Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Spika, kwa hekima na busara kubwa, napenda kuchukua fursa hii kwanza kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa uhai na kuniwezesha kushika kalamu na kutoa mchango wangu kwenye Wizara hii muhimu kwa ustawi wa maisha ya jamii yetu.

Mheshimiwa Spika, nianze mchango wangu kwa kuwapongeza Mawaziri wote wanaohudumu kwenye Wizara hii sambamba na watumishi wote walioko kwenye Wizara hii. Pongezi za kipekee kwa askari wetu wa usalama barabarani kwa kazi nzuri wanayoifanya. Japo wapo askari wanaolitia doa Jeshi la Polisi kwa kupenda kwao vipesa vidogo vidogo, ushauri wangu kwa hao wachache wanaochafua jeshi letu ni basi wakadhibitiwa ipasavyo na pale wanapobainika basi adhabu kali iwe juu yao.

Mheshimiwa Spika, nijielekeze kwenye makazi ya Askari Polisi na Magereza. Makazi ya askari wetu bado ni mabaya sana hasa kwa askari wa mikoani na kwenye magereza za pembezoni. Mfano, Wilaya ya Liwale ni wilaya ya tangu mwaka 1975 lakini hadi leo haina jengo la kituo cha polisi wala nyumba za askari licha ya halmashauri kutenga eneo zaidi ya heka 60. Jengo wanalolitumia ni jengo la nyumba ya mtu binafsi. Kitendo cha polisi kukaa uraiani kunawapunguzia weledi wa kazi yao. Pamoja na hivyo lipo pia Gereza la Kipule ambalo lilianzishwa tangu mwaka 1982 lakini hadi leo eneo linalomilikiwa na gereza hili halijalipiwa fidia toka kwa wananchi. Gereza hilo pia hadi leo lina majengo ya udongo na uzio wa miti na kufanya wale wafungwa sugu au wa muda mrefu kulazimika kupelekwa Lindi.

Mheshimiwa Spika, vitendea kazi vya askari polisi; Wilaya ya Liwale imezungukwa na misitu, ni wilaya yenye mtawanyiko mkubwa lakini kuna uhaba mkubwa wa gari la askari polisi. Pamoja na mwaka huu kuletewa gari la Canter nalo ni kubwa linashindwa kuingia kwenye barabara za vijiji au vichochoroni. Hata hivyo napashwa kwa niaba yao nishukuru kwa hilo gari kwani ni hatua moja ya kutatua matatizo la usafiri kwa Polisi wa Wilaya ya Liwale. Ni matumaini yangu Serikali inaona umuhimu wa kuwa na gari la polisi sambamba na nyumba za askari.

Mheshimiwa Spika, katika Idara ya Uhamiaji bado kazi zao wanafanya kizamani sana, bado hawaendi na kasi ya Mheshimiwa Rais. Bado habari ya njoo kesho, njoo kesho ni nyingi hasa kwa raia wanaoomba uraia wa nchi yetu kwa wale wageni wa muda mrefu. Ni bora mwombaji apewe majibu mapema kama anaweza kupata au amekosa sifa za kupata uraia basi ni bora akafahamishwa. Kuacha kumpatia majibu kwa muda mrefu kunajenga mazingira ya rushwa. Ni bora Uhamiaji wakawa wazi kama mtu anakosa sifa za kupata hati ya uraia.

Mheshimiwa Spika, kikosi cha Zimamoto, ni kikosi muhimu sana kwa ulinzi wa mali zetu na ulinzi wa maisha yetu ya kila siku, lakini jeshi hili halijapewa umuhimu unaostahili. Jeshi la Zimamoto hawana magari ya kutosha na vifaa vya kukabiliana na majanga ya moto.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo ziko wilaya ambazo hazina kabisa Jeshi hili la Zimamoto. Mfano Wilaya ya Liwale hakuna Askari hata mmoja wa Zimamoto na hivyo hata raia wa Liwale hawana uelewa wa kutosha juu ya kukabiliana na majanga ya moto, lakini wafanyabiashara bado wanalipa kodi ikiwemo ya zimamoto. Je, wanalipia huduma gani wakati hakuna ofisi ya zimamoto. Je, Mheshimiwa Waziri haoni kuwa watu hawa wanalipia huduma ambayo hawatarajii kuipata?

Mheshimiwa Spika, mimi mpaka leo sioni faida ya watu kukaa magerezani kama wafungwa. Kwa nini wafungwa wawe mzigo kwa Taifa kwa kuwalisha bila wao kujitegemea. Nilitarajia kuona magereza yetu yakijitegemea, huko nyuma, magereza mengi yalikuwa na mashamba makubwa ya mazao ya chakula. Pia kulikuwa na viwanda vya kusindika mazao ya wakulima na kadhalika. Vilevile kulikuwa na viwanda vya mazao ya mifugo na uvuvi na mazao ya misitu. Kwa ushauri wangu kama magereza haziwezi kujitegemea hakuna haja ya kupeleka wafungwa magerezani na hivyo Serikali itafute njia nyingine ya kuwarekebisha wahalifu au wafungwa.