Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017- Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji

Hon. Mwita Mwikwabe Waitara

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tarime Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017- Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji

eze hotuba nzuri ya Msemaji wa Kambi ya Upinzani kwenye idara hii ya viwanda. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nishukuru kwa kupata nafasi hii nichangie. Nikupongeze sana wewe binafsi, kulikuwa na maneno sana, sasa najaribu kulinganisha maneno yale juu yako na uongozi wako, wewe ni Mwenyekiti smart kweli kweli, hongera sana Mheshimiwa. Nitakuomba kwa umri wako na uzoefu umsaidia Naibu Spika asiharibu hili Bunge, kwa kweli nasema haya ni muhimu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana Mheshimiwa maana msema ukweli ni mpenzi wa Mungu kama unafanya vizuri tukupongeze, ukifanya vibaya tunakusema lakini sitarajii kwamba wewe utafanya vibaya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ni Wizara ya Viwanda na Biashara na nina hoja hapa ambazo ningeomba Mheshimiwa Waziri mhusika asikilize. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Waziri kwamba hoja za msingi sehemu kubwa ya hoja hizo zinatoka Upinzani naomba utusikilize vizuri, yale mambo mengine wayapuuze. Kwa sababu kwa mfano mtu akikusikiliza vizuri Mheshimiwa Waziri na akatafakari na mimi nimekusikiliza hapa mara kadhaa nikaenda nikakaa, nikarudi hapa nikaona maneno yako yale kama utaweza kuyatekeleza utakuwa ni Waziri wa kwanza ndani ya CCM kufanya kazi kubwa sana na mimi nakutakia kila la kheri. Siyo kwa sababu ni mtani wangu umekula senene hapana, lakini unavyozungumza nitaomba hayo mazungumzo ya-reflect actions pamoja kwamba kuna kazi kubwa sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Mheshimiwa Waziri atusaidie, CBE ipo chini ya Wizara yake na Mheshimiwa Waziri wa Elimu asikilize hapa. Nimepata taarifa kwamba CBE pale kuna majipu, ninazo document hapa ambazo Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana anazo, Mheshimiwa Katibu Mkuu wa Wizara hiyo anazo tena ni Profesa, Mheshimiwa Mwenyekiti wa Bodi ambaye ni Profesa wangu wakati nikiwa Chuo Kikuu Dar es Salaam nikiwa Rais wa Chuo kile alikuwa anaendesha Baraza la Chuo nikiwepo, Mheshimiwa Profesa Luhanga na wadau wengine. Wameleta malalamiko wanadai kwamba katika kile chuo, Mkuu wa Chuo pamoja na Mkurugenzi wa Fedha, chini ya Idara yako na hii sasa inaweza ikapunguza maneno yako haya nikatafsiri tofauti, kwamba kuna Mkurugenzi wa Fedha amekusanya zaidi ya shilingi milioni 400 bila kutoa stakabadhi anatoa risiti za karatasi zile baadaye hazionekani, vielelezo hivi hapa vipo, hii ni Idara yako na ulipopata taarifa hapa, wale watu ambao wameleta document hapa wakapigiwa simu wanatishiwa kwa nini wameleta taarifa kwako. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini hizi tuhuma Katibu Mkuu alipoandikiwa, yaani shilingi milioni 400 zimekusanywa, CBE pale kuna campus nne, nazungumzia Dar es Salaam wamekusanya fedha zaidi shilingi milioni 400 kwa utaratibu ambao kimsingi ni kinyume na utaratibu. Wanasema kuna wanafunzi ambao hawalipi ada wakiongea na Mkurugenzi wa Fedha wanamkatia kidogo anaenda anafuta zile kumbukumbu, wale wataalam wa fedha wanasema bad debtors kwa maana ya kupoteza ushahidi, pia haya ni malalamiko ambayo yapo kule. Kwa maelezo yao inaonesha kwamba Mkuu wa Chuo anaelekeza alama 50 ziongezwe kwa wanafunzi ambao wamefeli ambao yeye ana maslahi nao. Hii inaingia kwenye standard ya elimu na hivi vyuo vimekuwa na malalamiko muda mrefu kwamba wanafanya kazi pale kuonesha urembo CBE almost zote wanashiriki sana haya mambo yako.
Kwa hiyo, ina maana hapa inahusu vilevile na Waziri wa Elimu atambue kwamba ni suala la Wizara ya Biashara lakini pia kuna jambo hilo linazungumzwa. Kuna Mkaguzi wa Nje alipelekwa pale alikuwa hired na chuo, akaahidiwa kupewa shilingi milioni 13 akakubali kufanya forgery kwenye ukaguzi wake, aka-abuse profession lakini badaye akapewa shilingi milioni 3.5 sasa hivi analalamika mtaani kwamba amedhulumiwa, huyu naye ni jipu. Nilipoleta malalamiko kwamba kile chuo kichunguzwe, Mkuu wa Chuo kwa kuzungumza na Mkurugenzi wake wakazunguka hilo zoezi halijafanyika kufanya ukaguzi wa fedha. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, CBE ya Mwanza na yenyewe ina malalamiko, kuna mtu pale anaitwa Rose yupo Gerezani Segerea tangu mwaka 2011 lakini kapandishwa mshahara analipwa mshahara. Sasa unatafuta wafanyakazi hewa kumbe wapo, document hizi zipo, Waziri anazo, Katibu Mkuu anayo, Bodi inajua na Mkuu wa Chuo anafahamu. Sasa haya mambo Mheshimiwa Mwijage yatapunguza kasi na maneno yako yanaweza yakatia wasiwasi katika mazungumzo. Vielelezo hapa vipo mpaka risiti, mpaka bank statement hizi hapa zimetolewa. Kwa hiyo, ni muhimu sana haya mambo unapopanga uyaangalie, haya makandokando tunaposema wala siyo kuzomea huu ni ukweli mambo yapo, yafanyieni kazi haya, nendeni mkapeleke special audit, CAG akague hivi vyuo alete taarifa, hilo ni la kwanza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, mimi ni Mbunge wa Jimbo la Ukonga. Kule Ukonga tunayo shida ya sehemu ya kupata vifaranga, vingi vinatoka nje ya Jimbo na vingine hata nje ya nchi. Wananchi wengi wanafuga kuku, akina mama, vijana wa bodaboda, wauza maandazi wamekopa VICOBA wanafanya biashara ile kwa maana ya kujikimu. Mtu analisha almost miezi miwili, mitatu kwa gharama kubwa vinakufa vyote na hakuna fidia. Unakuja kutafuta unaambiwa eti havikuchanjwa, nani alipaswa kuchanja, nani ana-control standard, bidhaa inatoka wapi, kiwanda kinalipaje, hayo mambo yote wananchi wangu wanapata shida sana. Kwa hiyo, nitaomba unapokuja hapa pia ni muhimu tukapata majibu hayo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile tunajua kwamba kulikuwa na mpango hapa unazungumzia habari ya biashara lakini Serikali hii ya chama changu cha zamani na mimi huwa nazungumza nawashangaa ambao wanapiga humu. Mimi nilikuwa kada wa hicho chama yalinishinda nikabwaga manyanga, lakini niko vizuri kweli kweli. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa namwambia Mheshimiwa Nape kama wakiruhusu kuongea pumba sisi tunaweza kutengeneza pumba tukaitumia vizuri kuliko mtu anayeokota pumba. Kwa hiyo, ni muhimu sana tukazungumza mambo serious. Kule kuna kitu kinaitwa DECI na MALINGUMU, fedha zinapandwa, Serikali ilisajili watu wakawa wanalipa kodi, wakafungua na ofisi, hili jambo na lenyewe mpaka leo wananchi wangu wamepata shida. Watu wa Dar es Salaam wamedhulumiwa fedha kesi imeenda Mahakamani inaendelea au haiendelei haijulikani. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri ulivyozungumzia wafanyabiashara wadogo wasaidie hawa watu, hii DECI na MALINGUMU uje na majibu nani alisajili na Mawaziri wastaafu walihusika na fedha zilikusanywa zikaenda Hazina mpaka leo hawajarudishiwa mitaji yao, hawajalipwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, haya mambo ndiyo maana tukasema viwanda vilikufa watu wakauziana, leo mnakiri wenyewe na mnajua kwamba viwanda vingi vimekuwa scraper. Sasa watu hawa watengenezee matumaini waone hali sasa ni nzuri, makandokando yameondoka, viwanda vikianzishwa vitaendelea kudumu, vitazalisha, watapata ajira, ni muhimu sana kujua hayo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nimeenda kwenye kiwanda cha Mbagala kule, kuna kiwanda pale Ukonga cha Nguo kinaitwa Namel, hivi viwanda mmepitisha mshahara wa wafanyakazi maskini wetu wale wanalipwa shilingi laki moja kwa mwezi, nataka utuambie hivi unavyoanzisha sasa na vyenyewe mshahara shilingi laki moja inasaidia kitu gani. Wanafanya overtime wanalipwa shilingi elfu mbili, hawana gumboot, hakuna usalama mle ndani, wanafanya kazi zaidi ya masaa ya kazi, mikataba hawapewi, kwa hiyo ina maana watu wanaonewa. Kwa hiyo, viwanda vinaweza vikaja mkafurahi kupata kodi, hii milolongo ambayo hamjarekibisha wananchi wakaendelea kuumia na hiyo ni shida tutaomba pia uoneshe kama kuna mazingira rafiki ambayo yametengenezwa ili watu wetu waweze kufanya kazi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, chakula cha kuku Dar es Salaam ni shida sana, bei ni kubwa, kilikuwa kinauzwa shilingi 36,000 kimepanda mpaka shilingi 60,000. Nimejaribu kuuliza wananiambia mahindi, pamba na alizeti zinapelekwa nje bila kuwa processed na wafanyabiashara wakubwa wanaificha kwa hiyo inavyorudi bei inakuwa ni kubwa sana, hatuwezi ku-control.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeuliza kwa mfano dawa zikoje, zile dawa za chanjo za kuku hata ng‟ombe nyingi hazina TBS, nendeni pale Ukonga mkague maduka yale hakuna TBS, hawalipii, kwa hiyo bei wanajipangia wenyewe. Kuna biashara holela na hili linaweza kuhatarisha maisha yetu kwa sababu tunakula mayai ya kuku hawa kumbe yako below standard tunapata magonjwa mengine ya kutisha. Kwa hiyo, Mheshimiwa naomba utusaidie pia katika hilo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine nataka unisaidie ni kuhusu mifuko ile ya kijamii. Kumekuwa na malalamiko hapa kwamba wafanyakazi wale michango yao haipelekwi kwenye mifuko hii ya jamii. Sasa lazima uweke mazingira rafiki kwamba hili nalo ikitokea unafanyaje…
MHE. MWITA M. WAITARA: Dah, ahsante sana, siungi mkono hoja, ila nawasilisha.