Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Katiba na Sheria

Hon. Shabani Omari Shekilindi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lushoto

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Katiba na Sheria

MHE. SHAABANI D. SHEKILINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa naunga mkono hoja ya Katiba na Sheria kwa asilimia mia moja. Pia nampongeza Waziri Mheshimiwa Balozi Dkt. Mahiga na timu yake yote kwa kazi nzuri wanayoifanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Lushoto ina Majimbo matatu na Halmashauri mbili, na jiografia yake ni ya milima milima na mahakama zilizopo ni chache mno ambazo hazikidhi huduma kwa wananchi. Kwa hiyo, niiombe Serikali yangu Tukufu itujengee Mahakama za Mwanzo hasa katika maeneo ya Malibwi na Ngwelo. Pamoja na maeneo hayo ambayo hayana mahakama, kuna mahakama ambazo zinahitaji ukarabati. Mfano, Mahakama ya Gare na Mahakama ya Mlola.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mahakama ya Gare pamoja na kuomba kukarabatiwa, pia haina watumishi, wakati Mahakama ya Gare ilikuwa inafanya kazi, lakini nilishangaa mahakama ile imefungwa, kuuliza sababu nikaambiwa hakuna watumishi. Mahakama ile inasaidia zaidi ya kata nne, yaani Kata ya Kwemashai, Gare, Migambo, Kwai, Kata jirani ya Baga na Malibwi. Kwa hiyo, kufungwa kwa mahakama hii imesababisha usumbufu mkubwa sana kwa wananchi hao. Naiomba Serikali irudishe huduma hii haraka pamoja na ukarabati wa haraka ili wananchi wasipate usumbufu wa kutembea umbali mrefu kufuata huduma hiyo. Pia niiombe Serikali yangu Tukufu itoe ajira kwa watumishi katika mhimili huu wa mahakama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo, mahakama hizi zote mbili hazina vifaa kama photocopy machine, computer kwa ajili ya kurudufu nakala za hukumu na mambo mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mahakama ya Wilaya ya Lushoto ni ya zamani sana, kwa hiyo, niiombe Serikali yangu kama siyo kukarabati basi kujengewa mahakama nyingine ili na sisi wananchi wa Lushoto tuwe na mahakama ya kisasa na inayoendana na wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi wananchi wa Wilaya ya Lushoto tuna bahati ya kuwa na Chuo cha Mahakama Lushoto (IJA), lakini wananchi walio wengi hasa wa vijijini wanadhulumiwa haki zao na kutokana na wananchi hawa kutojua sheria. Sasa basi niiombe Serikali yangu Tukufu kwa kuwa tuna Chuo cha Mahakama, niiombe Serikali yangu wakati wanafunzi wanakwenda field basi waende vijijini hasa katika Vijii vya Lushoto ili wananchi wa Lushoto waweze kufaidika na fursa ya kuwa na Chuo cha IJA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo pia kuwe na dawati la kutoa elimu ya sheria kwa wananchi wa Lushoto na elimu hiyo itolewe na Uongozi wa Chuo cha Mahakama (IJA).

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuwasilisha na naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. Mungu ibariki Tanzania, Mungu mbariki Rais wetu Dkt. John Joseph Magufuli.