Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

Hon. Daimu Iddi Mpakate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduru Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

MHE. DAIMU I. MPAKATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuchangia jioni ya leo. Kwanza namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa uwezo wa kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu. Nitaenda moja kwa moja kwenye hoja ya msingi. Kwanza napenda kuunga mkono kwa asilimia mia moja hoja zote mbili na nitaanzia kwenye TAMISEMI kwa upande wa vituo vya afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishukuru Serikali yetu kwa kutupatia Jimbo letu la Tunduru Kusini vituo viwili vya afya ambavyo vimejengwa pale Mchoteka na kingine kimejengwa Rukasale. Nasikitika kwa kile kituo cha kwanza cha Rukasale kama Mheshimiwa Waziri alikuwa hana taarifa, bado hakijakamilika mpaka leo kutokana na matumizi mabaya ya fedha yaliyotokana na usimamizi mbovu wa Watendaji wetu. Hii imetokana na kwamba Halmashauri ya Tunduru haina mhandisi ambaye angeweza kusimamia vizuri katika ujenzi wa zile zahanati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na shukurani hizo, Jimbo la Tunduru Kusini lina Kata 15 na katika Kata 15 tuna vituo vya afya vitatu tu na tuna ahadi ya muda mrefu ya Kituo cha Afya Narasi iliyotokana na Rais wa Awamu ya Nne ambaye aliahidi kujenga kituo cha afya katika eneo lile. Nimeleta swali hili mara tatu katika Bunge lako Tukufu, nimeahidiwa kupewa pesa lakini hadi leo kile kituo bado hakijajengwa na watu zaidi ya 30,000 wako katika Kata zile mbili ambazo zinakitegemea sana na wapo mbali zaidi ya kilometa 70 kutoka Mjini Tunduru.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo napenda kuchangia katika hilo hilo, kulikuwa na ahadi vile vile ya Rais wa Awamu ya Nne ya kutoa gari kwa ajili ya Kituo cha Afya Mchoteka. Jambo hili bado nalo ni tatizo na Halmashauri yetu ina gari chakavu, ukizingatia kwamba Hamashauri ya Wilaya ya Tunduru ina eneo kubwa sana kuliko hata Mkoa wa Mtwara kwa ujumla wake. Kwa hiyo, tuna gari bovu la miaka ya 1980 mpaka leo hii, hatuna gari yoyote ambayo inaweza kusaidia wagonjwa wetu kutoka katika sehemu moja kwenda sehemu ya pili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ambalo napenda kuzungumzia ni suala la elimu. Katika suala la elimu tuishukuru Serikali kwa kutoa elimu ya msingi bila malipo, lakini kuna changamoto kubwa ambayo imejitokeza katika maeneo yetu hasa katika Jimbo la Tunduru Kusini kwamba watoto wamekuwa wengi, madarasa yamekuwa kidogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii imesababisha watoto wengi kusoma katika darasa moja zaidi ya 100 mpaka 200. Nikichukua mfano katika Shule ya Msingi Tuwe Macho ina zaidi ya watoto 800; Shule ya Msingi Semeni ina zaidi ya watoto 900; Shule ya Msingi Mtina ina watoto zaidi ya 1,000, lakini madarasa yaliyokuwepo hayazidi saba au matano. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunaomba katika miundombinu ya shule za msingi iongezwe bajeti ili kuhakikisha kwamba majengo yanajengwa ili watoto wale waweze kusoma katika mazingira mazuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo napenda kulizungumzia ni suala la watumishi. Kwa kweli tatizo la watumishi limekuwa ni kubwa sana katika Halmashauri ya Wilaya ya Tunduru. Tuna upungufu wa wafanyakazi katika Sekta ya Afya zaidi ya asilimia 65. Katika Sekta ya Elimu zaidi ya asilimia 50.

Mheshimiwa Mwenyekiti, shule nyingi za msingi katika jimbo langu zina walimu ambao hawazidi watano na minimum ni watatu; na shule hizo ziko kuanzia darasa la kwanza mpaka darasa la saba. Kwa kweli kwa walimu wale imekuwa ni mzigo mkubwa sana kufundisha madarasa saba wakiwa walimu watatu, wanne au watano. Naomba sana kwa kuwa tuko ndani ya bajeti tunaomba sana watumishi wa Sekta ya Elimu waongezwe ili kuhakikisha kwamba wanaweza kufanya kazi vizuri kwa ajili ya watoto wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, kuna tatizo la walimu waliostaafu katika kipindi hiki ambacho kikokotoo kipya kimetengenezwa. Walilipwa kwa hesabu ile ya kikokotoo cha zamani. Wamekuja ofisini kwangu mara mbili mpaka mara tatu, wanasema itakuwaje? Tumelipwa kwa kupunjwa na Rais amesema kikokotoo kitumike kile cha zamani. Walimu hawa wanaulizia watapewa lini mapunjo yao ili waweze kujikimu katika maisha yao ya kustaafu kama ilivyo sasa? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo napenda kuzungumzia ni suala la Makatibu Tarafa. Naishukuru Serikali katika Jimbo kangu la Tunduru Kusini kuna Tarafa tatu, mwaka 2018 tumepata watumishi wote, Maafisa Tarafa watatu. Changamoto waliyokuwanayo, hawana ofisi kabisa. Ofisi za Maafisa Tarafa hakuna kwenye Tarafa zetu. Halmashauri yote ina ofisi moja tu katika Tarafa saba. Kwa hiyo, hawana ofisi, hawana nyumba za kuishi, tunabanana nao humo humo kwenye maeneo yetu ambayo tunaishi. Tunaomba sana, mtengeneze angalau bajeti kwa kuwajali hao Maafisa Tarafa ili waweze kupata Ofisi na nyumba za kuishi waweze kufanya kazi vizuri zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la tano ambalo napenda nizungumzie ni suala la TARURA. Kwa kweli TARURA pamoja na kazi nzuri wanayoifanya, tatizo fedha inakuwa ni kidogo. Kwenye upande wa Jimbo langu la Tunduru Kusini, kuna barabara zina zaidi ya miaka 10 hazijawahi kutengenezwa. Tulitegemea TARURA atakuwa ni mkombozi katika kutengenezea barabara zile.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna barabara ya Lukumbule – Imani – Kazamoyo, kuna barabara ya Mlingoti – Tuwemacho – Ligoma, kuna barabara ya Chemchemi – Namasakata – Liwanga mpaka Msechela, kuna barabara ya Namasakata – Amani – Msechela, kuna barabara ya Nandembo – Mpanji mpaka Njenga, kuna barabara ya Mchoteka – Masuguru – Malumba. Barabara hizi zina zaidi ya miaka saba hazijafanyiwa kazi yoyote. TARURA kwa kweli kila unapoona hesabu yao, ukiangalia kwa sasa wamepewa 1.3 billion na hizi barabara zina zaidi ya kilometa 455. Kwa hela ile waliyopewa kwa matengenezo ya kawaida tu kwa kweli haitaweza kukidhi haja ya kutengeneza barabara hizi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba sana TARURA waongezewe pesa ili waweze kufanyia matengenezo barabara zetu ambazo zinatumika kwa ajili ya maendeleo ya wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho ambalo napenda kulizungumza ni suala la mapato ya Halmashauri zetu. Hapa kuna shida, hasa kwenye mikoa ya kusini; mwaka jana na mwaka juzi tulikuwa tunaenda vizuri, mapato yetu mengi tunapata kutokana na ushuru wa korosho. Bahati mbaya mwaka huu biashara ilivyokwenda, hatukuweza kupata ushuru wa korosho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Serikali, kwa kutambua kwamba walikuwa na mipango na bajeti zao kwa ajili ya kutekeleza miradi mbalimbali ambayo ilikuwepo kwenye mahesabu, basi Serikali ifanye huruma kuwasaidia angalau ruzuku Halmashauri zile ziweze kukidhi haja ya kuweza kutekeleza ile miradi ambayo ilikuwa imepangwa mwaka 2018/2019. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Mbunge.

MHE. DAIMU I. MPAKATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)