Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo

Hon. Joseph Leonard Haule

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Mikumi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo

MHE. JOSEPH L. HAULE: Mheshimiwa Naibu Spika, nichangie kidogo kwenye Wizara hii muhimu ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni ukweli kwamba wasanii wa Tanzania wanapata shida sana kutokana na usimamizi mbaya kwa maana ya ulinzi wa kazi za wasanii. Je Serikali haioni umuhimu wa kuileta kwenye Bunge lako Tukufu Sheria ya Hati Miliki na Hati Shiriti, Na.7 ili tuipitie upya na kuifanyia marekebisho? Kwani sheria hii imeshapitwa sana na wakati na inaonekana kuwa ndiyo chanzo cha wasanii wa Tanzania kuwa maskini na wengine kupata stress (msongo wa mawazo) na kujikuta wanajingiza kwenye matumizi ya madawa ya kulevya na unywaji wa pombe kupitiliza.

Mheshimiwa Naibu Spika, urasimishaji wa sanaa. Serikali haioni ikirasimisha rasmi wasanii itaweka mambo mengi kuwa rasmi na kusaidia Serikali kujua kipato cha kila msanii anachoingiza kupitia sanaa na kuweza kukusanya kodi yake vizuri tofauti na sasa ambapo vipato vya wasanii havijulikani na kusababisha Serikali kupoteza pesa nyingi kupitia kodi.

Mheshimiwa Spika, tumeona Serikali ikihangaika na mikataba mibovu waliyoingia wasanii na kunyonywa kwa kiwango cha ajabu na cha kusikitisha sana lakini mikataba kati ya wasanii na mashirika mbalimbali ingekuwa wazi ingesaidia sana mbali ya Serikali kupata kodi pia wasanii wangepata nafasi ya kuweza kukua zaidi na pia ingepelekea kupata ushauri mbalimbali juu ya kuwekeza (kuji-brand) zaidi ili kuwafanya wawe professional zaidi na kuepuka hali za wasanii wengi wa Tanzania ambao wengi wao wanakufa maskini kutokana na kutokuwa na msaada wowote wa kifedha na ushauri na mwisho wao kuwa mbaya na wa kusikitisha sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali iache kuwatumia wasanii kisiasa na ijikite kuwasaidia wasanii wawe neutral na kufanya shughuli zao za kitaifa na siyo kichama zaidi. Kwa kuwatumia wasanii kisiasa inawaumiza sana kwenye jamii kwani siyo kila shabiki wa muziki anaipenda CCM, hivyo kupelekea wale wasioikubali CCM kutowa-support kwa sababu wanatumiwa na CCM na mwisho wao kuwa mbaya, mfano, msanii Marlaw.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali iongeze bajeti ya BASATA maaana hawa ndiyo walezi wa sanaa ya Tanzania na pia ndio kama baba na mama wa sanaa ya Tanzania. Bajeti ya shilingi milioni 22 kwa mwaka ni ndogo sana na haitoshi kuwawezesha kuwafikia wasanii wote nchi nzima na kuwaelimisha na kuwasimamia kama majukumu yao yanavyojieleza.

Mheshimiwa Spika, lakini pia BASATA waache kufungia hovyo kazi za wasanii bila kufuata sheria kwani hakuna sheria inayoruhusu BASATA kufungia kazi za wasanii wa Tanzania. Kwa kufingia hovyo kazi za wasanii BASATA wanavunja sheria na wasipoangalia ipo siku watajikuta Mahakamani wakishtakiwa na wasanii wanaojielewa na itaharibu sana mahusiano kati ya wasanii na BASATA kitu ambacho kitadidimiza zaidi ukuaji wa sanaa yetu ambayo inategemea sana mahusiano mazuri kati ya wasanii na BASATA.

Mheshimiwa Naibu Spika, ieleweke BASATA ni mlezi wa sanaa ya Tanzania na siyo Mahakama ya kuwasulubu wasanii wa Tanzania. Naomba sana waitumie vema nafasi na heshima ya kuwa mlezi wa sanaa ya Tanzania na washirikiane vizuri na wasanii wa Tanzania kwa maslahi mapana zaidi ya sanaa ya Tanzania, Taifa letu na kizazi hiki na kizazi kinachokuja.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana.