Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

Hon. Leah Jeremiah Komanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Meatu

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Spika, naomba nikushukuru kwa kunipatia muda ili niweze kuchangia katika hotuba hii ya Mambo ya Ndani. Awali ya yote, naomba nimpongeze na kumshukuru Mheshimiwa Rais kwa kazi nzuri anayofanya, Mheshimiwa Rais amekuwa akiguswa na matukio yanayohusishwa na wananchi kuuawa kutokana na ajali na matukio mbalimbali na Mheshimiwa Rais amekuwa akichukua hatua mara moja bila kusita. Naomba pia nimpongeze Mheshimiwa Waziri toka ateuliwe, akishirikiana na wasaidizi wake pamoja na Naibu Waziri wameweza kusimamia vizuri Wizara ya Mambo ya Ndani na kuweza kudhibiti matukio makubwa ambayo yalikuwa ni tishio kwa usalama wa raia yakiwemo uvamizi mkubwa katika mabenki yetu ambao ulikuwa ukigharimu maisha ya raia pamoja na askari wetu.

Mheshimiwa Spika, mauaji ya watu wenye albino, mauaji ya watu wenye albino yameweza kudhibitiwa, tumekuwa hatusikii yakiripotiwa. Naomba niwapongeze sana. Naomba pia nipongeze kwa upande wa mauaji ya vikongwe; sisi tunaotoka Kanda ya Ziwa, jambo hili lilikuwa kero na lilitutia aibu wananchi tunaotoka Mikoa ya Kanda ya Ziwa, lakini nipongeze Jeshi hili limeweza kudhibiti mauaji ya wazee wetu vikongwe. Vile vile ajali za mabasi zimekwisha ama zimepungua, matukio yamekuwa hayaripotiwi. Naomba waendelee hivyo hivyo walivyoanza kwa kuendelea kutoa elimu kwa madereva pamoja na raia.

Mheshimiwa Spika, Askari hao wanafanya kazi nzuri sana lakini wana changamoto katika mazingira ya kufanyia kazi pamoja na vitendea kazi ofisini. Ukifika vituo vya polisi hata karatasi za kuandikia maelezo ya mtuhumiwa wanapata shida, inalazimu wakati mwingine kuomba waletewe na hii pia itaweza kusababisha wasitende haki kwa sababu hata vitendea kazi havipo.

Mheshimiwa Spika, nyumba wanazoishi ni shida, naomba waongezewe bajeti ya kutosha ili askari waweze kujengewa nyumba bora, waweze kutoka uraiani. Vile vile nishukuru kwa kutenga bajeti kwa ajili ya kukamilisha maboma katika Wilaya ya Meatu ambayo yalikuwa ya mwaka toka 1999. Maboma haya nimekuwa nikiyaongelea toka nilipoingia Bungeni na swali langu la pili lilikuwa kukamilisha maboma hayo. Nawashukuru kwa sasa wametenga bajeti kwa ajili ya kukamilisha maboma.

Mheshimiwa Spika, pia niongelee upande wa dawati la jinsia. Dawati la jinsia lipo kwenye level ya wilayani katika kituo cha Polisi, lakini ukatili mkubwa unafanyika katika ngazi ya chini. Naomba waboreshe waone namna gani wanaweza wakafanya ili kuweza ku- accommodate yale matukio kwa wakati yanayotokea katika ngazi za chini, kwa sababu matukio mengi ya ukatili yanafanyika katika ngazi ya nchini.

Mheshimiwa Spika, katika kudhibiti ajali za bodaboda, pia naomba elimu itolewe kwa raia pamoja na waendesha bodaboda hususan katika uvaaji wa helmet, nashauri ili waweze kuvutia uvaaji wa helmet…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. LEAH J. KOMANYA: Usafi uzingatiwe.

Mheshimiwa nashukuru na naunga mkono hoja. (Makofi)