Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote nichukue nafasi hii siku ya leo kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha kuendelea kuniweka hai na afya njema na leo kunipa uwezo wa kutoa mchango wangu kwenye hoja hii. Pia nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Rais Mheshimiwa Dkt. John J.P. Magufuli kwa kuliongoza Taifa letu kwa uadilifu mkubwa na kwa umahiri anaouonesha katika kusimamia rasilimali ya nchi yetu ili ilete manufaa kwa Watanzania wote. Uongozi unaozingatia, Katiba, usawa, haki, sheria na utu. Jambo linaloendelea kudumisha amani ya nchi yetu. Kwani hivyo ndivyo vielelezo vya amani yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa naomba nianze mchango wangu kwa kuishauri Serikali katika mambo yafuatayo:-

Kwanza, Watumishi wa Umma; kumekuwa na uhaba mkubwa sana ya watumishi katika Idara mbalimbali za Sekta ya Umma kama vile afya, elimu, ugani, Mahakama na kadhalika. katika idara nyingi za umma watumishi wengi wamekuwa wakikaimu, nafasi mbalimbali za utumishi, nafasi hizi wanakaimu kwa muda mrefu kiasi cha kuwapunguzia ufanisi katika suala la upungufu wa watumishi. Mfano Wilaya ya Liwale ina upungufu kama ifuatavyo:-

(a) Walimu shule za Msingi upungufu 298;

(b) Afya zahanati na vituo vya afya 261; na

(c) Maafisa Ugani upungufu ni 28.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hawa wachache waliopo, kuna ucheleweshaji mkubwa wa kupandishwa madaraja na pale wanapopandishwa madaraja mishahara mipya huchelewa kutolewa. Hivyo kupelekea Serikali kuwa na madeni mengi au makubwa.

Pili, ni TASAF; nashauri Serikali kufanya utafiti wa kutosha ili wale walionufaika na kuonekana wameshatoka kwenye kaya maskini ili waweze kuondolewa na wengine kupewa hizo nafasi, kwani bado ziko kaya nyingi zenye uhitaji hazijafikiwa na utaratibu huu. Vilevile Serikali ione umuhimu wa kuendelea kushirikisha wanufaika wa TASAF kwenye kubuni miradi mbalimbali, kwani iko miradi iliyoshindwa kufikia mafanikio tarajiwa kutokana na miradi kutokuwa shirikishi kwa wanufaika.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika dhana ya utawala bora Serikali ione umuhimu wa mafunzo kwa wateuliwa wapya juu ya majukumu yao. Uzoefu unaonyesha mara wateule hao wanapotekeleza majukumu yao wengine wanashindwa kujua mipaka ya majukumu yao. Aidha, Serikali ione umuhimu wa kuimarisha au kuboresha Chuo cha Utumishi wa Umma, sambamba na hilo kuwe na utaratibu wa kila mtumishi wa umma awe amepitia kwenye Chuo hicho hata kwa angalau miezi mitatu (3) iwe mara baada ya kuajiriwa au kuteuliwa kwa nafasi au ajira husika. Kama ilivyo kwa Chuo cha Utumishi wa Umma vilevile Serikali ione umuhimu wa viongozi kwenye ngazi mbalimbali wawe pia wamepata mafunzo ya uongozi. Kozi au mafunzo hayo, yatawajengea watumishi au viongozi hao kufanya kazi kwa uzalendo, utaifa na ufanisi mkubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kwamba Idara ya Polisi na Mahakama kuonekana ina tatizo kubwa la rushwa, lakini rushwa iliyoko kwenye Idara ya Uhamiaji ni ya hatari zaidi na idara hii rushwa zake ni ngumu sana kuzigundua, pamoja na madhara yake ni makubwa sana. kama ilivyo kwa Idara ya Uhamiaji, vilevile Idara/Wizara ya Uwekezaji inakuja kwa kasi kubwa sana jambo linalopunguza ari kwa wawekezaji wa ndani na nje. Hivyo nashauri Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa nchini kutupia macho sana taasisi hizi mbili nilizozitaja hapo juu. Sababu ya kutamalaki kwa rushwa kwenye Taasisi hizi ni kutokana na sababu kuu mbili:-

(1) Upungufu wa watumishi kwenye idara hizo; na

(2) Urasimu mkubwa uliopo unaotokana na watumishi wengi kushindwa kutoa maamuzi hata yale yaliyo chini au ndani ya uwezo wao, hivyo kufanya hali ya njoo kesho, njoo kesho zinakuwa nyingi na kutengeneza mazingira ya rushwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho kabisa, napenda kutoa pongezi kwa wateule wote katika Wizara hii wakiongozwa na Waziri mwenye dhamana pamoja na Naibu wake, bila kusahau, viongozi wa taasisi zote zilizo chini yake, kwa kazi kubwa wanayoifanya katika kulitumikia Taifa hili kwa weledi mkubwa. Kazi hii ya kutukuka inathibitishwa na amani na utulivu uliopo hapa nchini. Kwani ni jambo lililo wazi hakuna amani wala utulivu, mahali ambapo hakuna utawala bora.

Mungu ibariki Tanzania, Mungu ambariki Rais Mheshimiwa Dkt. John J. P. Magufuli.