Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze mchango wangu kwa kumshukuru Mungu kwa kunipa uhai na kuniwezesha kushika kalamu na kuchangia hoja hii. Pia napenda kuipongeza Serikali kwa kuja na hoja ya kupiga marufuku matumizi ya mifuko ya plastic nchini. Kwa hili, pongezi kwanza zimwendee Mheshimiwa Waziri Mkuu kwani yeye ndiye kwa kwanza kuja na tamko hili. Vilevile, nampongeza Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana kwa kuona umuhimu wa jambo hili na kuamua kuchukua hatua, tena niseme hatua hii imecheleweshwa sana hapa nchini, kwani athari za kimazingira juu ya matumizi ya mifuko hii ya plastic ni kubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nizungumzie uharibifu wa mazingira utokanao na shughuli za kibinadamu kama vile kilimo cha kuhamahama, biashara ya mazao ya misitu na ujenzi wa miundombinu mbalimbali za kimaendeleo. Mfano, katika Wilaya ya Liwale, Wilaya hii imezungukwa na misitu ya asili; na kwa kuwa huko nyuma hali ya miundombinu ya barabara ilikuwa siyo mizuri, uharibufu wa misitu hii haukuwa mkubwa sana lakini kwa sasa uvunaji wa magogo, mbao na mkaa ni biashara inayokua kwa kasi sana na ni uvunaji usiozingatia sheria na kuwaachia wananchi wa Liwale jangwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kiasi cha ushuru Halmashauri inachopata hakiwezi kurudisha uoto wa asili wa misitu hiyo kwani miti imekuwa ikipandwa pembeni mwa majengo ya taasisi za Umma kama shule, hospitali na kadhalika, lakini kule ambako miti hii imekatwa kunabaki kuwa jangwa. Hivyo, napendekeza Wizara ya Maliasili na Wizara ya Mazingira zikafanye kazi kwa pamoja kutafuta namna bora ya kuona misitu au miti inarudishiwa kupandwa pale mti ulipokatwa na Ikiwezekana fedha za upandaji miti ziongezwe na zikasimamiwe moja kwa moja na Halmashauri husika. Kiasi cha asilimia tano cha sasa kinachotokana na uvunaji wa mazao ya misitu kifanyiwe marekebisho ili kiendane na aina au kiasi cha uharibifu unaotokea, hivyo Halmashauri iweze kupanda miti ya kutosha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, elimu zaidi inahitajika juu ya utunzaji wa mazingira hasa kwenye utunzaji wa vyanzo vya maji. Ufugaji wa samaki pembezoni mwa mito ni bora ukapigwa marufuku, kwani mito mingi sasa imeanza kukauka baada ya watu kuchimba mabwawa ya samaki pembezoni mwa mito. Urinaji wa asali kwa njia za kizamani unachangia kwa kiasi kikubwa uharibifu wa misitu kwa kuchoma moto na kuharibu maisha ya viumbe vingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa naomba nichangie kidogo kuhusu Muungano wetu. Kwa kuwa Muungano huu ni wa muda mrefu, kizazi cha leo hakina uelewa wa kutosha kwa nini nchi hizi mbili; Tanganyika na Zanzibar ziliamua kuungana na faida za Muungano wetu na hivyo, kutambua dhamira ya Waasisi wetu. Ndiyo maana kizazi hiki kimeishia kuangalia changamoto tu za Muungano bila kuangalia faida zake kwa pande zote mbili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo basi, nazishauri Serikali zote mbili za Muungano kuwekeza zaidi kwenye elimu ya kuelimisha jamii ya leo kuelewa Muungano. Pia pale panapotokea changamoto, basi Serikali zote mbili zichukue hatua za haraka kutatua changamoto hizo kabla hazijaota sugu na kuchafua sura nzuri ya Muungano wetu, tena nyingine zinapaswa zitatuliwe na ngazi za Taasisi za chini kama zile za Uhamiaji, TRA na ZRA. Hivyo, naiomba Serikali kulinda na kudumisha Muungano huu kwa gharama yoyote ile.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa naomba nizungumze juu ya uchafuzi wa mazingira unaofanywa na viwanda vinavyotoa moshi au vumbi mawinguni. Jambo la viwanda vinavyorusha moshi angani na teknolojia iliyopitwa na wakati huchangia kwa kiwango kikubwa uchafuzi wa hali ya hewa ikiwa ni pamoja na magari yanayotoa moshi kupita kiwango.

Mheshimiwa Mwenyekiti, viwanda vinavyotoa moshi nashauri viwe vinatozwa tozo za uchafuzi wa mazingira ili iwe kama ni juhudi za kulinda mazingira, kwani sasa nchi za wenzetu viwanda hivi sasa haviko tena na pale vilipo, teknolojia yake haitoi tena huo moshi. Hivyo basi, imefika wakati sasa kuazima teknolojia hiyo ili kulinda mazingira yetu. Viwanda hivi ni kama vile vya cement, chuma na viwanda vya nafaka kama ngano na vile vya kuchakata kokoto na Marumaru.