Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo

Hon. Amina Saleh Athuman Mollel

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo

MHE. AMINA S. MOLLEL: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami nichangie bajeti ya Wizara ya Habari. Kama alivyosema mwenzangu Mheshimiwa Juma Nkamia na kwa sababu sisi wote ni wanataaluma, tumekuwa katika taaluma ya habari, naomba niseme kwamba hakuna uhuru usiokuwa na mipaka.

Mheshimiwa Spika, niseme tu kwamba, Tanzania ni nchi ya pili kwa Afrika Mashariki kwa uhuru wa habari, pamoja na kwamba imeshuka nafasi 10. Kwa mujibu wa report ya Without Borders na The Press Freedom Index ya 2018 Tanzania kwa Afrika na kwa dunia pia ni ya 93. Kenya yenyewe ni ya 96, Uganda ni 117, Rwanda ya 156 na Burundi ni ya 159. Kwa hiyo, utaona kwamba, Tanzania bado sisi ni kinara, tuko vizuri katika uhuru wa vyombo vya habari.

Mheshimiwa Spika, Tanzania pia imeshika nafasi ya pili kwa kuenzi uhuru wa habari na wa kisiasa. Imetanguliwa na Kenya kwa Afrika Mashariki na hii ni kwa mujibu wa report ya Freedom House ambayo ni ya mwaka huu wa 2019.

Mheshimiwa Spika, vilevile kwa sababu hiyo, tunakumbuka kwamba mwaka 2018 Rais wetu mpendwa Mheshimiwa Dkt. John Joseph Pombe Magufuli alichaguliwa pia kama kiongozi bora. Ni maoni na kura kutoka kwa wananchi katika Bara hili la Afrika ambao wametambua utendaji wa Rais wetu mpendwa kwa kazi kubwa anayoifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, naomba niendelee kwa kuchangia. Ninaomba niende moja kwa moja kwa Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC). TBC ni Shirika la Umma na mashirika yote duniani hata ukienda CNN, BBC, yote hayo yamefikia pale kutokana na jitihada nzuri za Serikali. Na mimi nina imani kubwa sana na Serikali na jitihada kubwa anazofanya Rais wetu katika kuhakikisha kwamba TBC inasimama.

Mheshimiwa Spika, zile fedha tulizopitisha mwaka 2018, hata kwa bajeti ya mwaka huu utaona ni kwa jinsi gani tunaliboresha Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC) ili liweze kuwa kama zamani lilivyokuwa pamoja na maslahi ya wafanyakazi wa TBC.

Mheshimiwa Spika, naomba pia, nizungumzie Waandishi wa Habari wa Tanzania. Hali ilivyo sasa ni mbaya. Waandishi wengi bado hawalipwi maslahi yanayostahili na wanafanya kazi katika mazingira magumu. Namwomba Waziri tuone ni kwa jinsi gani tunavyowasaidia Waandishi wa Habari ili basi na wao waweze kufurahia kazi yao.

Mheshimiwa Spika, sisi hapa bila Waandishi wa Habari, wananchi hawawezi kupata habari zinazoendelea.

MHE. PASCAL Y. HAONGA: Mheshimiwa Spika, kuhusu utaratibu.

MHE. AMINA S. MOLLEL: Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ninaomba…

SPIKA: Mheshimiwa Amina, Kuhusu Utaratibu.

KUHUSU UTARATIBU

MHE. PASCAL Y. HAONGA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi. Kanuni ya 64(1)(a) inasema, “Bila kuathiri masharti ya Ibara ya 100 ya Katiba inayolinda na kuhifadhi uhuru wa mawazo na majadiliano katika Bunge, Mbunge:-

(a) Hatatoa ndani ya Bunge taarifa ambazo hazina ukweli.”

Mheshimiwa Spika, mchangiaji anayeendelea kuchangia saa hizi amelieleza Bunge hili kwamba, Rais alichaguliwa kuwa Rais bora. Sasa naomba atusaidie tu kwa uelewa mpana kwamba hizi taarifa naona kama haziko sahihi, hizi kura zilipigwa wapi? Atusaidie tu kwa sababu, naona kama taarifa kidogo hazina…

SPIKA: Kanuni zetu zinasema wewe kwa kuwa umesema hajasema ukweli, wewe unausema ukweli sasa. Yaani wewe ndio uliambie Bunge ukweli ni upi? (Makofi)

MHE. PASCAL Y. HAONGA: Mheshimiwa Spika, kwa sababu, hili jambo sijawahi kulisikia, nataka tu kusema kwamba kwa nini Mbunge anayecha…

SPIKA: Sasa mbona umesimama kumbe hata hulijui! Basi huna hoja kaa. Endelea Mheshimiwa Amina, endelea na mchango wako. Endelea na mambo mengine tu. (Makofi)

MHE. AMINA S. MOLLEL: Mheshimiwa Spika, kwa kumsaidia tu aende katika Jarida la African Leadership Magazine ambalo lina Makao yake Makuu London, Uingereza, atapata taarifa hizi, lakini pia taarifa ziliwekwa wazi kwa vyombo vya habari. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niendelee kwa kuchangia. Niliishia pale kwa kuzungumzia Waandishi wa Habari. Naiomba Serikali na ninajua Serikali ni makini kuangalia kwamba hata baadhi ya wamiliki ambao hawawalipi Waandishi wa Habari ambao ni waajiriwa wao maslahi wanayostahili. Wapo ambao bado wanadai mishahara yao. Waandishi wa Habari kwa kweli wana hali ngumu. Namwomba sana Mheshimiwa Waziri kulisimamia hili kuhakikisha kwamba hawa waandishi wa habari wanaweza kulipwa maslahi yao.

Mheshimiwa Spika, tuzungumzie pia suala zima la wasanii. Wasanii wa kizazi kipya wamekuwa na mchango mkubwa sana katika nchi hii. Nakumbuka wakati nafanya kazi ya Uandishi wa Habari miaka ya 1990 nyimbo zilizokuwa zimetawala ni kutoka Congo, kutoka Mataifa ya nje, lakini muziki wa kizazi kipya umebadilisha hiyo mentality na hivi sasa katika vyombo vyetu vya habari, redio, TV na hata maeneo mbalimbali ni muziki wa kizazi kipya.

Mheshimiwa Spika, ukienda Kenya, utaona jinsi ndani ya Afrika Mashariki, Tanzania tunavyoongoza kwa muziki huu wa kizazi kipya. Tuone sasa ni kwa jinsi gani tunawapatia haki zao, ambapo nakumbuka tulipitisha sheria kuona ile percentage wawe wanalipwa. Je, napenda kufahamu kwamba ile sheria tuliyopitisha, tayari imeshaanza kufanya kazi?

Mheshimiwa Spika, je, tunajiandaa vipi katika kujenga kumbi za kisasa kama walivyo wenzetu, nchi zilizoendelea? Ukienda India kuna Bolywood, ukienda Marekani pia hivyo hivyo. Sasa je, tunafanyaje kwa nchi yetu hapa Tanzania? Tunaona sasa hivi filamu zimeporomoka hapa nchini kwa kweli, siyo kama ilivyokuwa. Naomba Waziri atuambie kwamba ni kwa sababu gani?

Mheshimiwa Spika, niende pia kwa Msemaji Mkuu wa Serikali. Mimi binafsi nampongeza kwa kazi kubwa na nzuri anayoifanya katika kuhakikisha kwamba yale yanayofanywa na Serikali yetu jamii na Watanzania wanatambua; lakini tuna umuhimu wa kuhakikisha kwamba Ofisi hii ya Msemaji Mkuu wa Serikali inakuwa siyo idara, iwe ni ofisi maalum ambayo itakuwa na uhuru mpana zaidi.

Mheshimiwa Spika, pia, kama ilivyokuwa Dar es Salaam tunaona Serikali imehamia hapa, lakini je, hapa Dodoma Hakuna Idara ya Habari Maelezo? Wakitaka kuzungumza, wengi tutawasikia wamekwenda Dodoma Hotel na maeneo mengine. Tunahitaji kuwa na ukumbi wa kisasa ambapo watu mbalimbali watakwenda hapo kwa ajili ya kwenda kuzungumza na Waandishi wa Habari na sivyo kama ilivyo sasa hivi ambapo hatujui na hatujaona Ofisi Maalum ambayo ni ya Mtendaji Mkuu wa Serikali ambaye ni Msemaji.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naomba sana Mheshimiwa Waziri atakapokuja ku-wind up atueleze ni kwa namna gani basi Serikali imejipanga katika kuhakikisha kwamba tunapata Ofisi Maalum ya Msemaji wa Serikali ambaye anafanya kazi nzuri sana katika kuweka mambo mazuri yanayofanywa na Serikali yetu ya Chama cha Mapinduzi.

Mheshimiwa Spika, mwisho kabisa, kutokana na utendaji huo ndiyo maana waafrika wengi wanatambua jitihada anazofanya Mheshimiwa Rais wetu. Nasi pia tunamuunga mkono Mheshimiwa Rais wetu kwa kazi kubwa anayofanya na tunazidi kumtia moyo kuona kwamba tunakwenda katika nchi ya viwanda ambayo uchumi wake unakua. Pamoja na changamoto hizo tulizonazo…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. AMINA S. MOLLEL: Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. Tanzania Rais Magufuli na Serikali yake nawaombea Mungu na iendelee kusonga mbele. Ahsante. (Makofi)