Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

Hon. Joseph Leonard Haule

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Mikumi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

MHE. JOSEPH L. HAULE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili nami niweze kuchangia kwenye bajeti ya Wizara hizi mbili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote, nijielekeze kusoma Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Ibara ya 13(1) inasema: “Watu wote ni sawa mbele ya sheria, na wanayo haki, bila ya ubaguzi wowote, kulindwa na kupata haki sawa mbele ya sheria”. Vilevile Ibara ya 14, inasema: “Kila mtu anayo Haki ya Kuishi na kupata kutoka katika jamii hifadhi ya maisha yake, kwa mujibu wa sheria” (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, najielekeza kwenye Wizara ya Utawala Bora. Wiki iliyopita nilisimama katika Bunge lako Tukufu nikizungumzia kwamba kuna upotevu wa watu kumi katika Jimbo la Mikumi maeneo ya Ruhembe, Kidodi pamoja na Ruaha na niliongea hapa kwenye Bunge nikiamini kwamba Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imo humu ndani. Pamoja na kuongea hapa Bungeni na kumfuata Waziri wa Maliasili na Utalii na kuwafuata wahusika wote mpaka leo watu wamenyamaza kimya kana kwamba hakuna kilichotokea katika Hifadhi za Mikumi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nimekuwa nikijiuliza, Serikali hii inajipambanua kwamba inajali utu, haki lakini pia utawala bora, pamoja na hayo kila siku tunaimba kwamba Tanzania ina amani lakini ni jambo la kushangaza sana unapoona kwamba kuna watu kumi na tunaripoti kwenye Serikali wamepotea katika mazingira ya kutatanisha tangu tarehe 2 Aprili, leo ni tarehe 12, siku kumi hakuna mtu yeyote amezungumzia lolote katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hali hii imetusikitisha sana na bado majonzi yamekuwa makubwa sana katika Jimbo la Mikumi maeneo Ruhembe na niseme kitu kimoja kwamba hali hii inaendelea kuleta taharuki na imani ya wananchi kwa Serikali imekuwa ndogo na inazidi kushuka kila siku. Kwa kuwa tunajua kwamba TANAPA na Polisi wana helikopta au helikopta hizo zinakuwa kwa ajili ya intelijensia kuwakamata wapinzani tu na kushindwa kuelewa Watanzania wengine wasiokuwa na hatia wanaopotea katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, siku kumi ni nyingi watu wanapokuwa hawaonekani. Tukasema labda tupeleke kwa Serikali itatafuta namna ya kutupa majibu ya jambo kama hilo, inasikitisha sana kuona mpaka leo siku ya kumi watu wamekuwa na majonzi. Basi hatuombei labda wamekufa tuseme lakini hatuombei hivyo, kama wamekufa basi mtupe hata nguo zao ili tukazizike au tukaendelee na misiba katika Jimbo la Mikumi, labda huo ndiyo utawala bora mnaoujua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, maana imeundwa Kamati imekwenda kule, RCO pamoja na watu wa hifadhi, you can’t be a judge of your own case, huwezi kuwapeleka watu ambao tunahisi na wananchi wanalia kwamba watu wamepotea katika hifadhi yao, halafu bado wao wao ndiyo wakaenda kuangalia na kufanya uchunguzi mpaka leo hakuna majibu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili jambo tunaomba mliangalie kwa kina na tupate majibu ya Serikali hawa watu kama wamekufa tujue, kama wamepotea tujue, tunatakiwa tujue ripoti yao. Nina nia ya kuomba Bunge lako Tukufu liunde Tume ambayo itakwenda kufanya uchunguzi katika maeneo hayo ya Ruhembe ili tuweze kuwapa haki hawa wananchi ambao ndugu zao wamepotea katika hifadhi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo nataka kuzungumzia ni kuhusu Tume ya Uchaguzi. Kila siku tumekuwa tukizungumza Tanzania ni kisiwa cha amani lakini naona watu wana nia ya kupoteza kisiwa cha amani cha Tanzania. Labda niwashauri tu Wabunge wa CCM ambao mnashabikia sana kuhusu hii Tume ya Uchaguzi, muangalie sasa hivi katika TV za kimataifa, CNN, Al-Jazeera na sehemu nyingine, jinsi ambavyo kumekuwa na unrest katika dunia kwa sababu ya mambo kama haya. Watu wamefungwa mikono, watu wanashindwa kusema lakini Tume imekuwa haitendi haki kwa wapinzani wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jana Sudan mmeona kimemtokea nini Al-Bashir lakini ukiangalia Algeria na Venezuela kuna vitu kama hivyo na hapa Tanzania kama tutaendelea kucheka na hii Tume ya Uchaguzi ambayo sasa matokeo yamekuwa yakitangazwa vice versa, leo tu Mahakama ya Mbeya imetoa hukumu kwamba katika Kata ya Ndalambo ambapo alitangazwa mgombea wa CCM lakini wameona ni jinsi gani ambavyo Serikali ya CCM imekuwa ikiiba kura kila siku na sasa hivi wameonekana wameiba na mgombea wa CHADEMA ametangazwa kushinda pale. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini watu wanasema Tume hii ni huru kwa sababu akina Profesa Jay walitangazwa; hamjui mbilinge tulizozifanya huko mpaka tukatangazwa. Tumefanya uchaguzi tarehe 25, tarehe 26 unaona magari yanakuja yanaondoka, tarehe 27 CCM wanabeba magari ya matangazo wanataka kujitangaza kwa nguvu, nyomi linaongezeka pale na pale kweli asingetoka mtu. Napenda kusema kwa Wanamikumi kwamba nitaendelea kusimama pamoja nanyi na niombe watu wote wapenda amani hapa Tanzania wasimame pamoja kuhakikisha kwamba Tume hii inabadilishwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ni mwanamuziki wa hip hop lakini pia napiga ngumi mbili, tatu, napenda boxing; kama wewe ni referee kama Tume ya Uchaguzi, basi usinifunge mikono mimi halafu ukamuacha jamaa anipige mangumi mengi mengi usoni, unanifunga kamba halafu unamwambia jamaa apige, haiwezekani. Ipo siku hizi kamba zitakatika na nitawapiga manondo ya kutosha ndugu zangu kwa sababu tunakwenda kushinda na tunaamini tutakwenda kufanya hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwaombe tu watu wote ambao wamepitia katika nyanja na matatizo mbalimbali waamini kwamba haya mambo ni ya kupita tu. Watu wangu wa upinzani tulizeni ball, mwaka huu ni wa uchaguzi tunakwenda oya oya na mzuka kama kawaida maeneo ya katikati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, niende kwenye Wizara ya TAMISEMI kwa Mheshimiwa Jafo. Nashukuru sana ulifanya ziara Jimboni Mikumi lakini kiukweli kabisa ni kwamba katika Kituo cha Afya cha Mikumi baada ya ziara yako ndiyo mambo kidogo yameanza kwenda vizuri na mimi kama Mbunge nimechangia mifuko 200 kuonesha kwamba nina-support kile kinachotokea kwa ajili ya Kituo cha Afya cha Mikumi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, bahati mbaya ni kwamba wale wafanyakazi waliopewa kazi za ziada bado hawajalipwa mpaka leo na wameniagiza nikwambie kwamba wameshaleta barua kwako wanasubiri uwasaidie. Wale ni walalahoi wa Mikumi wamefanya kazi pale wanataka uwasaidie wapate haki yao ya msingi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia wananchi wa Malolo wanajenga Kituo cha Afya kwa nguvu zao wenyewe na mimi kama Mbunge nimepeleka tena mifuko 200 ku- support juhudi hizo. Tunaomba Serikai nayo ituongezee hela kidogo ili tuweze kukamilisha nia yao ya kuweza kuwa na kituo chao cha afya kama ambavyo sera inasema kila kata iwe na kituo cha afya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kituo cha Afya cha Ulaya, nilishaongea muda mrefu kimechakaa, tunaomba Serikali ipeleke pesa kule. Pia Waziri wa Nishati alishafanya ziara pale, aliona kwamba hakuna umeme na alisema atatuletea umeme, watu wanasubiri maeneo ya Mikumi, Ulaya pale tuweze kupata umeme.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nishukuru kwamba tuliomba magari, kwa sababu Mikumi pale kuna ajali nyingi sana Mitaa ya Msimba, Ng’apa mpaka Ruaha Mbuyuni lakini sasa hivi kinajengwa pale kituo cha dharura kwa ajili ya ajali na kwamba tutaletewa magari mawili kama ambavyo Mbunge niliomba. Kwa sababu tumegundua kwamba pale Mikumi kuna matatizo mengi ya ajali mbugani na sehemu nyingine na tukasema kwamba tukipata magari ya wagonjwa yatasaidia kukimbiza wale watu wanaopewa rufaa. Maana kutoka Mikumi mpaka Kilosa ni kilometa 78; Mikumi mpaka Morogoro kwenye Hospitali ya Rufaa ya Mkoa ni kilometa 120; Mikumi mpaka Iringa ni zaidi ya kilometa 200.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe shukrani kwamba tumeambiwa haya magari yapo, Wanamikumi wanayasubiri kwa nguvu na kwa hamu kubwa ili tuweze kuwasaidia Watanzania. Maana Mikumi pale inapita barabara kubwa inayotoka Tanzania kwenda Zambia mpaka South Africa, tunaamini hata watu wa Nyanda za Juu wanaopata ajali maeneo yale watapata nafuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye TARURA. Kwa kweli TARURA bajeti yao ni ndogo na ndiyo maana mwaka jana nilipiga kelele hapa nikisema Wilaya ya Kilosa ni kubwa lakini imekuwa na bajeti ndogo sana, TARURA hawana hata gari. Nashukuru tumeletewa gari lakini bado TARURA uwezo wake ni mdogo. Kuna barabara kutoka Ruaha Mbuyuni - Malolo - Kibakwe; kuna barabara ya kutoka Dumila - Kilosa - Mikumi lakini pia kuna barabara nyingine ya kutoka Ulaya – Madizini - Malolo, hizo zote ziko chini ya TARURA, tunaamini inaweza kutusaidia. Hii barabara ya Dumila – Kilosa iko chini ya TANROADS, naamini nao watatusikia waweze kutusaidia kwa sababu ni barabara muhimu sana kwetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilitaka kuongelea kuhusu upungufu wa watumishi na kwa Wizara ya Elimu katika Wilaya yetu ya Kilosa tumekuwa na upungufu mkubwa sana wa walimu. Mfano shule ya msingi ina wanafunzi wa awali wa darasa la kwanza hadi la saba 107,000 lakini walimu wako 2,393 tu na tuna upungufu wa walimu 929. Pia tuna maboma 39 tunaomba Serikali itusaidie; sekondari tuna madarasa pungufu 129, majengo ya utawala 28, nyumba za walimu 689 lakini pia tuna upungufu wa hostels 27. Wananchi wamefanya juhudi kubwa sana ya kujenga maboma tunaamini Serikali itatusaidia ili tuweze kuboresha elimu katika Wilaya yetu ya Kilosa ambayo ni wilaya kongwe sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa niseme kwamba tuko pamoja na Kambi Rasmi ya Upinzani na nimheshimu sana Mheshimiwa Japhary Michael ambaye amewasilisha hotuba ya Msemaji wa Kambi Rasmi ya Upinzani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)