Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

Hon. Janet Zebedayo Mbene

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ileje

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

MHE. JANET Z. MBENE: Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru Mungu kwa fursa hii ya kuwepo hapa kujadili hotuba hii ya Wizara muhimu sana katika kuchangia na kukuza maendeleo ya Taifa letu. Nakushukuru kwa fursa ya kuchangia.

Mheshimiwa Naibu Spika, nachukua fursa hii kumpongeza Mheshimiwa George H. Mkuchika, Mbunge wa Newala na Waziri katika Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora; Naibu Waziri, Mheshimiwa Dkt. Mary Mwanjelwa, Katibu Mkuu na Watendaji wote na taasisi zote zilizo chini ya Wizara hii kwa kazi kubwa wanayofanya kuhakikisha kuwa utendaji wa Serikali ni mzuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa kuipongeza Serikali kwa utekelezaji mzuri wa mpango wa kurasimisha rasilimali na biashara za wanyonge (MKURABITA). Mpango huu ni muhimu sana kwa kuhakikisha kuwa wananchi wote wenye uwezo wanajumuishwa kwenye uchumi wa nchi kwa kuwawezesha kutumia rasilimali za kukopa au kuwekeza kiuchumi. Kwa umuhimu wa mradi huu na faida na mafanikio yaliyopatikana hadi sasa, tunapenda kuona Serikali ikizidisha juhudi katika kuwekeza fedha nyingi zaidi kuthamini na kutoa hati nyingi zaidi nchi nzima hasa kule ambako fursa za kiuchumi ni kubwa na utayari wa wananchi kuchapa kazi ni kubwa pia.

Mheshimiwa Naibu Spika, Sekta isiyo rasmi ni kubwa sana na ina mchango mkubwa katika kuondoa umasikini, kuongeza ajira na kuchangia pato la Taifa. Kwa hiyo, MKURABITA upanuliwe na uenee nchi nzima kwa haraka zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, TASAF, naipongeza Serikali sana kwa mpango huu wa ruzuku kwa kaya masikini. Mpango umeonesha matokeo mazuri sana. TASAF ipo sasa awamu ya tatu na inatekeleza mpango wa kunusuru kaya masikini kuanzia mwaka 2013. Kumekuwa na mafanikio makubwa kwa kaya zilizoandikishwa na kupata ruzuku. Maisha yao yameboreshwa na wanashiriki vizuri katika shughuli za kiuchumi kuweza kuongeza kipato zaidi katika sekta mbalimbali.

Mheshimiwa Naibu Spika, natambua mpango huu haukuwafikia masikini katika vijiji na mitaa yote na pia katika vijiji ambavyo vimefikiwa, kuna kaya nyingine masikini hazikuridhishwa kwa sababu mbalimbali. Kwa mfano Wilaya ya Ileje, kati ya vijiji 71 ni 50 tu zilizofikiwa. Vijiji 21 bado havijafikiwa. Sasa ni lini hizi kaya masikini zitaingizwa kwenye mpango? Ninapata maswali mengi kutoka Jimboni kwangu kwa wapiga kura wangu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu ya uendelevu wa mpango huu: Je, kuna mikakati ipi ya ufadhili wa mpango huo? Kwa sababu sehemu kubwa ya fedha zinazotumika ni michango ya wadau wa maendeleo na Serikali inachangia kidogo, tunaona hata katika bajeti Serikali inatoa kidogo na sehemu kubwa ni fedha ya nje. Je, ikikosekana?

Mheshimiwa Naibu Spika, watumishi wa Umma wengi bado wanafanya kazi kwa mazoea. Wengi hawabebi haya maono ya Mheshimiwa Rais na wala hawaendani nayo. Hii inazorotesha watendaji, inapunguza tija na huzidisha gharama. Iko haja kuhakikisha kuwa Chuo cha Utumishi kinajikita zaidi katika mafunzo yaliyokuwa yakitolewa kwa watumishi wa kada ya kata ili kuwajengea uwezo wa jinsi ya kutekeleza majukumu yao Serikalini, kuwa na weledi wa masuala mbalimbali ya utumishi wa Umma. Hii itasaidia katika kuboresha ufanisi wa watumishi wa Umma.

Mheshimiwa Naibu Spika, huko nyuma Chuo cha Mzumbe kilitumika kutoa mafunzo yaliyojenga uwezo wa Watendaji Wakuu wa Taasisi za Umma, lakini walipoamua kukigeuza kuwa chuo cha kawaida na kupoteza fursa ya kuwajengea uwezo viongozi wa Mashirika ya Umma. Kwa sababu hiyo, ninapendekeza ufanywe utaratibu wa kutumia Chuo cha Uongozi (institute) kutoa mafunzo ya Watendaji Waandamizi kabla ya kupangiwa taasisi za Umma kuziongoza. Hii itasaidia kuongeza ufanisi wao na kuboresha huduma za wateja wao na kuvutia uwekezaji, uzalishaji kwa jumla na kuongeza mapato ya Serikali na kukuza uchumi kwa jumla.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukuzaji wa taaluma, kukidhi ubora unaotakiwa, kuongoza taasisi zetu, uzingatiwe na hii iendane na suala zima la uteuzi wa watumishi wenye vigezo na watakaopewa viashria vya kutumika kuwapima. Vetting ya wateule wa taasisi inachukua muda mrefu na kusababisha kuzorota kwa kazi za Serikali na Mashirika yake.

Mheshimiwa Naibu Spika, rushwa imepungua na kama inafanywa, kwa kiasi kikubwa watu wanajificha, lakini bado zile taasisi zilizoendeleza rushwa kama Polisi, Mahakama, Mamlaka ya Kodi, Hospitali na ambako rushwa bado inafanywa bila kificho. Ili kupunguza rushwa kubwa, tunaishauri Serikali ipunguze kutoka shilingi bilioni moja ili iwezeshe watu wengi zaidi wanaojihusisha na rushwa kupelekwa kwenye Mahakama ya Ufisadi na kupunguza vitendo vya rushwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, watendaji waliokuwa wanafaidika na mfumo uliokuwa unatoa mwanya wa rushwa wameamua kufanya kazi kwa kukomoa na kula rushwa kwa kisingizio cha Hapa Kazi Tu na hawa wamekuwa wakiharibu jina la Serikali na kuwapaka matope viongozi wetu. Iko haja ya kutupia jicho eneo hili kama TRA, Taasisi na Idara za huduma muhimu za Serikali zinazotoa vibali, leseni na kadhalika. Serikali ijitahidi kueneza mifumo ya TEHAMA ili kupunguza mawasiliano ya watu na watendaji hawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, hotuba ya Mheshimiwa Waziri haijazungumzia lolote juu ya Watanzania walio ughaibuni kama sehemu yenye fursa ya utumishi wa Umma. Kwa bahati mbaya Watanzania wengi wamekuwa na mtazamo hasi dhidi ya Watanzania walioko ughaibuni, lakini mimi ninaamini kuwa tukiwa na utaratibu mzuri wa kuwatumia ni hazina kubwa kwa Taifa letu na wengi wanapenda kurudi kufanya kazi Tanzania wakipewa nafasi. Nchi nyingi hata za jirani wamewatumia sana raia wao walio ughaibuni na kunufaika na weledi na ujuzi wao. Wakati umefika kubadilisha mtazamo wetu juu ya wenzetu walioko kwenye Diaspora ili wachangie maendeleo ya Taifa letu.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.