Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

Hon. Jitu Vrajlal Soni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Babati Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

MHE. JITU V. SONI: Mheshimiwa Spika, naomba nichukue fursa hii kwanza kumshukuru Mwenyenzi Mungu kunipa fursa kuchangia siku ya leo. Nimpongeze Mheshimiwa Rais wetu kwa kazi nzuri anayoifanya katika kuendeleza Taifa letu.

Mheshimiwa Spika, nichukue fusa hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu, Katibu Mkuu na timu nzima ya Wizara pamoja na viongozi wetu wakuu wa majeshi chini ya Wizara hii kwa kazi kubwa na nzuri wanayoifanya. Pamoja na changamoto kubwa ya uhaba wa vifaa na nyenzo za kufanyia kazi, hongereni kwa kazi kubwa na nzuri.

Mheshimiwa Spika, naomba nishauri katika baadhi ya maeneo ili kuboresha huduma katika majeshi yetu. Nianze na Jeshi la Magereza, wanafanya kazi kubwa na nzuri. Wana majukumu makubwa sana ya kuwahifadhi wahalifu walioshtakiwa kwa makosa mbalimbali na zaidi ya hapo kutoa elimu ya kuwarekebisha wahalifu (re-habilitation). Jambo hili la kuwarekebisha wahalifu wakiwa katika kutumikia adhabu zao huwa gumu kwa sababu ya kukosa nyenzo, vifaa na mazingira ya kufanya hivyo.

Mheshimiwa Spika, Wizara ingeweza kulisaidia Jeshi letu la Magereza kupata mkopo wa kupata vifaa vya kufundishia, vifaa vya ujenzi kwa ajili ya kujenga karakana na madarasa. Jeshi letu hili lina wataalam wa kutosha, mfano mainjinia wa majengo (civil engineers), wachora ramani, mafundi umeme, mafundi bomba na wengine.

Mheshimiwa Spika, tukitumia force account wanaweza kujenga na kupanua magereza mbalimbali. Tukifanya hivyo tutakuwa tumesaidia Watanzania wengi sana watakaopata adhabu na wakitoka baada ya kifungo wawe na utalaam. Gereza liwe ni chuo cha ufundi, wafungwa wapewe vyeti vya kuhitimu mafunzo. Baadhi ya mafunzo yanayoweza kutolewa ni ufundi uashi, umeme, seremala, bomba, gesi, kuchomelea (welding), IT (computer), ushonaji, lugha mbalimbali na uchoraji.

Mheshimiwa Spika, pia kwa wale wanaosubiri kesi (mahabusu) wapate huduma bora zaidi kwa upande wa chakula, makazi, kupata taarifa mbalimbali kupitia redio au TV sababu inawezekana mwisho wa siku anatoka bila kuwa na kesi au adhabu kupitia mahakama.

Mheshimiwa Spika, Jeshi letu la Magereza lina uzoefu na wataalam wa kutosha katika fani mbalimbali, mfano, ujenzi wana usajili wa daraja la kwanza, kilimo, ufugaji, useremara na hata katika kuzalisha mali kupitia miradi mbalimbali na viwanda vidogo. Mfano Babati Magereza imeshirikiana na VETA kujenga jengo lenye thamani ya shilingi milioni 495 ambapo likiisha itafikia shilingi milioni mia tatu wameweza kuokoa shilingi milioni 195 kupita force account. Vilevile jengo la Uhamiaji Arusha lilijengwa na Magereza. Naomba jeshi letu lipewe vifaa vya kisasa vya ujenzi ili kitengo chao cha ujenzi kiweze kufanya kazi ya ukandarasi na washindane katika soko.

Mheshimiwa Spika, pia katika kilimo, ufugaji na uzalishaji mali (kusindika), Jeshi letu likopeshwa zana za kufanyia kazi kama matrekta, vifaa vyake (implements) ili waweze kuzalisha chakula chao na cha biashara na iwe sehemu ya shamba darasa. Kila mwaka katika Maonesho ya Nane Nane hupata kikombe cha ushindi ya kwanza. Wanafuga kuku, bata, ngombe, samaki, mbuzi na sungura kwa ufanisi mkubwa. Siyo lazima baadhi ya hivi vitu viwe kupitia bajeti, wanaweza kukopeshwa mfano matrekta na zana zake kupitia mfumo wetu unaokopesha raia wengine na pia kupitia TADB, Mfuko wa Pembejeo na taasisi zingine za fedha. Pia Serikali kupitia ruzuku na Magereza ipewe mashamba darasa ya kilimo, mifungo na usindikaji.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine muhimu ni suala la mazingira na matumizi ya nishati. Tunashauri Magereza zetu ziwe mfano ya matumizi bora ya nishati (kuni, mkaa na umeme). Leo hii magereza mengi hutumia kuni nyingi sana kwa ajili ya kupikia. Nashauri kwa kupitia CAMARTEC, magereza yote yajenge mifumo ya nishati ya kutumia gesi inayotokana na vyoo na mifungo (biogas na bio-latrine). Hii inaweza kupunguza matumizi ya kuni, pia kuweka mifumo ya solar, upepo na hiyo gesi utakayozalishwa kwa wingi (bio- latrine) wanaweza kupata nishati ya umeme na kupunguza gharama za umeme.

Mheshimiwa Spika, nashauri magereza yetu yote yawekewe mifumo ya kuvuna maji ya mvua. Hii itasaidia kupata maji ya matumizi ya kawaida na pia kupunguza gharama za malipo ya ankara za maji.

Mheshimiwa Spika, mwisho, nashauri taasisi chini ya magereza zinazozalisha mali ziimarishwe. Pia tuangalie namna ya kuwakopesha Askari wetu wa Magereza usafiri wa pikipiki au magari kutokana na nyadhifa zao na wawe wanalipa kwa mwezi. Vilevile kuwe na bulk procurement kwa vifaa vya ujenzi.

Mheshimiwa Spika, natoa pongezi na naunga mkono hoja.

Mheshimiwa Spika, naomba nichukue fursa hii kumpongeza Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu pamoja na walio chini yao ikiwa na Viongozi Wakuu wa Majeshi yaliyoko chini ya Wizara hii. Naomba nishauri katika maeneo machache.

Mheshimiwa Spika, Jeshi la Zimamoto na Uokoaji; naomba nishauri kwanza Jeshi hili lipatiwe zana za kutosha za kufanyia kazi yao vizuri. Leo hii kwa jina la Zimamoto tunatoza kila biashara, viwanda, mgodi na hata kilimo kwa ekari, gharama za fire inspection fee, ni fedha nyingi sana zinazokusaywa. Nashauri badala ya kuweka bajeti ya kununua vifaa vya kuzima moto na fedha huwa haitoki kwa wakati, makusanyo ya tozo tunayokusanya aslimia 20 ziende katika Mfuko Maalum wa Zimamoto ili waweze kununua vifaa vyao vyote.

Mheshimiwa Spika, hapo pia watapata bajeti ndogo ya kutoa elimu juu ya uokoaji wakati wa dharura kwa raia. Pia Wizara ifanye kazi karibu na mipango miji na taasisi za maji kuweka fire hydrants mabomba ya kutolea maji katika kila eneo ili wakati wa dharura zitumike. Huko miaka ya nyuma ilikuwa ni lazima kila eneo liwe na bomba la kutolea maji (fire hydrants).

Mheshimiwa Spika, pia nishauri Idara ya Uhamiaji ambao wanafanya kazi nzuri sana mifumo yao iunganishwe na NIDA, Polisi na Idara ya Kuandikisha Vifo na Vizazi. Itasaidia kupata taarifa mapema na ya uhakika. Nashauri Wizara kupitia Uhamiaji pia iangalie suala la uraia wa Watanzania ambao wamezaliwa Tanzania, wamekulia Tanzania, wazazi wao walizaliwa Tanzania ila hawakujua sheria na utaratibu wa kukaa na uraia wa awali na kupata cheti cha uraia wakati wa uhuru.

Mheshimiwa Spika, nipongeze jitihada za Wizara kupunguza ada ya kupata vyeti vya uraia kwa Watanzania ambao hawakufanya hivyo awali kutoka Dola za Kimarekani 5,000 hadi milioni mbili dependant pass kutoka Dola za Kimarekani 500 hadi 100,000 kwa depandant wa Kitanzania. Nashauri hawa Watanzania waliokuwa na vyeti hivyo tuweke muda maalum, mfano mwaka mmoja wapatiwe kipaumbele na viwango vya milioni mbili vipunguzwe na iwe angalau laki tano kwa kipindi hiki maalum na tuwaondoe hofu Watanzania hawa. Wengi hawana uwezo wa milioni mbili baada ya hapo tubaki na wanaoomba uraia wa kawaida.

Mheshimiwa Spika, pia haki ya kuomba uraia wa mwanaume aliyeoa mwanamke Mtanzania na mwenye watoto ambao Watanzania iwe na fursa ya usawa kwa uraia wa wanawake raia wa nje walioolewa na mwanaume Mtanzania, Fast Track.

Mheshimiwa Spika, pia Somo la Uraia litolewe kuanzia ngazi ya shule ya msingi na sekondari, itasaidia kuongeza uzalendo.

Mheshimiwa Spika, nayapongeza Majeshi yetu ya Zimamoto na Idara ya Uhamiaji kwa kazi nzuri inayofanywa.