Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

Hon. Dr. Shukuru Jumanne Kawambwa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bagamoyo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

MHE. SHUKURU J. KAWAMBWA: Mheshimiwa Mwenyekjiti, nashukuru kwa kunipa nafasi hii ya kuchangia hoja ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Utumishi na Utawala Bora. Nitangulize kwa kuwapongeza Waheshimiwa Mawaziri hawa kwa kazi nzuri ambayo wanaendelea kuifanya ya kumsaidia Mheshimiwa Rais pamoja na kulitumikia Taifa hili kwa juhudi kubwa na kwa nidhamu kubwa. Naomba pia niwapongeze Manaibu Waziri, Mheshimiwa Mwita Waitara, Mheshimiwa Kandege na Mheshimiwa Dkt. Mary Mwanjelwa kwa kazi nzuri wanayoendelea kuifanya kuwasaidia Mawaziri na kumsaidia Rais katika kulitumikia Taifa hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na sekta ya afya; naomba kuchukua fursa hii kuishukuru sana Serikali ya Awamu ya Tano na kuwashukuru sana Mawaziri kwa kutuwezesha sisi Jimbo la Bagamoyo kuweza kupata vituo viwili vya afya. Vituo hivi viwili vya afya kimoja kimejengwa Kata ya Kerege, kingine kimejengwa katika Kata ya Yombo. Vituo hivi vitachangia sana kutoa huduma nzuri ya afya kwa wananchi wetu akinababa na akinamama na watoto katika kata hizi na kwa maana hiyo pia kupunguza mzigo mkubwa ambao ulikuwepo katika hospitali ya Wilaya ya Bagamoyo ambayo ilikuwa inazidiwa kiasi cha kwamba inashindwa kutoa huduma nzuri. Tulitengewa pesa nyingi jumla ya shilingi milioni 910 kwa ajili ya ujenzi wa vituo hivi vya afya, lakini pia tumetengewa pesa jumla ya shilingi milioni 400 kwa ajili ya vifaa tiba kwa vituo hivi viwili. Nashukuru sana kwa kazi hii nzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu kwamba, hili jambo ni kubwa sana. Tunapozungumzia kuunganisha au kujumuisha ukuaji wa uchumi na maendeleo ya wananchi hapa ndipo ambapo kwa kweli mwananchi anaweza akaona ukuaji wa uchumi wa nchi yake na hili ndiyo jambo kubwa la kumfanyia mwananchi wa Tanzania. Mwananchi mfanyie mambo mawili; mpe elimu na mpe afya bora. Hivi vitu viwili ndivyo vinatengeneza rasilimali kuu ya nchi yetu ambayo ni mwananchi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Hakuna rasilimali zaidi ya rasilimali watu katika hii nchi yetu. Kwa hiyo niishukuru sana Serikali kwa jambo hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kituo kile cha afya katika Kata ya Kerege kimeshaanza kazi na kituo cha afya katika Kata ya Yombo kinatarajiwa kuanza kazi baada ya muda mfupi. Nimwombe Mheshimiwa Waziri, katika Kata yetu ya Kerege ambapo kituo kimeanza kazi, lakini bado kina upungufu. Upungufu ni katika theatre haijakamilika na vifaa tiba bado havijakamilika, kwa maana hiyo hata upasuaji bado inabidi tuendelee kuufanya kule katika hospitali ya Wilaya ya Bagamoyo. Hivyo, tunaomba tusaidiwe ili upungufu huu uweze kuondoka, tuwe na jengo la OPD, theatre ikamilike ili wananchi wetu waweze kupata huduma ile ambayo inatarajiwa katika Kituo cha Afya cha Kerege.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kituo cha Afya cha Yombo chenyewe bado hakijakamilika kwa maana kinahitaji sasa samani na vifaa tiba ili kituo hiki kiweze kufanya kazi, lakini pia hakijapangiwa watumishi bado. Kwa hivyo, tumefanya kazi nzuri ya kujenga vituo hivi na nina imani kwamba, kwa kazi nzuri ambayo tumeifanya na mwaka jana tulitangazwa kuwa ni Jimbo namna moja kwa ubora wa kituo cha afya tulichokijenga katika awamu ile. Kwa hiyo Mheshimiwa Waziri atuunge mkono ili tukamilishe na hiki Kituo cha Afya cha Yombo ili nacho kiweze kuanza kufanyakazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maboresho haya yanapelekea wivu pia kwa sababu afya ni jambo muhimu sana. Katika Jimbo langu la Bagamoyo, barabara hii inayotoka Bagamoyo kwenda Msata njia nzima hii kuna zaidi ya vijiji 20, Kijiji cha Makurunge, Kidomole, Fukayosi, Mwavi, Mkenge, Kiwangwa na vijiji kadhaa ndani ya Jimbo la Chalinze vyote hivi havina huduma yoyote inayofanana na kituo cha afya. Kwa hivyo, Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI kwa heshima na taadhima niombe katika bajeti hii inayokuja angalau tupate kituo kimoja cha afya katika barabara hii ya Bagamoyo kwenda Msata ambacho kiweze kuhudumia wananchi wengi katika vijiji vingi katika eneo hili, pamoja na wasafiri kama ambavyo nakumbushwa. Barabara hii imeshaanza kuwa maarufu sana na inatumika na wananchi wengi wa Kanda ya Kaskazini. Kwa hiyo, ni muhimu sana tuwe na huduma nzuri ya afya katika eneo hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichangie kuhusu TARURA; Waheshimiwa Wabunge wamezungumza sana na hili jambo ni nyeti, ni muhimu sana Serikali ikaliangalia kwa mapana yake. Katika Halmashauri ya Wilaya ya Bagamoyo, barabara za TARURA zina jumla ya kilomita 332 lakini ziko katika hali ngumu sana. Mwaka huu wa fedha hakuna pesa kabisa ambayo imetengwa kwa ajili ya miradi ya maendeleo ya barabara za vijijini kwa maana hiyo hatuwezi kufungua barabara, hatuwezi kuzitengeneza barabara katika hali nzuri zaidi. Kipindi kama hili cha mvua barabara zimefungwa kabisa, vijiji vimefungwa, huduma za jamii kama shule, afya na kadhalika zinakuwa mtihani kupatikana. Tumetoka safari ndefu sana ya miaka mingi iliyopita wakati Wilaya zilikuwa hazijaunganishwa kwa barabara za lami, mikoa haijaunganishwa na barabara za lami, lakini hivi sasa kwa kazi kubwa ambayo zimefanywa na Serikali zilizopita na Serikali ya Awamu ya Tano mikoa yote inafikika kwa barabara za lami na karibu Wilaya zote zinafikika pia. Sasa mkazo tuupeleke kwenye barabara za vijijini huku ambako wananchi wanaishi na huku ambapo wananchi wanafanya kazi nyingi sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningeshauri Serikali yetu iangalie uwezekano hata wa kubadilisha mgao ule katika Mfuko wa Barabara ambao traditionally tulikuwa tunapeleka asilimia 70 ya TANROADS, asilimia 30 katika Halmashauri na kwa sasa TARURA ili angalau tuifanye 50 kwa 50 ili tuweze kufanyakazi nzuri zaidi ya barabara katika vijiji vyetu. Huko tutakuwa tumemkomboa mwananchi aweze kuzalisha mazao na kufanya kazi zingine zitakazotuletea maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie eneo la mpango wa kunusuru kaya maskini chini ya TASAF. Mpango huu ni mkombozi sana kwa kaya maskini, ni mpango ambao unaleta tabasamu kwa kaya maskini, yaani hakuna jambo ambalo limenifurahisha katika Jimbo langu kama pale kukutana na mwananchi wa kaya maskini naye anatabasamu…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa kwa mchango wako.

MHE. SHUKURU J. KAWAMBWA: Mheshimiwa Mwenyekjiti, naunga mkono hoja. (Makofi)