliyobaki madogo madogo tuyamalize, ili mafunzo yaanze kutolewa katika kile chuo. Kile chuo kimejengwa pembeni kidogo na maeneo wanayokaa watu, kwa hiyo, wanafunzi wanahitaji mabweni, lakini vilevile walimu wanahitaji nyumba. Niombe sana tusaidiane hayo nayo yakamilike ili wana Namtumbo na watanzania wote kwa ujumla waweze kuanza kukitumia kile chuo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo hilo tu, katika sera ya kila kata kuwa na Sekondari, lengo la Serikali ilikuwa kwamba kila Sekondari, iwe ni ya day, iwe ni ya kutwa, na kisera tuko sahihi kabisa. Lakini tunapokuja kwenye utekelezaji, kuna baadhi ya kata zinaunganisha vijiji ambavyo viko mbalimbali sana. Nikitolea mfano, Kata yangu ya Magazine, kijiji hadi kijiji ni kilomita zisizopungua 20 na viko vijiji vitatu. Siyo hiyo tu, kuna Kitongoji ambacho kipo kilomita 26 kutoka kwenye makao makuu ya kijiji, cha mwisho kabisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa katika mazingira haya, hatutarajii sekondari hiyo isikose mabweni. Tunakubaliana kwamba sekondari zote za kata ni za kutwa, sisi hatuna tatizo na hilo, tatizo tulilonalo ni kwa idara hii ya udhibiti elimu kutuzuia kujenga mabweni, ni sisi wenyewe tunaamua kujenga mabweni, na tunayahudumia wenyewe kwa sababu tunataka watoto wetu wale waliokusudiwa kuitumia hiyo shule ya sekondari, waweze kupata masomo, isitokee ni kile kijiji kimoja tu ambacho sekondari imejengwa na vijiji vingine vikakosa hiyo fursa kwa sababu ya umbali, umbali ni mkubwa sana na haiwezekani wakasoma kwa kutwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niombe, ni kata nyingi ambazo katika wilaya yangu zina mazingira hayo na kata zote zenye mazingira hayo zimeamua kujenga mabweni, wenyewe, na wenyewe wanahudumia! (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuna walaka umetolewa, na hii idara ya kudhibiti elimu inayokataza mabweni hayo yasifanye kazi na yasiendelee kujengwa. Niombe sana hilo liangaliwe. Shule hizo ziendelee kuchukuliwa kama shule za kutwa, lakini sisi wenyewe tulioamua kuhudumia wanafunzi wetu wanaosoma katika shule hizo kwa kujenga mabweni na kujenga eneo la kulia chakula na shuguli zote zile tunahudumia wenyewe, turuhusiwe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani siyo sahihi kutuzuia kwa sababu ukituzuia, maana yake unatuzuia fursa ya kutumia hizo shule za kutwa kupata elimu kwa watoto wetu. Niombe sana hilo liangaliwe kwa makini sana. Lakini ni utekelezaji mzuri sana wa hiyo sera kwa sasa kwa kweli ni kwa mara ya kwanza sisi Namtumbo napo tunapata wanafunzi wengi wanaomaliza kidato cha nne na wengine sasa wanaingia kidato cha tano kwa sababu kiwango kile cha ufaulu kimeanza kuongezeka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini niombe, kama ambavyo wengine wamesema, naomba hasa walimu wa sayansi, tunaomba sana muendelee kutusaidia. Najua mnaendelea kuajiri, lakini kasi ya kuajiri ni ndogo sana, hata kama tatizo ni ukubwa wa bajeti ya mishahara ya Serikali kwa ujumla, naomba sana Serikali itoe kipaumbele kwa masuala ya elimu pamoja na afya kwa maana ya zahanati na vituo vya afya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hizi sekondari pamoja na shule za msingi, tutoe kipaumbele, tusijali sana ukubwa wa bajeti ya mishahara katika kuzuia kuajiri. Nikuombe sana Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Utumishi na Utawala Bora) utusaidie kwenye hilo. Tunaomba walimu ili tuweze kupata ile elimu iliyokusudiwa kupitia hizi shule za sekondari za kata lakini vilevile shule za msingi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu vyuo vya walimu, hapa nilitaka tu kusema, kule kwetu Namtumbo, kilianzishwa chuo cha Walimu, kipo katika Kijiji cha Nahoro, kinamilikiwa na Chama Kikuu cha Ushirika cha Songea na Namtubo, (SONAM). Chuo hiki kilianzishwa ili kujaribu kutatua changamoto za watoto wetu wengi wanaomaliza kidato cha nne lakini hawapati fursa ya kwenda kwenye vyuo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na kilipoanza, kimedahili mara mbili kwa kutumia kile kibali cha muda, (provisional registration). Sasa baada ya miaka miwili, mmetuzuia tusiendelee kudahili, ni sawa, ni suala la udhibiti, lakini kinachoshangaza ni kwamba, katika miaka ile miwili ya udahili, kile chuo kilikuwa ni kati ya vyuo bora Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika ile miaka miwili, mitihani waliyofanya miaka ile miwili, hicho chuo kilikuwa bora kabisa na kikaanza kuvuta wanafunzi wengi kutoka maeneo, nje ya Namtumbo, nje ya Mkoa wa Ruvuma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hatuelewi, kimezuiwa kweli ni kwa sababu hakijakidhi viwango kwa maana hawana jengo la kompyuta na mengine, au pengine ni kuzuia tu watu wasiende Namtumbo au na watu wa Namtumbo wasipate fursa ya kudahiliwa katika chuo hicho! Maana yake inawezekana tatizo tunaofanya kazi kwenye idara mbalimbali, unaweza ukafanya kitu sahihi kabisa, lakini motive yako ikawa tofauti. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwangu kwa mfano, nilifikiria, badala ya kukizuia, mngeweza kukisaidia kimalize zile changamoto kilizonazo ili wanafunzi waendelee kudahiliwa. Kwa sababu, tatizo halikuwepo katika ubora wa elimu inayotolewa, ubora wa elimu unaotolewa katika kile chuo ni the best na ndiyo maana katika ile miaka miwili kilikuwa kati vya vyuo bora Tanzania, kwa hiyo, hakukuwa na tatizo la ubora. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kukizuia, inawezekana kweli ni kwa sababu ya hizo sababu ambazo Idara ya Udhibiti wa Ubora wa Elimu imezitoa kwa kuzuia lakini sisi kule tunaona kama ni kutunyima fursa ya kukitumia kile chuo. Nikuombe sana Mheshimiwa Waziri, changamoto hizo, kama ni kweli ndiyo, is it core or subsidiary. Mimi nadhani, kama siyo core reasons, kile chuo kiendelee kudahili, kwa sababu kinatoa mafunzo mazuri na kwa kweli, kinatoa walimu the best kati ya the best vyuo katika Tanzania. Nikuombe sana uliangalie hilo kwa makini na utusaidie.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli, nichukue fursa hii kuipongeza tena Wizara kwa kukiorodhesha Chuo cha Maendeleo ya Jamii cha Mputa, kati ya vyuo vitakavyofanyiwa ukarabati katika Awamu ya II, nikupongeze sana Mheshimiwa Waziri, Umeendelea kutembea katika kivuli cha Mheshimiwa Rais, cha kuiona Namtumbo ambayo iko nyuma sana, ni kati ya wilaya ambazo ziko nyuma sana katika wilaya zile ambazo ziko Tanzania nyuma sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, na wewe unaanza kutembea katika kivuli cha Mheshimiwa Rais, cha kutuona sisi wana Namtumbo na kutusaidia. Nimefurahi sana na wana Namtumbo watafurahi sana kusikia chuo chao cha Mputa cha Maendeleo ya Jamii kinakwenda kukarabaitiwa… (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimwa.

MHE. ENG. EDWIN A. NGONYANI: Kimekuwa kikiishi kama chuo yatima…

MBUNGE FULANI: Muda umeisha, unga mkono hoja.

MHE. EDWIN A. NGONYANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja asilimia 100 na kwa kweli nashukuru sana, kama nilivyosema hatuna maneno juu ya Wizara hii. (Makofi)