Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo

Hon. Dr. Harrison George Mwakyembe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kyela

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo

WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Spika, nianze kwa kushukuru Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kwa hotuba nzuri iliyosheheni maoni na ushauri ambao Wizara yangu inaahidi kuuchukua na kuufanyia kazi.

Mheshimiwa Spika, aidha, nitumie nafasi hii vilevile kuwashukuru Waheshimiwa Wabunge wote waliochangia katika hotuba yangu ya bajeti ya mwaka 2019/20 kwa kauli na kwa maandishi. Michango mingi iliyotolewa kwa kweli inalenga kuimarisha na kuendeleza Sekta ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo na ni sekta ambazo zinasimamiwa na Wizara yangu, hivyo, niseme tu kwamba michango yote tumeipokea na tutaizingatia katika utekelezaji wa majukumu kwani wajibu wetu sote ni kuwahudumia Watanzania waliotupa dhamana na wenye matarajio mbalimbali kwetu.

Mheshimiwa Spika, kutokana na muda, nitajibu machache. Kwa kifupi bajeti yangu imechangiwa na Waheshimiwa Wabunge 46 ambapo waliochangia kwa maandishi ni 28 na kwa kauli ni 18. Niwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge wote waliotambua jitihada zinazofanywa na Wizara katika kuendeleza sekta inazozisimamia kwa kutoa pongezi mbalimbali. Kwa niaba ya Wizara nazipokea pongezi hizo na ushauri uliotolewa kwa kuboresha zaidi utekelezaji wa majukumu yetu.

Mheshimiwa Spika, namshukuru vilevile Naibu Waziri kwa kutolea ufafanuzi hoja kadhaa, tena nyingi, kwa haraka. Nami nitatolea ufafanuzi hoja zingine chache kadri muda utakavyoruhusu.

Mheshimiwa Spika, nianze na mchango adhimu wa Mheshimiwa Dkt. Jasmine Tisekwa ambaye aliongelea masuala mengi muhimu kuhusu uzalendo na umuhimu wake katika maendeleo na ulinzi wa taifa. Ameongelea masuala ya Tunu za Taifa na umuhimu wake kwa maana ya utambulisho wa taifa ukiwemo Mwenge wa Uhuru, yote aliyoyasema namhakikishia Mheshimiwa Dkt. Tisekwa tumeyazingatia kwa maana ya kuyafanyia kazi ya ziada. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, moja tu la Mwenge nilitolee mkazo zaidi kwamba kila taifa duniani lina tunu zake ambazo zinalitambulisha na kulipa msingi wa uwepo wake na mwelekeo wa taifa hilo kisiasa, kijamii na kiuchumi. Waliotangulia kujitawala, chukulia wenzetu kama Wamarekani ambao wana Katiba ya mwaka 1787, wana stars and stripes (nyota na mistari) ambayo ni bendera yao na inaakisi historia na dira yao. Nyota zile 50 ni yale Majimbo yaliyoungana kuunda Marekani na ile mistari 13 ni yale makoloni yaliyomgomea Muingereza kuweza kuendelea kutawala. Pia wana tai kwenye nembo zao na tunu zao na yote hii inaashiria malengo pamoja na dhamira ya taifa hilo.

Mheshimiwa Spika, wenzetu Wahindi wana Tiranga, bendera yao yenye rangi tatu, ambayo inaashiria ujasiri, amani na imani. Vilevile katikati wana gurudumu ambalo linaelezea ndoto aliyokuwa nayo Mahatma Gandhi ya India kuwa na viwanda vya nguo kuweza kujitosheleza.

Mheshimiwa Spika, sisi tuna bendera yetu yenye rangi nne zinazoakisi amani na umoja na rasilimali tele ambazo Mungu ametubariki na ambazo sisi tuna wajibu wa kuzilinda kwa faida yetu na vizazi vinavyokuja. Pia tuna Mwenge wa Uhuru na Kiswahili. Kwa hiyo, utambulisho wetu umeainishwa kwenye sera, nina uhakika Waheshimiwa Wabunge wote wameiona Sera yetu ya Utamaduni lakini utekelezaji kisheria wa maudhui ya sera yetu haujawa wa kasi kutokana na Wizara zinazosimamia utamaduni kubadilika mara kwa mara, nafikiri tumekuwa na Wizara kumi zikisimamia utamaduni katika historia yetu.

Mheshimiwa Spika, nitoe tu mfano mdogo kwamba Sera yetu inasema lazima tuwe na taratibu maalum ambazo zitalinda hadhi ya utambulisho wetu. Nitoe mifano michache tu, kwanza, misingi ya Katiba ya Taifa ifundishwe kwa wanafunzi wote katika ngazi za elimu ya msingi na sekondari. Pili, Wimbo wa Taifa ufundishwe kwa wanafunzi wote kuanzia shule za awali na inasema Wimbo wa Taifa utaimbwa kila siku kabla wanafunzi hawajaingia darasani katika shule za awali, msingi na sekondari. Watu wote watasimama kuimba Wimbo wa Taifa kabla ya kuanza maonesho na michezo yote yenye hadhi ya kitaifa na kimataifa. Tatu, itakuwa marufuku kupandisha Bendera ya Taifa iliyopasuka au iliyopauka. Nne, Mwenge wa Uhuru utaendelea kukimbizwa nchini na Serikali itahakikisha kwamba wananchi wote wanauthamini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi naona ipo sababu pamoja na kwamba Wizara zinabadilikabadilika kwa hiyo utekelezaji wa maudhui wa mambo mengi imekuwa siyo rahisi sana, ipo sababu kwa kweli kwa Wizara kutafsiri maudhui ya sera kisheria ili tusiyumbe tena. Namshukuru sana Mheshimiwa Dkt. Jasmine kwa mchango wake.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa William Ngeleja ameongelea maendeleo ya soka nchini na wengine wengi wamegusia suala hili. Ni kweli kabisa tumepiga hatua kubwa pamoja na Timu yetu ya Vijana kukwama kusonga mbele katika Fainali za AFCON Jijini Dar es Salaam.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo, tumejifunza mengi, nimepata bahati ya kukutana na akina El Hadji Diouf, Tim Etoo na wengine ambao wapo Dar es Salaam kufuatilia vipaji vya Tanzania, wanasema Tanzania tayari ni kivutio cha mataifa na wataalam mbalimbali kuja kuangalia vipaji vilivyopo hapa. Siyo kwa kubahatisha ni kwa sababu sasa hivi, pengine Watanzania hatuoni tu lakini kwa kweli anayeongoza kwa ufungaji magoli Ulaya ni kijana kutoka Bara la Afrika na kijana kutoka Tanzania, kwa hiyo, tuna vivutio vingi sana. Tatizo letu ni kwamba tuko juu changamoto yetu ni kubakia hapo juu na kusonga mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ahsante Mheshimiwa Ngeleja kwa wazo la kuwa na sports academies kikanda ili kuvuna vipaji vikubwa tulivyo navyo pembe zote za nchi. Wazo ni zuri lakini haliwezi kufanywa na Serikali peke yake, tunahitaji kwa kweli ushirikiano wa karibu na sekta binafsi. Changamoto tuliyonayo ni kwamba tunapovumbua vipaji vizuri sana kupitia UMITASHUMTA na UMISETA na vipaji vingine mitaani, tunakosa mahali pa kuvilea kwa mpangilio.

Mheshimiwa Spika, wakati tunahimiza sekta binafsi kushiriki katika ujenzi kwa kweli wa hizo academies kwenye kanda zetu, Wizara kwa kushirikiana na TAMISEMI na Wizara ya Elimu kwa kweli tunataka tuanze mara moja kujadiliana na sports academies zilizopo na zipo nyingi, kama tano, sita, tuangalie tunaweza kushirikiana kiasi gani kuweza kuchukua vijana wenye vipaji. Tuna Azam, Alliance ya Mwanza, Trust St. Patrick Schools Arusha, Lord Baden-Powell ambayo ipo Bagamoyo na Fountain Gate Academy Dodoma. Nafikiri tukikaa chini tunaweza tukaanza mahali fulani tukasogea. Nakuhakikishia tutafanya hivyo ndani ya muda siyo mrefu kutoka sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nije upande wa habari lakini naomba nianze na utangulizi mfupi ili tuelewane. Habari yoyote inayoandikwa na kuchapishwa yenye athari ya kuharibu sifa ya mtu katika jamii ni kashfa. Ni haki kwa mtu aliyekashifiwa kwenda Mahakamani kudai fidia kwa maumivu aliyosababishiwa chini ya kifungu cha 41 cha Sheria ya Huduma za Habari ya Mwaka 2016. Mara zote tunawahimiza walalamikiwa kutumia kifungu cha 40 kuomba radhi (offer of amends) na ukiomba radhi kwa anayejisikia kuathirika, hakuna haja hata kwenda Mahakamani.

Mheshimiwa Spika, mara zote tunawasisitizia pia na ningependa pia hili lieleweke hapa kwamba tuepuke kujichukulia sheria mikononi kwa kumnanga aliyekukashifu kupitia njia mbalimbali za mawasiliano, sasa unaondoa uzito wa kesi yako mwenyewe. Wanasheria tunayo kanuni ya haki (equitable principle) ambayo inasema he who seeks equity should come with clean hands. Anayehitaka haki, basi njoo na mikono misafi. Ukisema umetupiwa madongo, kweli umejaa madongo kwenye shati na wewe umeshika madongo kumtupia mwingine, hoja yako haiwezi kuwa safi sana wakati na wewe una madongo mikononi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mkurugenzi wa Idara ya Habari ndiye mwenye mamlaka chini ya sheria ya kutoa Leseni ya Magazeti kuchapishwa na kuuzwa kwa kuzingatia masharti kadhaa. Hii siyo Tanzania tu, ipo duniani kote. Ana mamlaka chini ya sheria hiyo ya kifungu cha 9 ku-suspend, yaani kusimamisha leseni hiyo pala anapoona masharti ya leseni yanakiukwa. Tatizo la walio wengi, wakishasimamishiwa leseni, hawaendi Mahakamani, bali wanakimbilia kwenye Balozi. Hiki ni kitu cha ajabu nimekiona hapa nchini.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Devotha Minja alinioji, napata wapi mamlaka ya kufungia gazeti kwa muda; kama nilivyofanya huko nyuma? Nitamjibu, lakini nami namwomba kupita kwako atafakari ni kifungu kipi cha sheria kinasema usipokubaliana na Mkurugenzi wa Maelezo, basi kimbilia kwenye Balozi? Sijakiona hicho kifungu. Sijui, nadhani ni aina fulani ya ulimbukeni.

Mheshimiwa Spika, maana sheria inasema, kata rufaa kwa Waziri. Hakuna anayekata rufaa kwa Waziri na wanasema hata Waziri akishatoa uamuzi wake, bado una haki ya kwenda Mahakamani kumshungulikia huyo Waziri pamoja na Mkurugenzi. Hatutumii hiyo nafasi, tunakimbilia Ubalozi; na Balozi zinakuja kila mara kwetu nasi tunawajibu, mmesoma hiyo sheria?

Mheshimiwa Spika, nimalizie kwa kumjibu Mheshimiwa Devotha kuwa Waziri ana mamlaka chini ya kifungu 59 kinachosema, Waziri ana mamlaka ya kuzuia uchapishaji wa maudhui yenye athari kwa usalama wa nchi au amani katika jamii. Waziri anafikia hatua hiyo siyo tu haraka haraka, hapana. Ni baada ya mtu kuonywa au gazeti kuonywa mara nyingi sana; mara nane, tisa, kumi. Nyie hamwezi kuona hivyo, kwa sababu hamfanyi kazi kwenye hayo magazeti. Sisi tunafahamu, hatuchukui hatua hizi bila kumwonya mtu mara kadhaa. Hii ni kwa mujibu wa mkataba wa Kimataifa wa haki za kisiasa na kiraia ya mwaka 1966. Wengi hawapendi kuisikia hiyo, lakini ndiyo hiyo International Covenant on Civil of Political Right duniani kote tumeridhia na hata wakubwa wanaitumia hiyo hiyo. Wewe mchukulie kama Bwana Hasanja ambaye huu ni mwaka wa saba hayupo huru akikwepa kupelekwa Marekani kujibu mashitaka ya kuhatarisha usalama wa Marekani. Ila kwa sababu ni Marekani, aah, ila Tanzania ikitumia hiyo sheria, haki za binadamu kwa sababu pengine NGO’s nyingi zinafadhiliwa kutoka huko, hatuoni hiyo ya huyo anayetoa hela.

Mheshimiwa Spika, siyo kweli, kinyume na alivyosema Mheshimiwa Devotha kuwa tunafungia magazeti kila siku. Sasa kila siku kweli! Pengine hiyo ni lugha tu, siyo kweli. Tulifungia magazeti manne mwaka juzi, 2017 ili Waandishi na wamiliki na wadau waelewe kuna sheria mpya ambayo walikuwa hawaitaki. Hawaitaki tu, hata kuisoma hawajaisoma.

Mheshimiwa Spika, leo hii nikisema nimwulize mtu gani ameisoma Sheria ya Huduma za Habari, naomba Mungu awe shahidi yangu nina uhakika, hata wanaolalamika hapa hawajaisoma hiyo sheria. Ndiyo tatizo letu kubwa tulionalo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwaka 2018 sijafungia gazeti lolote; ni juzi tu Citizen waliadhibiwa na Mkurugenzi kwa siku saba kwa kushindwa kufuata masharti ya leseni baada ya kuonywa na kuonywa. Baadhi ya Waheshimiwa Wabunge wanadai kuwa Tanzanite halichukuliwi hatua, siyo kweli kwa sababu nyie hamko ofisini kwetu, uliza uweze kupata taarifa. Kwanza mnataka hatua zipi tuchukue? Kulifungia?

Ndugu zangu, malalamiko mengi zaidi ya Tanzanite, kama ilivyo kwa gazeti la Tanzania Daima na mengine, ni kashifa. Unakashiwa wewe, heshima yako imeshushwa; unaitaka dola ifanye nini kwa heshima yako kudhalilishwa? Nenda Mahakamani. Ukija kwetu, sisi kazi yetu kubwa ni kumwita chini ya kifungu cha 40 kumwambia omba radhi, huyu akikupeleka Mahakamani utalipa fidia kubwa. Wengi wanaomba radhi, wengine wanakwenda Mahakamani.

Mheshimiwa Spika, kwa sababu muda wenyewe ndiyo unakimbia hivi, Mheshimiwa Aida Joseph Khenani amedai usalama wa wanahabari nchini ni mdogo sana, kuna vitisho, yaani ni hatarishi. Bahati mbaya ametoka, napenda nimwombe Mheshimiwa Mbunge kupitia kwako atembelee tovuti www.forb.com. Forb ni chombo maarufu cha takwimu duniani aangalie taarifa yao ya mwisho wa Desemba mwaka 2019 inayohusu deadliest countries for journalist in 2018, nchi hatari kweli kweli kwa Waandishi wa Habari duniani. Inataja India, Mexico, Marekani yenyewe, Brazil na Israel. Tanzania hatumo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nawaomba Waheshimiwa Wabunge tupunguze Kauli kali sana hizi bila kufanya hata utafiti, pengine kwa sababu hatujui yanayotendeka sehemu nyingine.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Joseph Osmund Mbilinyi na Anatropia Theonest wameongelea uamuzi wa Mahakama ya Afrika Mashariki kukosoa baadhi ya vipengele kwenye Sheria ya Huduma za Habari ya mwaka 2016 na kutaka viondolewe baadhi ya vifungu. Hii ni mara ya tatu sheria hii inapelekwa Mahakamani. Mara ya kwanza tulikwenda Mwanza haikufanikiwa, mara ya pili Mahakama Kuu Dar es Salaam haikufanikiwa. Sasa imepelekwa Mahakama ya Afrika ya Mashariki.

Mheshimiwa Spika, nataka kusisitiza hii ni haki ya Watanzania wanapoona hawajaridhishwa na maamuzi, pengine wana wasiwasi na maamuzi ya vyombo vya ndani, nenda, ndiyo fursa. Ndiyo maana nchi yetu inajivuna kwamba tumewapa wananchi wetu uhuru mpana. Nenda; Mahakama ya Afrika Mashariki wamekwenda. Wengine wanachukulia kama Serikali hapa imeshtuliwa kweli kwa kupelekwa Mahakamani. Hapana, sisi ni Waasisi wa Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Mheshimiwa Spika, Mkataba wa Afrika Mashariki sehemu kubwa kwa Tanzania tumechangia na kuanzishwa hii Mahakama, nenda kwenye records, sisi ndiyo tumepiga kelele lazima tuwe na Mahakama ya Afrika Mashariki kwa sababu tunataka wananchi wetu wakiona hawawezi kupata haki, waende sehemu nyingine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka tu nisisitize kwamba uamuzi huo tumeona una upungufu na tarehe 11 mwezi huu Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali ilipeleka notes ya kusudio la kukata rufaa ngazi ya juu ya East Africa Court Justice. Sisi tunataka tu tuelewane kwenye vipengele mbalimbali, lakini kwa sababu liko Mahakamani sitalijadili sana. Tuna hoja nzito, nina uhakika tutashinda.

Mheshimiwa Spika, siwakatishi tamaa Watanzania wetu ambao mmepewa na nchi yenu uhuru mpana zaidi. Bado wana nafasi ya kwenda Mahakama ya Haki za Binadamu ya Afrika, ipo Arusha. Hiyo Mahakama iliazishwa mwaka 1998, nchi 30 zilikubali tukaanzishwa.

Mheshimiwa Spika, naomba ni sisitize, kuielewa nchi yetu ilivyo, ni nchi tano tu kwa muda mrefu zimekubali wananchi wake waweze kuishitaki Serikali kwenye hiyo Mahakama. Tanzania tumo, sasa hivi tuko tisa. Jamani, mnyonge, mnyongeni. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Khatibu Haji na Mheshimiwa Devotha Minja walioji kwa nini Mkurugenzi wa Maelezo alivitaka Vyombo vya Habari vilivyoandika habari za ACT vijieleze?

Mheshimiwa Spika, naomba nisisitize kuwa hali haikuwa hivyo. Tarehe 4 Aprili, Kiongozi wa ACT Wazalendo, Mheshimiwa Zitto aliitisha Mkutano na vyombo vya habari kutoa maoni yake kuhusu Ripoti ya CAG. Hili siyo kosa. Naomba nisisitize Watanzania; Mtanzania ana haki. Ripoti ya CAG iko pale, zungumza unavyotaka u-base kwenye hiyo ripoti, hatuna shida. Mheshimiwa Zitto alitumia haki yake ya kikatiba kuweza kujadili Ripoti ya CAG. Aidha, kisheria hakuna kosa lolote kwa chombo cha habari kunukuu kile kilichomo kwenye taarifa hiyo. Sasa nashangaa ilionekana kwamba tumezuia, haiwezekani kunukuu chochote, hapana, siyo hivyo. Tena naomba nisisitize kwamba tatizo lililojitokeza pale ambapo magazeti yalipoiacha Taarifa ya CAG na kujielekeza kwenye maoni binafsi ya Mheshimiwa Zitto.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Zitto alianzisha ya kwake, sasa tukawa na CAG wawili. Sasa kwa maadili ya Uandishi wa Habari, kwa sababu hiki ni kitu kipya, siyo based kwenye ripoti ya CAG, inabaidi umhoji na yule mwingine ambaye anatuhumiwa humo kwamba amepoteza shilingi bilioni 800, ni pesa hii kwamba haionekani, hiyo ni yake wala hata CAG hakusema. Ndiyo maana Mkurugenzi wa Habari akasema, jamani eeh, hebu elezeeni, mbona mnakiuka maadili? Hiki kitu kipya wala hakipo kwenye taarifa ya CAG. Kule kuuliza tu imekuwa nongwa; na hakuna hata mmoja aliyesimamishwa kwamba unasimamishwa kwa sababu ulimnukuu Zitto wa ACT.

Mheshimiwa Spika, naomba tu kusema kwamba Mkurugenzi wa Idara ya Habari alifanya hivyo kwa mujibu wa Kifungu cha 27 cha Sheria ya Huduma ya Habari, hakukosea popote. Mheshimiwa Joseph Kasheku ameongelea hali ya wana tasnia wa filamu; wapo wengi sana hapa; kuwa wana hali ngumu mno na hivyo wanasababisha kujihusisha na kula michango ya misiba; pili, kuendesha madanguro.

Mheshimiwa Spika, napenda kumwelezea Mheshimiwa Musukuma kupitia kwako kuwa vitendo hivyo havikubaliki kisheria. Ni kosa la jinai kuendesha madanguro. Ukisoma penal code cap 16, ni kosa. Namwomba tu Mheshimiwa Waziri wa Mambo ya Ndani asilichukulie hili kwa nguvu. Nadhani Mheshimiwa alikuwa anatia tu chumvi kidogo ili asikike zaidi hapa.

Mheshimiwa Spika, naelewa vijana wetu wa filamu wanafanya vizuri kuliko kipindi chochote katika historia ya nchi hii. (Makofi)

Ndugu zangu, kwa mara ya kwanza naweza pia kusema katika historia ya tasnia ya filamu, Wizara imeingilia kati mikataba ya wanatasnia wa filamu. Kwa mfano, Kampuni ya Jerusalem ya JB na Kampuni ya kijana wetu Kigosi RJ zililipwa jumla ya shilingi milioni 32 kwa intervention ya Wizara. Bodi ilikuwa pale kwa niaba ya Wizara, ikafanya kazi nzuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, siyo hiyo tu, tuna mifano mingi ambapo Kampuni, huyu Hussein Kim, amelipwa shilingi milioni
18 na Kampuni ya Proin Promotions na Puppy Zee. Ninachotaka kusema tu ni kwamba hebu rudi kwenye kitabu changu cha hotuba, tumefanya mengi sana kuweza kuisaidia tasnia ya filamu na sanaa nzima. Najivuna kwamba katika kipindi changu nimeweza hata katika kutetea vijana wetu, wasanii wawili, wanamuziki wameweza sasa hivi kuwa mamilionea kwa sababu wamelipwa zaidi ya shilingi bilioni mbili kwa haki ambayo ilikuwa inapotea. Bila Wizara kusimama kidete wasingepata hiyo pesa.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mwakajoka, amezungumzia uhuru wa habari. Ahsante kwa ufafanuzi ulioutoa Mheshimiwa Spika. Unajua uhuru anaoulilia Mheshimiwa Mwakajoka mdogo wangu pale. Sijui ndiyo ule uhuru wa mtu anaamka tu asubuhi anaamua kumfungisha ndoa Mheshimiwa Dkt. Mwakyembe na Mheshimiwa Halima Mdee! Maana ndiyo uhuru mnaoutaka huo, bila kujali kwamba unafanya hivyo wakati sisi watu wengine tuna familia, tuna watoto. Ina-impact kubwa sana, lakini ndiyo uhuru tunaoutaka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mtu amekaa tu; na uzuri wake nimewaomba wataalamu wa TCRA waangalie ni nani. Sitaki kumtaja jina hapa, ni mtu mzima ana familia yake, kakaa nyumbani anaanzisha rumors za kipuuzi kama hizo. Sasa hizo turuhusu, itakuwa nchi gani hii? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mwakajoka amemwongelea Ansbert Ngurumo. Nafikiri hao wengine aache tu wajitetee wenyewe kwa sababu nikisema niletee hapa ushahidi kwamba Ngurumo amewahi kutuhumiwa na Serikali hata siku moja; ndiyo utagundua kwamba watu wengine wanaenda Ulaya ni mshiko tu. Kwa kweli hajatuhumiwa na mtu yeyote yule.

Mheshimiwa Spika, nimalizie kwa sababu nimepigiwa kengele, niongelee kidogo tu kuhusu hoja aliyoelezea Mheshimiwa Juma Nkamia kwamba vijana wetu wa Serengeti kwa kweli hawakuandaliwa vizuri, pengine ndiyo maana hawakufanya vizuri sana, hapana. Mpira ni mpira. Tuliwaandaa vizuri sana.

Mheshimiwa Spika, niulize swali, hawa vijana wamechukua makombe competitive kama CECAFA na COSAFA kwa kubahatisha? Hapana, ni kwa sababu ya mazoezi mazuri waliyokuwa nayo, lakini mpira ni mpira, lazima mtu mmoja ashindwe na mwingine ashinde.

Mheshimiwa Spika, vilevile vijana wetu walikuwa na pressure kubwa mno ya kubeba matumaini ya Watanzania. Umri wa miaka 16 ni mdogo sana. Vilevile nawalaumu watu wanaoitwa ma-agents. Wamekuja ma-agents kutoka nchi mbalimbali, wote akina Diouf hao, kundi la Etoh, kuja kwa watoto wadogo wale unawaambia tunakuhitaji kwenye timu yetu, tutakulipa shilingi milioni 100 kwa mwezi, kanachanganyikiwa. Kanacheza pale kanaangalia ile hela; wazazi wengine wanapata taarifa kwamba mtoto wako bwana ameahidiwa shilingi milioni 100 mpaka 200 kwa mwezi. Wanawaambia, mwanangu usicheze, utavunjika mguu. Hii hela ndiyo itatutoa.

Mheshimiwa Spika, sasa nafikiri imetufundisha. Nimeiagiza BMT itengeneze Kanuni kwa ajili ya kuendesha shughuli za u-agency hapa nchini kuhusu vijana wetu. Nimalizie na Mheshimiwa Aida Khenani, kwamba Serikali inasema nini kuhusu Azory? (Kicheko)

Mheshimiwa Spika, kwa kweli niwaombe Waheshimiwa Wabunge, tunaongelea kesi ambayo ni dhaifu sana, tena sana. Mwandishi huyu amepotea. Eneo ambalo mamia ya Watanzania wengine wamepotea hawaulizwi wao, huyo mmoja ndiyo dhahabu. Halafu inaulizwa Serikali ambayo yenyewe imeshughulikiwa kwa kiasi kikubwa kweli kweli.

Mheshimiwa Spika, Maafisa wetu wa Serikali wamekufa wengi kule. Leo tunaulizwa mmoja, it is extremely unfair. Najua mnawalisha Wazungu na wafadhili wengi, matango pori hayo, acha wayapate, lakini ninachosema hatujakosa chochote, acha tushushwe hayo madaraja, sisi bwana uhuru wetu kwanza tunauthamini, hayo madaraja baadaye. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimalizie kwa neno moja tu kuhusu hoja ya Mheshimiwa Rashid Shangazi. Kwanza namshukuru kwa kunukuu Ibara ya 18 na 30 kwa pamoja, kueleza kwamba uhuru duniani kote lazima uwe mipaka. Walikuwa kuniona wale Waandishi wa (International Press Institute - IPI). Huyo Mhindi ndio alikuja akaniambia kwamba tumekuja Tanzania kwa sababu tuna taarifa ya kwamba kuna Waandishi wa Habari 30 wako kizuizini. Nikamwambia naomba usitoke ofisini kwangu unithibitishie hao 30 ni akina nani? Baadaye akaishia kusema nimeona kwenye mtandao wa jamii.

Mheshimiwa Spika, naomba niishie hapo. Naomba kutoa hoja. (Makofi)

WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, naafiki.