Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

Hon. Lolesia Jeremia Maselle Bukwimba

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Busanda

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

MHE. LOLESIA J. BUKWIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili nami niweze kuchangia bajeti muhimu kabisa ya Ofisi ya Rais, TAMISEMI pamoja na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Magufuli, kwa usimamizi mzuri ambao anaufanya kila wakati. Ameweza kusimamia, kwa kweli tunaona matokeo makubwa kwa kipindi kifupi tunaona mambo yanaendelea vizuri. Ni Serikali inaendelea kusimamia vizuri na kutekeleza sera kwa vitendo ambazo zipo katika nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nichukue nafasi hii pia kumpongeza Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI na Mheshimiwa Waziri wa Utawala Bora na Naibu Mawaziri wote, watumishi wote wa Wizara kwa kazi kubwa wanazozifanya. Wote tunafahamu TAMISEMI imebeba wananchi wa nchi hii ya Tanzania. Inashughulika na changamoto nyingi katika Taifa hili. Masuala ya elimu, afya, barabara na kwa kweli TAMISEMI ni kila kitu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee kabisa nikianza katika Sekta ya Afya, nitumie nafasi hii kuipongeza Serikali kwa kazi kubwa ya ujenzi wa vituo zaidi ya 352 Tanzania nzima. Kwa kweli ni kazi kubwa iliyotukuka. Napongeza kazi hii kubwa ambayo imeifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikiangalia pia katika mkoa wangu, hasa katika Halmashauri ya Wilaya yangu, nitumie fursa hii kuishukuru Serikali kutupatia shilingi bilioni 1.5 ambazo zimejenga Hospitali ya Halmashauri katika eneo la Nzela. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile nichukue nafasi hii kumshukuru Mheshimiwa Waziri kwa kutupatia shilingi milioni 400 kwa ajili ya kujenga Kituo cha Afya Nyarugusu. Natoa shukrani hizi kwa sababu kusema ukweli kikikamilika kituo hiki kitapunguza changamoto kubwa ambayo wananchi wa Nyarugusu walikuwa wakiipata. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa kunatokea mambo ya vifo pamoja na changamoto mbalimbali, lakini kwa kupewa hizi shilingi milioni 400, kwa kweli kwa niaba ya wananchi, wanashukuru sana kwa kazi kubwa na fedha nyingi ambazo mmetupatia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, katika Sekta ya Afya najua bado changamoto zipo. Kwa mfano hii hospitali ambayo tumepewa, inajengwa Nzela, lakini jiografia yetu katika Halmashauri ya Wilaya ya Geita kwa kweli changamoto ni kubwa sana. Haiwezekani mtu akatoka Jimbo la Busanda kwenda kutibiwa Nzela, ni mbali. Afadhali hata akatibiwe Geita Mjini. Kwa hiyo, tunaona jiografia yake ni ngumu, itawezesha wananchi watapata changamoto kubwa kabisa kwa ajili ya usafiri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri Mkuu alikuja mwaka 2018 akatuahidi kujenga hospitali Katoro. Nimeangalia kwenye bajeti sijaweza kuona. Kwa hiyo, nitumie fursa hii kumwomba Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI, Mheshimiwa Jafo, tuangalie, maadam Waziri Mkuu ametuahidi, alikuja Geita akatuahidi pale pale Katoro na wananchi wakafurahi wakiamini kwamba hospitali itajengwa Katoro. Kwa hiyo, nitumie fursa hii kumwomba Mheshimiwa Waziri kwamba hebu atutafutie fedha popote ili hospitali hii iweze kujengwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wote tunafahamu Katoro ni Mamlaka ya Mji Mdogo, lakini ukiangalia uhalisia ni zaidi ya Mamlaka ya Mji kamili. Kwa hali halisi ya kibiashara kutokana na shughuli za uchimbaji wa madini, pamoja na shughuli za uvuvi na shughuli za biashara, watu wengi sana wako mahali pale. Kwa kweli ni Mji wa kibiashara, tunahitaji hospitali. Watu ni wengi, tunahitaji huduma. Ukienda kwenye kile Kituo cha Afya cha Katoro kimezidiwa. Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri kwa kweli mtutazame kwa macho mawili. Ninajua kwamba wewe umeshafika Katoro, kwa hiyo, nakuomba kabisa, ikiwezekana tuma timu maalum ije iangalie changamoto ilivyo kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wanawake wanahangaika sana. Mara kwa mara hata ukienda katika hosptali ya rufaa ya mkoa zaidi utakuta watu wengi wanatoka Katoro, kila dakika gari la Katoro linapeleka wagonjwa kwenye Hospitali ya Rufaa. Kwa hiyo, naomba sana Mheshimiwa Waziri atuangalie; na Mheshimiwa Waziri Mkuu ameshatuahidi kwa hiyo tunaomba sasa utekelezaji uweze kufanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo pia, katika Sekta hii ya Afya tuna upungufu mkubwa sana wa watumishi. Kwenye Wilaya ya Geita tu tuna upungufu wa takribani watumishi zaidi ya 150, ni wengi sana. Kwa hiyo, tunaiomba Serikali katika bajeti hii tuangalie namna ya kuwekeza zaidi kuajiri watumishi katika Sekta ya Afya ili hatimaye tuweze kufikia ile azma ya kuweza kupunguza vifo kwa ajili ya akina mama pamoja na watoto. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaamini kabisa kwamba kwa juhudi ambazo zinaendelea kufanyika na Serikali ile changamoto iliyokuwepo katika Mikoa ya Kanda ya Ziwa ya vifo vya akina mama tuna imani kabisa kwamba itakwenda kupungua sasa. Cha msingi, naiomba Serikali iendelee kutuongezea kipaumbele, yaani mtupe kipaumbele zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Sekta hiyo hiyo ya Afya, kuna Kituo changu cha Afya cha Bukoli ambacho kwa muda mrefu sana kimekuwa na changamoto kubwa sana. Hatuna gari la wagonjwa katika eneo hilo, tarafa nzima haina gari la wagonjwa. Bahati nzuri Mheshimiwa Waziri aliniahidi. Kwa hiyo naomba sana, mara magari yakipatikana, tunaomba sana ukumbuke Kituo hiki cha Afya cha Bukoli kiweza kupatiwa gari la wagonjwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile naomba Wizara ya TAMISEMI pamoja na Wizara nyingine kama Wizara ya Nishati. Wizara ya Nishati kuna changamoto kubwa sana, unakuta eneo umeme umefika, lakini unakuta kwenye huduma za afya, labda kwenye elimu; shule za sekondari hakuna umeme. Hii ipo, kwa mfano, Kituo cha Afya Bukoli, pamoja na kwamba umeme umefika Bukoli mwaka 2014 lakini mpaka leo kituo cha afya hakina umeme. Kwa hiyo, upasuaji hauwezi kufanyika bila ya kuwa na umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kibaya zaidi wamefuatilia lakini wanaambiwa ili kuweka tu umeme pale watoe shilingi milioni 10. Yaani kituo cha afya kupatiwa umeme lazima shilingi milioni 10 zitolewe zilipwe TANESCO. Kwa hiyo, ninaiona hii ni changamoto kubwa sana. Kwa hiyo, naiomba Wizara ya TAMISEMI pamoja na Wizara nyingine; Wizara ya Nishati, hebu tuangalie namna bora ya kuweza kufanya kazi kwa ushirikiano. Hapa tutaweza kuokoa maisha ya wananchi wetu na wataweza kupata huduma zao vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nichukue nafasi hii kipekee kumpongeza Mheshimiwa Waziri wa Utawala Bora. Nimeangalia katika kitabu chake ukurasa wa 83 ameweza kuzungumzia jinsi ambavyo ameandaa Mpango wa MKURABITA wa kurasimisha maeneo maalum kwa ajili ya wachimbaji wadogo wa madini katika Mkoa wa Geita. Kwa hiyo, nitumie fursa hii kumpongeza sana kwa mpango huu. Naomba utekelezaji uweze kufanyika kama ambavyo ameweza kupanga. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wote tunafahamu mkoa wetu, tunategemea shughuli za uchimbaji wa madini. Kwa miaka mingi wachimbaji hawa walikuwa wadogo wadogo, walikuwa hawawezi kutambulika. Kwa mpango huu sasa wa kurasimisha wachimbaji wadogo, tuna imani kubwa kwamba tutaweza kupata mchango mkubwa sana katika pato la Taifa kwa ujumla pamoja na mkoa wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini vilevile…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Lolesia Bukwimba.

MHE. LOLESIA J. BUKWIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, basi ninaunga mkono hoja. Ahsante sana kwa nafasi. (Makofi)