Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017- Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji

Hon. Saed Ahmed Kubenea

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Ubungo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017- Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji

MHE. SAED A. KUBENEA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia hotuba ya Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naanza kwa kupongeza hotuba ya Msemaji wa Upinzani Bungeni aliyoitoa leo asubuhi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeambiwa na nimemsikiliza Waziri wa Viwanda akizungumza jinsi ya kuifanya Tanzania iwe ya viwanda, lakini katika hotuba nzima sijasikia Serikali ikisema kwa nini viwanda vyetu vilikufa? Nchi hii ilikuwa na viwanda vingi, ilikuwa na mashamba, ilikuwa na migodi na mabenki, yamegawanywa na yameuzwa kwa bei ya kutupa, halafu leo Serikali inakuja inasema inaanzisha viwanda.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilitegemea kwamba wangekuja na mkakati wa kutueleza kwanza viwanda vyetu vilikufaje. Tumeambiwa, baadhi ya Wabunge wamezungumza humu kwamba viwanda vyetu vimekufa kwa sababu Taifa hili halina uzalendo. Nikiangalia Waheshimiwa Wabunge na Mawaziri waliomo humu ndani upande huu wa pili, asilimia kubwa sio wazalendo. Viwanda hivi hata vikianzishwa vitakufa! Hata kuanzishwa, havitaanzishwa! (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hakuna fedha kwenye bajeti hii ya kuanzisha viwanda. Bajeti nzima imetengewa shilingi bilioni 80. Kiwanda kimoja zaidi ya shilingi bilioni 60, unajenga wapi hivyo viwanda? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikimwangalia huyu Waziri na mbwembwe alizokuja nazo asubuhi kwamba ataanzisha viwanda, namfananisha na yule aliyekuwa Waziri wa Habari wa Iraq wakati wa vita vya Ghuba ya Pili Al-Sahaf; ndiye mwenye mbwembwe kama hizi. Anaweza kukuaminisha pepo wakati bado uko hai, hujafa, akakwambia kuna chakula kiko hapo, kula, chakula hakipo! Huyu anafaa kuwa Waziri asiye na Wizara Maalum, ahamasishe kuzibua mito, ahamasishe kuzibua mitaro, hiyo ndiyo kazi anayoiweza, siyo kazi kubwa kama hii. Viwanda haviwezi kujengwa kwa namna hii. Huyu anaweza kufanya kazi ya uhamasishaji, ile ambayo inaweza kufanywa na watu wale.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2015 nilipata nafasi ya kwenda Uingereza. Nikiwa pale Uingereza nilitembelea kituo chetu cha biashara cha London. Nilikwenda Ubalozi, wakatueleza, pale London kuna kituo chetu cha biashara kinaitwa London Trade Center.
Kituo hiki kilianzishwa baada ya maelekezo ya Rais wa wakati huo mwaka 1989. Hali ya kituo cha London inasikitisha! Wafanyakazi wa Kituo cha London hawajalipwa mishahara toka Disemba mwaka 2015. Mkurugenzi wa Kituo cha London, nyumba yake inadaiwa kodi, hajalipwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wameandika barua chungu nzima kwenye Wizara, Mheshimiwa Waziri anazo barua hizo, wanakumbushia juu ya malipo ya mishahara, wanakumbushia malipo ya pango, lakini Serikali haijapeleka fedha London. Wakati Waziri anajibu hoja za Wabunge nataka alieleze Bunge hili Tukufu ni lini Serikali itapeleka fedha za mishahara London?
Mheshimiwa Mwenyekiti, kituo hiki kimefanya kazi kubwa sana ya kuitangaza Tanzania nje, lakini wafanyakazi wa kituo hiki wameachwa solemba, wameachwa yatima. Wameandika barua, kuna barua hapa ya tarehe 22 Februari, 2016. Kuna barua wanaeleza jinsi ambavyo wasivyokuwa na fedha, wako hoi, hata kazini hawawezi kwenda, hawana nauli, halafu mnaweka watu nje wadhalilike! Wamekopa, mpaka mzigo wa madeni umewazidi! Kama hamuwezi, warudisheni Tanzania, badala ya kuja na mbwembwe hapa mtaanzisha viwanda; mnashindwa kulipa wafanyakazi wenu waliopo London, mtaanzishaje viwanda? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukweli ni mchungu. Bahati mbaya sana, tukizungumza sisi tunaitwa wapinzani. Amezungumza Mheshimiwa Bashe, amewaambia mnahitaji miujiza ili muweze kutekeleza hii bajeti. Sisi tunazungumza kama Taifa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, huwezi kujenga nchi kama huna bandari. Sisi Mungu ametujalia tuna bandari, lakini bandari yetu tumeiua. Leo mizigo inayopita bandarini asilimia 40 ya mzigo imeshuka kwenye makontena. Matokeo yake, badala ya kuiendeleza bandari, kila siku tunakwenda kuvunja Bodi ya Bandari.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Harrison Mwakyembe amekuwa Waziri wa Uchukuzi, amekwenda kuvunja Bodi ya Bandari, akamfukuza na Mkurugenzi wa Bandari Mheshimiwa Mgawe; amekuja akaunda Bodi yake. Akaja Mheshimiwa Sitta akafukuza Bodi ya Mwakyembe; akaja Waziri Mkuu akafukuza Bodi ya Mheshimiwa Sitta na miongoni mwa Wajumbe waliofukuzwa ni Naibu Spika. Sasa haya ni mambo gani? (Kicheko/Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo bandari miezi mitano haina Bodi, haina Management, unaendeshaje nchi? Bandari haina Mkurugenzi, unaendeshaje nchi? Halafu unasema unaweza ukaleta Tanzania ya viwanda; viwanda vipi bila bandari? Ndiyo maana Waziri katika bajeti yake yote, anazungumza juu ya bomba la gesi linalotoka Uganda kwenda Tanga. Pia kuna reli inajengwa kutoka Uganda kwenda Rwanda. Katika mipango hii ya Waziri hakuna reli ya kutoka Kagera ambako ndiko karibu na Uganda, lakini hakuna mpango mkakati wa biashara katika mkoa huu; na huo ndiyo mkoa Waziri anakotoka! Mkoa wake! Hakuna biashara! (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sisemi afanye upendeleo, lakini hii ni kuonesha kwamba hakuna connection kati ya Waziri wa Viwanda na Biashara na Waziri wa Miundombinu, hakuna! Hiyo ndiyo Serikali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumefika mwaka 2015 wakati wa kampeni, mimi sio mwenyeji sana huko, Rais Magufuli aliongelea Special Economic Zone Kagera. Katika eneo alilolisema nadhani ni Omukanjuguti, labda akina Mheshimiwa Tibaijuka na Mheshimiwa Lwakatare wanaotoka huko, wanaweza kujua zaidi. Utueleze basi katika majibu yako, mipango gani ya kibiashara unayopanga kwa ajili ya kilimo cha mboga na matunda kinachohitajika uwanja wa ndege? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, haya mambo ya kuzungumza bila kuleta hoja nzuri hatutafika. Hapa tunazungumza juu ya mradi wa Mchuchuma na Liganga, lakini wale Wachina, nyaraka zilizopo na Serikalini mnazo, zinaonesha Wachina hawana fedha ya kuendesha huu mradi, wanataka kukopa dola milioni sita kutoka Benki ya Exim na dhamana yao ni Mchuchuma na Liganga.
Sasa mali yetu inachukuliwa dhamana halafu Mheshimiwa Nagu anasimama hapa anasema tuwe na viwanda. Alikuwa Waziri wa Viwanda na Biashara na ripoti ya CAG imesema ule mkataba ni fake, uvunjwe; Mheshimiwa Mama Nagu akiwa Waziri. Mambo gani? Mnaambiwa mnasema tunatukana. Sisi tunawaeleza! (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi hii haitaenda kwa ngonjera na usanii na kwa mtu kuwa Al-Sahaf. Nchi hii itakwenda kwa uchumi endelevu kwa watu kukaa kwenye meza, kuchora uchumi, kuendesha nchi kwa data, hesabu, numbers. Bila hesabu, bila namba, hakuna uchumi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalize kwa kusema kwamba Taifa letu limebahatika, lina utajiri mkubwa, lakini tusije tukarudia makosa wakati wa ubinafsishaji. Tuliuza mabenki, tukauza viwanda…
MHE. SAED A. KUBENEA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.