Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

Hon. Dunstan Luka Kitandula

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mkinga

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa fursa hii na mimi niweze kuchangia hoja iliyopo mbele yetu. Nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema ambaye ametuwezesha kuiona siku hii ya leo. Pili, niwapongeze Waheshimiwa Mawaziri wa Wizara zote zenye hoja hii na kwa bahati nzuri sana wote wamefika Mkinga, wanaifahamu Mkinga, wanajua changamoto za Mkinga, nawapongeza kwa jitihada mnazozifanya za kutusaidia watu wa Mkinga tuweze kupiga hatua, ahsanteni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue fursa hii kuishukuru sana Serikali kwa jitihada ambazo imefanya kuhakikisha kwamba sekta ya afya katika Wilaya yetu inapiga hatua. Mwaka jana tulipata fedha za vituo viwili vya afya takribani Sh.1,100,000,000. Vituo vile vimekamilika na nimepata taarifa tumepata vifaa vya takribani shilingi milioni 300, kwa hiyo, vituo vile vitaanza kufanyakazi haraka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa naangalia bajeti ya mwaka huu unaokuja nimeona kilio chetu kimesikilizwa. Moja ya kilio ambacho nimekuwa nakipigia kelele sana kila mwaka ilikuwa ni ujenzi wa hospitali ya wilaya. Waziri alipokuwa akiniahidi nilikuwa naona kama vile ananidanganya lakini leo nimeona tumetengewa milioni 500 tuanze ujenzi wa hospitali ya wilaya, nashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kwamba mmeweka benchmark kwenye ujenzi wa hospitali za wilaya, tumezoea tukisikia Sh.1,500,000,000 sasa sisi mmetuanzia na Sh.500,000,000 tunajua hizo bilioni zinafuata. Kwa hiyo, tunaomba muemndele kuweka nguvu ili tuweze kupata fedha hizi. Jambo hili litawasaidia sana watu wa Mkinga lakini litatusaidia vilevile kwenye hospitali yetu ya Mkoa ya Bombo ambayo imekuwa na msongamano mkubwa wa kupata wagonjwa kutoka Mkinga, jambo hili sasa linakwenda kuondoka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilipokuwa nikipitia hotuba ya Waziri ukurasa wa 32 mpaka 34 nimefarijika kwa sababu mwaka jana kwenye eneo la lishe nilishangaa kwamba hakukuwa na neno lolote kuhusu lishe. Waziri akaniambia ilikuwa ni kupitiwa na kweli kwa sababu mwaka huu naona ameweka page maalum kwa ajili ya lishe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze dada yangu Mheshimiwa Sakaya amezungumzia jambo hili la lishe. Mimi kama Mwenyekiti wa kikundi cha lishe napokuwa na Wajumbe makini namna hii wanaoweza kuzielezea issue tunazozijadili kwa umahiri nafarijika sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba tusikilizane kidogo, kama Taifa tuna tatizo kubwa la lishe. Utafiti wa Hali ya Afya Nchini wa mwaka 2015/2016 unatuambia kwamba watoto wetu chini ya miaka mitano asilimia 30 wana udumavu. Hii maana yake ni kwamba watoto milioni 2,700,000 wamedumaa katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii maana yake nini? Maana yake watoto hawa hawawezi kufundishika vizuri, makuzi yao ni tatizo na fursa huko mbele ya safari za kuijiondoa kwenye umasikini ni giza. Kwa kuwa na watoto hawa ambao wa udumavu maana yake watazalisha vilevile kizazi chenye udumavu, kwa hiyo, hili ni janga kwa Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka jana Bunge hapa tulipitisha shilingi bilioni 15 kwa ajili ya lishe. Kinachonisikitisha ni kwamba mpaka Desemba, fedha zilizotoka kwa ajili ya jambo hili ni asilimia 40 tu. Takribani Halmashauri 31 zilikuwa hazijatenga fedha kwa ajili ya jambo hili, hii haikubaliki. Najua kazi kubwa mnayoifanya Wizara lakini hebu tuwabane hawa ambao hawaoni kwamba tuna changamoto na tuna janga kubwa kama hili kwenye Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna Mikoa ambayo utapiamlo ni zaidi ya asilimia 40. Mikoa hiyo ni Dodoma, Ruvuma, Rukwa, Kigoma, Katavi na Geita. Cha kusikitisha katika Mikoa hiyo ni Dodoma peke yake ndiyo ilikuwa imetenga fedha zile na zimetumika, mikoa mingine utumikaji wa fedha zile ni kwa kiasi kidogo sana. Niwaombe Serikali muwabane watendaji katika maeneo haya ili waone umuhimu wa kutenga fedha hizi na kutumika ili tuweze kuondoa tatizo hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie elimu. Tunashukuru Serikali kwa kutupatia fedha wka ajili ya ujenzi wa madarasa, mabweni na mabwalo katika shule zetu mbili za Maramba Sekondari na Mkingaleo Sekondari ambazo hivi sasa zinakwenda kuwa za kidato cha tano na cha sita. Mkingaleo tayari imeanza, imani yangu ni kwamba tukikamilisha kutoa fedha za haraka, Maramba Sekondari nayo mwaka huu inaweza kupokea vijana wa kidato cha tano na cha sita. Nawasihi sana tupeleke fedha hizi ili tumalizie ile kazi ndogo iliyobaki pale ili Maramba Sekondari na yenyewe iweze kupokea vijana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna changamoto ya maboma kwenye shule zetu. Tuna maboma karibu 40 ya shule za msingi lakini hatujapata fedha. Tuna upungufu wa walimu ambapo mahitaji yetu ni walimu 883 waliopo ni 481, karibu asilimia 50 upungufu, naomba tulitupie macho jambo hili. Hata kwenye sekondari walimu wa sayansi tuna upungufu karibu walimu 60, walimu 38 kwenye masomo ya baiolojia, fizikia na chemistry lakini walimu 22 kwenye somo la hisabati, tunaomba mtuangalie kwa jicho pekee.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini maombi mahsusi, shule yetu ya Kigongoi wiki mbili zilizopita tumepata balaa, madarasa matatu yameezuliwa na upepo. Tunaomba jitihada za haraka zifanyike ili tuweze kupata fedha za kurejesha madarasa yale kwenye hali yake ya kawaida ili wanafunzi wasipate shida ambayo inaendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka jana nilizungumzia Shule yetu ya Lanzoni kwamba shule ile ya sekondari hatuna maji. Watoto wanalazimika kwenda kuchota maji mtoni, mto ule umejaa mamba. Hebu tuwaondolee balaa hili ili watoto wale wasije wakajeruhiwa au wakauawa na mamba. Tunahitaji fedha pale karibu shilingi milioni nane ili tuweze kupeleka maji kwenye shule ile, tusaidieni tuondokane na kadhia hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, Mheshimiwa Waziri unajua kwa muda mrefu nimekuwa nikizungumzia suala la upungufu wa fedha za kiinua mgongo cha Madiwani. Shilingi milioni 11 zisisababishe kilio hiki bila sababu. Mheshimiwa Waziri ukiamua najua ndani ya wiki mbili zijazo hili litakuwa limeondoka, tusaidie kelele zimezidi.

Mheshimiwa Mwenyeiiti, baada ya kusema hayo, nawashukuru sana, ahsanteni. (Makofi)