Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

Hon. Shabani Omari Shekilindi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lushoto

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

MHE. SHAABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze Waziri mwenye dhamana ya Wizara hii pamoja na timu yake yote kwa kazi nzuri anayoifanya.

Mheshimiwa Spika, Serikali iliyotoa shilingi milioni 500 kwa ajili ya kujenga Kituo cha Polisi Lushoto lakini mpaka sasa kituo kile hakijakamilika. Nilipofuatilia nikaambiwa fedha zimeisha na wakati jengo lipo kwenye usawa wa lenta. Kwa hiyo, niiombe Serikali yangu ifuatilie fedha hizo ili jengo lile liweze kuisha na kama unavyofahamu Kituo cha Polisi Lushoto ni cha tangu Mkoloni, kwa hiyo ipo haja kubwa kumalizia kituo kile.

Mheshimiwa Spika, pamoja na hayo, kuna tatizo kubwa sana la nyumba za Askari Polisi na Askari Magereza. Kama nilivyotangulia kusema kuwa Kituo cha Polisi pamoja na Magereza majengo haya ni ya tangu Mkoloni na hii imefanya Askari wetu kuishi katika mazingira magumu mno. Kwa hiyo, niiombe Serikali yangu Tukufu ipange bajeti mwaka huu ili tupate hata nyumba kidogo za wafanyakazi wa Polisi pamoja na Magereza.

Mheshimiwa Spika, sambasamba na hayo, Gereza la Wilaya Lushoto lipo katikati ya mji ambapo siyo salama kwa Askari wetu wa Magereza, kwani wanakuwa na kazi ya ziada na hii inapelekea kutoroka kwa wafungwa. Kwa hiyo, niiombe Serikali yangu itenge fedha ili kujenga gereza lile eneo ambalo tayari limeshatengwa la Yogoi.

Mheshimiwa Spika, kumekuwa na baadhi ya Askari wanafanya vitendo vya kihalifu lakini yote haya ni kutokana na kukaa kwa muda mrefu katika kituo kimoja, ndiyo maana Askari hawa wanatumika na wenyeji hasa wenye uwezo wa kifedha kufanyia matukio watu ambao hawana hatia, hasa kuwabambikia kesi, ili mradi tu hakupewa rushwa na mhusika. Kwa hiyo, niishauri kama siyo kuiomba Serikali kuwahamisha Askari hawa, hasa katika Wilaya ya Lushoto kuna Askari wanataka kuzeeka hapo hapo Lushoto.

Mheshimiwa Spika, kumekuwa na malalamiko mengi kutoka kwa wananchi wetu kucheleweshewa Vitambulisho vya Taifa, hasa wale waliopo vijijini kwani tumekuwa tukikosa majibu ya kuwajibu wananchi wetu. Kwa hiyo, niiombe Serikali yangu ifanye haraka iwezekanavyo, iwapatie wananchi vitambulisho hivyo na kama unavyojua vitambulisho hivyo ni muhimu katika usajili wa mambo mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, Wilaya ya Lushoto ni ya milima na mabonde, kwa hiyo, kwa jiografia hiyo wananchi wengi hasa wa pembezoni hawapati huduma hasa ile ya usalama pamoja na mali zao. Hii imepelekea wananchi kuvamiwa mara kwa mara na kupoteza maisha pamoja na mali zao au kujeruhiwa mwisho wa siku anakuwa ni mlemavu wa viungo. Kwa hiyo, niiombe Serikali yangu Tukufu ijenge vituo vidogo vya Polisi katika kila Kata ili kupunguza changamoto hizi zinazoendelea kujitokeza.

Mheshimiwa Spika, Askari wa Barabarani wamekuwa wakiwanyanyasa madereva wa magari hasa wa Noah, bodaboda pamoja na wa magari ya mizigo. Hali hii imekithiri katika Wilaya ya Lushoto. Nimuombe Waziri atume hata wataalamu wake ili wakajionee jinsi madereva wale wanavyonyanyasika, hasa hawa wa bodaboda, ukizingatia bodaboda hawa, pikipiki nyingi wamezaminiwa utakuta mwisho wa siku anarudi mtaani na kufanya vitendo vya kihalifu. Niendelee kuiomba Serikali yangu kuwasimamia vijana hawa wa bodaboda waweze kufanya kazi zao bila ya bughudha.

Mheshimiwa Spika, pamoja na hayo, Mheshimiwa Waziri alitoa tamko la zile pikipiki zilizokamatwa kwa makosa madogo madogo ziachiliwe lakini ukifika Kituo cha Polisi Lushoto, pikipiki hizo zimejaa. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri na hili ulifanyie kazi.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.