Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Katiba na Sheria

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Katiba na Sheria

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mara nyingine tena naomba nichukue fursa hii kumpongeza sana Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa hatua mbalimbali katika kuhakikisha haki na utu wa kila Mtanzania unathaminiwa kwa kuimarisha Wizara hii muhimu katika kusimamia usawa na upatikanaji wa Hakimu katika kutafasiri katiba na sheria mbalimbali.

Hata hivyo, nawapongeza pia wateule wote walioko chini ya Wizara hii wakiongozwa na Mheshimiwa Waziri Augustine Mahiga bila kuwasahau watumishi wote walioko katika Wizara hii.

Mmheshimiwa Mwenyekiti, ni Sera ya Taifa kuwa kila kata nchini iwe na huduma ya Mahakama ya Mwanzo na kila Wilaya kuwa na Mahakama za Wilaya, lakini katika Wilaya la Liwale pamoja na kuwa ni Wilaya ya siku nyingi, tangu mwaka 1975 Wilaya hii ina Kata 20 lakini ina Mahakama mbili tu ya mwanzo, yaani ile ya Liwale mjini na ya kata ya Kibutuka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile Wilaya ya Liwale hadi leo haina jengo la Mahakama ya Wilaya. Jengo linalotumiwa ni lile lililokuwa la Mahakama ya Mwanzo ya Liwale Mjini. Upo uhitaji mkubwa sana wa jengo la Mahakama Wilayani Liwale, sambamba na uwepo wa watumishi wa kutosha. Wilaya pia inahitaji kuwa na Mahakama ya Mwanzo kwenye Kata za Lilombe na Miruwi kwa kuwa kata hizo zina shughuli mbalimbali za uchumi ikiwepo uchimbaji wa madini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, uwezo wa watumishi wa Idara ya Sheria ni mdogo sana jambo linalosababisha Halmashauri zetu kuingia mikataba isiyo na tija na kuzisababishia Halmashauri kuingia kwenye migogoro ya kisheria mara kwa mara. Pia watumishi hawatoshi, kuwepo kwa mwanasheria mmoja kwenye Idara ya Sheria kunapunguza ufanisi kwenye Idara ya Sheria na Halmashauri zetu. Mfano Wilaya ya Liwale ina mtumishi mmoja tu kwenye idara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tume ya Kurekebisha Sheria ni bora ikafanya mapitio ya sheria mbalimbali mara kwa mara kwani zipo sheria nyingi zinazohitaji kufanyiwa mapitio. Ili zifanyiwe marekebisho ziendane na wakati uliopo kwani kuwepo kwa sheria zilizopitwa na wakati ni kuwapora haki wananchi. Mfano sheria inayoruhusu Serikali kumkamata tena mtuhumiwa aliyefutiwa mashtaka na Hakimu baada ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kushindwa kupeleka mashahidi Mahakamani, ni sheria inayojaza mahabusu kwenye Magereza zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sheria nyingine ni ile ya maliasili kuhusu kifuta machozi kwa waathirika wa kushambuliwa au mashamba kuliwa na wanyama waharibifu. Ni bora sasa wakapewa fidia badala ya hicho kinachoitwa kifuta machozi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Ofisi ya Mwendesha Mashitaka Mkuu imekuwa ni sababu kubwa ya kulundikana kwa mahabusu nyingi; imekuwa ikishindwa kupeleka majalada mbalimbali Mahakamani, hapa ndipo hadi sasa pana rushwa kali sana. Ili jalada lifike Mahakamani, ni lazima mhusika atoe chochote hasa zile kesi kubwa kubwa. Ofisi hii pamoja na changamoto za kifedha, bado kuna utendaji usiozingatia misingi ya Utumishi wa Umma. Ndiyo sababu ya Mahakimu kufuta mashitaka na Mwanasheria Mkuu kuwakamata tena kwa sheria niliyoitaja hapo juu. Wapo mahabusu wengi kwenye Magereza nchini wakisubiri majalada toka kwa DPP.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri kwamba Ofisi ya Mwanasheria Mkuu ni vyema ikawa na Wanasheria waliobobea kwenye fani ya sheria na wanaoijua jamii ya Watanzania na mazingira halisi ya nchi yetu, kwani Miswada mingi inayoletwa Bungeni kwa ajili ya kutungiwa sheria na mengine kukosa kabisa uhalisia kiasi cha kudhani watu wanaoandaa Miswada hiyo sio watu wanaotoka katika jamii yetu; kiasi cha kufanya Miswada inayoletwa na Serikali kufanyiwa marekebisho na Bunge pengine ni kwa asilimia zaidi ya 80. Hili huchangia kulifanya Bunge kutunga sheria inayodumu kwa muda mfupi.