Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017- Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji

Hon. Omary Tebweta Mgumba

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017- Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji

MHE. OMARY T. MGUMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi hii ya kuchangia katika Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji.
Pili, namshukuru Mwenyezi Mungu aliyenijalia kufika siku ya leo, kunipa afya na uzima.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tatu, naomba niwape pole Wapiga Kura wangu wa Jimbo la Morogoro Kusini Mashariki na Morogoro Vijijini kwa ujumla kwa mafuriko makubwa yaliyowakuta ya mvua ambapo mashamba yao yote yameharibika na mvua hiyo!
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nichukue nafasi hii kumshukuru sana Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Mheshimiwa Dkt. Kebwe na Mkuu wa Wilaya kwa hatua yao waliyoichukuwa ya kutusaidia chakula ingawa kidogo lakini siyo haba, kimesaidia sana waathirika hawa! Nachukua fursa hii kuiomba Serikali, tunaomba misaada zaidi ya chakula katika maeneo yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia nampongeza sana Waziri wa Viwanda na Biashara kwa hotuba yake nzuri ambayo inaonyesha dhamana aliyobeba ya kutimiza matakwa na ndoto za Rais wa Awamu ya Tano, Mheshimiwa John Pombe Magufuli. Kwa sababu Rais wa Awamu ya Tano tangu anaomba kura mpaka sasa anajipambanua kwamba Serikali yake itakuwa ni ya viwanda. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimtie moyo Mheshimiwa Waziri wa Viwanda na Biashara angalau ameanza kuleta mpango. Pamoja na wengine wanasema kwamba umekuja na mpango lakini fedha ambazo umeziomba ni chache sana, kuna tatizo moja ambalo kama wazungu wanavyosema, ukitaka kumnyima kitu Mwafrika, kiweke kwenye maandishi. Kwa sababu umeongelea vizuri kwenye ukurasa wa 140 kwenye mikakati yako.
Mheshimiwa Mwenyekiti, cha kwanza kabisa naomba ninukuu na umesema; “kuhamasisha sekta binafisi, kuanzisha na kuendeleza viwanda vinavyotumia malighafi za hapa nchini na kuvutia wawekezaji kujenga viwanda vya vifungishio (packaging) na kadhalika.”
Mheshimiwa Mwenyekiti, hiyo ni nini maana yake? Maana yake ni kwamba siyo Serikali ndiyo itajenga viwanda, bali ni sekta binafisi ndiyo itajenga viwanda. Kazi ya Serikali itakuwa ni kuweka mazingira mazuri ya kuivutia sekta binafisi kuja kuwekeza katika viwanda na hatimaye kutoa ajira. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa wenzetu wanaosema kwamba bajeti ni ndogo, nafikiri kwamba hiki kitabu kama ulivyosema au tulivyokiona ni kikubwa sana, watu wanaona uvivu kukisoma chote. (Makofi)
La pili, Mheshimiwa Waziri unalaumiwa na unaambiwa kwamba mpaka leo miezi sita haujaanzisha kiwanda chochote. Hawa wenzetu ndiyo maana tunasema wenzetu vigeugeu! Juzi tu hapa wamekuja walikuwa wanailaumu Serikali hii kuhusu kuhamisha fedha kutoka sehemu moja kwenda sehemu nyingine kuwahudumia Watanzania. Leo hii ndani ya miezi sita, hili ndilo Bunge la Bajeti ya kwanza la Serikali ya Awamu ya Tano; kwa fedha gani ungeweza kuitumia kujenga viwanda hivyo ndani ya miezi sita? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nafikiri ndiyo maana ameleta hapa sasa tumpe ili mwakani akija ndiyo tumkabe koo. Kwa hiyo, niwaombe tu ndugu zangu kwamba pamoja na kwamba tunatamani sana hivyo viwanda vijengwe, lakini haviwezi kujengwa bila kupitisha bajeti na mipango aliyoileta katika Bunge hili na hiyo ndiyo kazi yetu sisi Wabunge, tumpitishie halafu tuje tumhukumu mwakani akija. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya utangulizi huo, naomba nichangie katika mpango wenyewe aliouleta. Mheshimiwa Waziri kama ulivyosema, miongoni mwa changamoto zinazowakabili wawekezaji wengi ni malighafi isiyokuwa ya uhakika, maana yake nazungumzia viwanda ambavyo vipo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nitangaze interest, maana unaweza kusema mimi nazungumzia korosho. Mimi niliwahi kufanya kazi katika kampuni inayohusika na mazao ya biashara miaka 19 kwa ajili ya exportation.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ninachoongelea nina uzoefu kidogo wa kujua ni changamoto gani ambazo wanakumbana nazo hususan kwenye korosho, pamba, kahawa, mbaazi, dengu, choroko, mpunga na kadhalika. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nizungumzie changamoto zinazowakabili wawekezaji wa viwanda vya korosho, kwa sababu viwanda hivi vinabeba uchumi mkubwa sana hasa kwa wakulima wa Mikoa ya Lindi, Mtwara, Pwani na sehemu ndogo ya Mkoa wa Morogoro katika upande wa Mkulazi kule tulikopakana na Kisarawe. Ndiyo maana nafarijika na hili kulizungumzia mara nyingi kwenye upande wa viwanda.
Mheshimiwa Mwenyekiti, viwanda hivi kama nilivyowahi kusema mwanzoni, sababu mojawapo ambayo wawekezaji wengi wamefunga viwanda vya kubangua korosho, miongoni mwa sababu mojawapo ni mfumo wa stakabadhi ghalani ambao hauwapi fursa wawekezaji wa ndani kupata raw materials.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ule mfumo unaoenda kuwashindanisha wawekezaji wa ndani wenye viwanda pamoja na wabanguaji wa India kwenye uwanja mmoja. Haiwezekani hata siku moja mwenye kiwanda cha ndani atafute raw materials mpeleke kwenye mnada akashindane na wabanguaji wa India, hawezi kupata raw material. Ndiyo maana uliona sababu, kulianzishwa viwanda zaidi ya 10, tulishafikia kubangua zaidi ya tani 50,000, nchini leo vyote vimefungwa vimebaki viwili tena vinasuasua!
Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo jambo jepesi, mtu kawekeza mtaji wake, ka-run kiwanda zaidi ya miaka mitano, leo anafunga na Serikali tumekaa kimya, wanahamishia nchi za wenzetu za jirani, kuna tatizo! Naomba kushauri katika hili, kama kweli tunataka kuwavutia wawekezaji wengi waje kwenye kuwekeza Tanzania husasan katika viwanda vinavyotumia malighafi za Tanzania, kwa mfano kama korosho, ni lazima tuwatengenezee mazingira mazuri ya kuhakikisha wanapata malighafi hiyo, la sivyo itakuwa ni ndoto. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakupa mfano tu, kwa mfano, huwezi kushindana na India kwa sababu India wenyewe ukizungumza korosho, unazungumza siasa za India. Wale wana uwezo wa kubangua tani 1,600,000, lakini uzalishaji wao ni tani 600,000 tu. Kwa hiyo, ni lazima wanahitaji tani milioni moja kutoka nchi mbalimbali. Ndiyo maana wanawapa mpaka incentive ya 2% kwa ajili ya mtu ku-export korosho iliyobaguliwa kutoka India, Tanzania kwetu hakuna! Pia mtu akibangua kule, by product kwa maana ya vipande vya korosho, kwa maana ya maganda ya korosho, yote ni biashara lakini Tanzania hakuna. Kwa hiyo, kuna incentive kubwa zaidi India kuliko Tanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu katika hili, tuweke kabisa Sera ambayo inatambulika na itawavutia wawekezaji kwamba mtu yoyote anayewekeza kwenye Korosho hapa Tanzania, tutahakikisha anapata raw material kwanza kwa ajili ya kutosheleza kiwanda chake kwa mwaka mzima, ndiyo turuhusu mnada mwingine kwa ajili ya kupeleka nje ya nchi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hapo watakuja, kwa sababu hata sera yetu nchini hairuhusu ku-import raw material kutoka nje, wakati nchi nyingine kama Vietnam na India wanaruhusu ku-import raw material kutoka nchi nyingine. Sababu ni nini? Kumpunguzia gharama za uzalishaji huyu mwekezaji. Kwa sababu usipomruhusu a-import raw material kutoka nchi nyingine, ukizingatia korosho ni biashara ya msimu ya miezi mitatu, maana yake unamlazimisha mwekezaji wa Tanzania, kama ana kiwanda cha kubangua tani 50,000 anunue hiyo raw material ya 50,000 kwa miezi mitatu na ai-store.
Mheshimiwa Mwenyekiti, maana nyingine gharama itakuwa kubwa kwenye storage, kwenye mtaji, kwenye weight loss, kwenye running na kwenye mishahara kwa ajili ya walinzi na wafanyakazi wengine kulinda hiyo, kitu ambacho kwingine hamna. Wanaruhusu ndani ya miezi mitatu kwa sababu biashara ya korosho ni rotation business in the world.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hii biashara, watu wanazunguka, wanunuzi ni hao hao. Miezi mitatu wako Tanzania, baada ya Machi wanakwenda India mpaka Juni; baada ya Juni wanakwenda Afrika Magharibi kwa maana ya Nigeria, Guinea Bissau na Ivory Coast. Kwa hiyo, mtu ana fursa, atakuja kununua hiyo mwezi Oktoba kwa ajili tu ya kutumia hiyo miezi mitatu, baada ya hapo anakwenda sehemu nyingine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu muda siyo rafiki sana, nitakuona Mheshimiwa Waziri nikupe mchango zaidi katika hili ili ukusaidie katika kuwekeza katika kilimo hususan mazao ya kilimo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili nisije kusahau nyumbani, sisi ni wakulima wa matunda na ninakushukuru sana Mheshimiwa Waziri Mwijage kwa juhudi zako kubwa unazozifanya kwa ajili ya kutukumbuka watu wa Morogoro hususan kwenye kilimo cha ndizi na kututafutia wawekezaji kwa ajili ya kiwanda cha ndizi ili tuweze kupata soko la uhakika kwa ajili ya matunda yetu, mananasi, ndizi na menginyo yanayopatikana ndani ya Morogoro Vijijini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hapo naomba nitoe ushauri mwingine. Kwa sababu hii korosho tukibangua hapa tutapata ile korosho iliyobanguliwa ambayo kitalaam inaitwa kernel, lakini baada ya kernel kuna vile vipande vipande. Hivi vipande vipande, soko hakuna kwingine zaidi ya India. Ila kudhibiti kutaka watu wakabangue kule, India wameweka import duty kubwa.
Nakuomba Mheshimiwa Waziri uende kwenye Ubalozi wa India ukawaombe angalau ili kuvutia wawekezaji waje wawekeze hapa, waondoe ushuru huu wa vipande ili tupate soko la hao wanaobangua hapa, vile vipande tukauze India.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, nakuomba kwa sababu wewe ndio Waziri wa Uwekezaji na Biashara, katika suala la mchakato wa kupata leseni za biashara, ni vizuri ukafungua dawati moja ambalo litarahisisha hao wawekezaji kwa maana ya sehemu zote kupatikana katika…
MHE. OMARY T. MGUMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naomba kuunga mkono hoja.