Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira

Hon. Augustino Manyanda Masele

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbogwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira

MHE. AUGUSTINO M. MASELE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja ya Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa napenda kuchangia zaidi katika suala la mazingira hasa juu ya uharibifu wa mazingira unaotokana na ukataji wa miti hovyo kwa matumizi mbalimbali ikiwemo uchomaji wa mkaa, kuni, utayarishaji wa mashamba na kadhalika. Uharibifu huu unafanyika bila ya kuwepo hatua madhubuti za kuhakikisha nchi yetu haiwi jangwa. Watanzania walio wengi hawana destruli ya kupanda miti ni mabingwa wa kukata miti na hawaelewi kuhusu uharibifu wa mazingira. Ifike mahali Serikali ichukue hatua kali kabisa dhidi ya Watanzania wenzetu wanaoharibu mazingira kwa kukata miti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri zitungwe sheria za kumtaka kila Mtanzania mwenye umri wa kuanzia miaka 18 kupangiwa utaratibu wa kupanda miti angalau 10 kwa mwaka kwa kuwa miti ndiyo chanzo cha mvua na hifadhi ya mazingira. Bila kuchukua hatua za makusudi, Tanzania inakwenda kugeuka jangwa ndani ya kipindi kifupi. Hivyo basi ni wajibu wa Serikali kuchukua hatua madhubuti kukabiliana na hali hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ongezeko kubwa la watu na wanyama wafugwao kunachangia kwa kiwango kikubwa uharibifu wa mazingira. Kuna umuhimu mkubwa kuingiza masomo yanayohusiana na uhifadhi wa mazingira katika mitaala ya elimu nchini kuanzia chekechea hadi chuo kikuu. Madhara ya uharibifu wa mazingira ni pamoja na ukame, mafuriko na mmomonyoko wa ardhi. Ipo sababu ya msingi kabisa kwa Serikali kusisitiza umuhimu wa kuwataka Watanzania kujenga tabia ya kupenda mazingira kwa kuzuia ukataji miti badala yake wawe wanapanda miti katika mashamba yao na kwenye makazi yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina ushauri ufuatao:-

(i) Uzazi wa mpango upewe kipaumbele;

(ii) Idadi ya mifugo inayohamahama ipunguzwe;

(iii) Watanzania wanaofanya biashara ya mkaa wapewe masharti ya kuwa na mashamba ya kupandwa kwa ajili ya ukataji miti ya kuchoma mkaa; na

(iv) Kila Mtanzania mwenye umri wa kuanzia miaka 18 apewe malengo ya kupanda angalau miti 10 au zaidi katika mashamba na kwenye viwanja vya makazi, maeneo ya biashara na makazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.