Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

Hon. Abdallah Dadi Chikota

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nanyamba

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Mwenyekiti,nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia hoja iliyoko mbele yetu ambayo ni Wizara mbili, Ofisi ya Rais, TAMISEMI na Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora. Kwanza nipende kuchukua nafasi hii kuwapongeza Mawaziri wa Wizara hizi mbili, Mheshimiwa Jafo na Mheshimiwa George Huruma Mkuchika hongereni sana. Pili, nichukue nafsi kuwapongeza Manaibu wa Wazara hiyo, Ofisi ya TAMISEMI kuna Mheshimiwa Waitara na Mheshimiwa Kandege, lakini Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma kuna dada yetu Dkt. Mwanjelwa, hongereni sana kwa kazi mnazozifanya.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nitaanza kupongeza kwa kazi nzuri ambazo TAMISEMI wamefanya na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma ambazo ziko wazi kwa sababu si vyema kuanza kulaumu bila kupongeza, mnyonge mnyongeeni lakini haki yake mpeni. Kuna ujenzi mkubwa wa vituo vya afya 352 ambavyo vimesimamiwa vizuri na vingi vimeshakamilika na Mheshimiwa Rais wiki iliyopita alifanya uzinduzi Mkoani Mtwara katika kituo cha afya, Mbonde, Wilayani Masasi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kuna ujenzi wa hospitali za Wilaya 67 ikiwemo na ya Jimbo langu la Nanyamba na kwenye vituo vya afya 352 Mheshimiwa Jafo na TAMISEMI nawapongeza sana kwa sababu katika Jimbo langu tulikuwa hatuna kituo hata kimoja lakini wametuona na tumepewa vituo vitatu na vimeshakamilika na vimeshaanza kutoa huduma, kilichobaki sasa tunasubiri mashine na vifaa vingine ili huduma ziweze kutolewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, si hivyo tu kuna fedha zaidi bilioni 29 zimetolewa kwa ajili ya kukamilisha maboma. Kila siku tulikuwa tunaimba hapa kwamba kuna nguvu za wananchi zimetumika, lakini Serikali haijaunga mkono. Kwa hiyo naipongeza sana TAMISEMIkwa kuliona hili nakupeleka bilioni 29 na kunusuru hayo maboma 2,392 ambayo fedha hizo zimeenda katika Mikoa yote Tanzania Bara. Si hivyo tu kuna kimiradi ya TASAFna MKURABITA tumeona jinsi inavyotekelezwa katika maeneo yetu. Kwa hiyo nawapa hongera sana.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijatoa rai na ushauri kwa Wizara hizi nataka niweke record vizuri kuhusu mambo mawili ambayo wachangiaji waliopita wamezungumzia. Kwanza kuna mzungumzaji jana alisema maamuzi mabaya ya Serikali imepelekea Mheshimiwa Rais kusema kwamba kangomba hawana makosa. Mheshimiwa Rais kwenye ziara yake ya Mtwara hakusema hivyo, alichosema Mheshimiwa Rais ni kutoa msamaha kwa kangomba na hakusema kwamba kangomba siyo makosa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukisoma Sheria iliyoanzisha Bodi ya Korosho, Sura 203, kifungu cha 4(1), kinatoa majukumu ya Bodi ya Korosho, jukumu la kwanza ni kuhakikisha linasimamia suala la soko la korosho, lakini la pili kutoa leseni kwa mnunuzi na muuzaji wa korosho, kangomba hana leseni. Kwa hiyo Mheshimiwa Rais hakusema hivyo, Mheshimiwa Rais ametoa msamaha na hiyo ni sifa ya viongozi ambao wanasikiliza watu wao, hongera sana Mheshimiwa Rais. Kwa hiyo, tusimwekee maneno Mheshimiwa Rais wetu, hakusema hivyo Mtwara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo nataka tuweke rekodi sawa, kaka yangu hapa Makamu Mwenyekiti wa Chama cha CUF Taifa, Mheshimiwa Maftaha amesema Mkuu wa Mkoa wa Mtwara kazi yake ni kuwanyima wapinzani nafasi kwenye mikutano. Hiyo siyo sahihi, Mkuu wetu wa Mtwara anajua majukumu yake, ni mtu ambaye anafuata taratibu lakini sisi Wabunge kama viongozi tufahamu itifaki ya ugeni wa Rais. Siku ya ugeni wa Rais kuna itifaki zake na mgeni pale ni mmoja tu Mheshimiwa Rais. Tulikuwa na Mawaziri wengi hawakupewa nafasi ya kuongea.

T A A R I F A

MHE. MAFTAHA A. NACHUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Tulikuwa na Wabunge wengi walipewa nafasi ya kuongea.

MHE. MAFTAHA A. NACHUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Maftah taafifa.

MHE. MAFTAHA A. NACHUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kumpa taarifa Mheshimiwa Chikota namheshimu sana kwa yale ambayo anayozungumza kwa sababu alivyokuja Mheshimiwa Rais siku ya tarehe 2 tulipewa ratiba siku moja kabla ya ziara yake katika Jimbo langu la Mtwara Mjini ilikuwa ni pale Uwanja wa Ndege (Airport) na pale Naliendele na ratiba imepangwa, Mbunge wa Jimbo la Mtwara Mjini ambaye ndiyo mimi ninayezungumza sikuwepo kwenye ratiba hiyo. Sasa asijaribu kupotosha Bunge, kile nilichokizungumza ni kitu sahihi kabisa kwamba Mkuu wa Mkoa anakiuka taratibu za utawala bora.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Abdallah Chikota.

MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Mwenyekiti, siipokei taarifa hiyo, nilikuwa naendelea kusema kwamba siku ya pili, siku ya uzinduzi wa ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami kutoka Mtwara - Newala - Masasi kilometa 50, Mheshimiwa Rais alimuita Mbunge wa Jimbo husika na Mheshimiwa Maftah hakuwepo na ndiyo maana Mheshimiwa Rais akasema Mbunge wa Viti Maalum, akampa nafasi Mheshimiwa Wambura. Kwa hiyo, angekuwepo siku ile angepewa nafasi ya kuongea.

T A A R I F A

MHE. SELEMANI S. BUNGARA: Taarifa.

MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naendelea na mchango wangu.

MHE. SELEMANI S. BUNGARA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naendelea na mchango wangu na kuweka record sawa.

MHE. SELEMANI S. BUNGARA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Haya Mheshimiwa Bwege, taarifa.

MHE. SELEMANI S. BUNGARA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Mbunge anayeongea sasa hivi asipotoshe. Mimi nilikuwepo katika msafara na Mheshimiwa Maftaha ni Mbunge wa Jimbo la Mtwara Mjini na Mkutano wa kwanza ulifanyika Mtwara Mjini, Mheshimiwa Maftaha hakupewa nafasi lakini tulipofika pale…

MWENYEKITI: Sasa unachangia au taarifa? Si umeshasema taarifa tayari?

MHE. SELEMANI S. BUNGARA: Tulipofika katika Kiwanda cha Korosho akaitwa Mheshimiwa Hawa Ghasia akapewa nafasi akahutubia. Kwa hiyo, kuna ubaguzi mkubwa katika jambo hili, kwa taarifa yako. Mlipotambua Mheshimiwa Maftaha hakuwepo siku ya pili ndiyo mkamuita, kwa hiyo, ubaguzi…

MWENYEKITI: Mheshimiwa Chikota.

MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Mwenyekiti, sipokei taarifa hiyo, Mheshimiwa mzungumzaji aliyepita sasa hivi hakuwepo siku ya pili alikimbilia Chuo cha Ualimu Kitangali kwa ajili ya ufunguzi wa Chuo cha Ualimu Kitangali, kwa hiyo, hajui kilichotokea pale Naliendele asilipotoshe Bunge.

MHE. SELEMANI S. BUNGARA: (Hapa hakutumia kipaza sauti)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Bwege, naomba unyamaze tu, endelea.

MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naendelea na mchango wangu na sasa nataka nitoe rai kwenye mambo matatu kuhusu Ofisi ya Rais, TAMISEMI. Suala la kwanza ni kuhusu fedha za mchango wa Mfuko wa Maendeleo ya Wanawake, Vijana na Walemavu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hizi fedha kwa sababu sasa hivi Wizara inaandaa Kanuni, naomba tuzingatie ushauri ambao tumepokea katika maeneo mbalimbali. Mimi kama Mjumbe wa Kamati ya LAAC tumepita maeneo mbalimbali, ushauri unaotolewa tusizingatie kutoa fedha hizi kwenye vikundi tu, tufikirie wazo la kutoa fedha hizi za mkopo kwa mtu mmoja mmoja, mlemavu mmoja, kijana ambaye ana mradi wake ambao unawezekana kupewa mkopo akiwa peke yake apewe na mwana mama ambaye ana mradi wake ambao ni viable kupewa mkopo siyo lazima awe kwenye vikundi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile tunaweza kwenda mbali tukajifunze Mkoa wa Shinyanga hasa Wilaya ya Kahama, wameamua kutenga eneo maalum kwa ajili ya vijana. Tunaweza kuchukua mfano ule tukapeleka kwenye mikoa mingine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu wa pili ni kuhusu uchaguzi wa Serikali za Mitaa ambao unakuja. Naomba Ofisi ya Rais, TAMISEMI itenge fedha za kutosha kwa ajili ya kugharamia uchaguzi huu. Tuna uzoefu kwenye chaguzi zilizopita zinatengwa fedha ndogo na kuwaambia Halmashauri wachangie kiasi kinachobaki. Halmashauri zetu uwezo wake tunaufahamu, kwa hiyo, tusiwape mzigo, tutenge fedha za kutosha ili uchaguzi huu uende kama ulivyopangwa, tukamilishe bila ya kuwa na dosari zozote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu wa tatu ni kuhusu TARURA. Kama walivyosema Wajumbe waliopita; TARURA kwa kipindi kifupi imeonyesha mafanikio makubwa sana, imefanya kazi nzuri sana lakini ina changamoto mbili. Changamoto ya kwanza bado fedha wanazopewa ni chache lakini changamoto ya pili ni watumishi. Walipewa watumishi wachache kutoka Mamlaka za Serikali za Mitaa na kutengeneza pengo la uhaba wa Wahandisi kwenye Mamlaka za Serikali za Mitaa. Kwa hiyo, nashauri Ofisi ya Rais, TAMISEMI kwa kushirikiana na Ofisi ya Menejimenti ya Utumishi wa Umma watoe kibali maalum ili TARURA waweze kupata wafanyakazi wa kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu mwingine ni kuhusu Ofisi ya Rais, TAMISEMI; kuna changamoto ya Wakuu wa Idara wengi kuwa makaimu na hii naomba mshirikiane na kaka yangu Mheshimiwa George Huruma Mkuchika, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa sababu malalamiko mengi ambayo wanatoa Wakurugenzi kwamba suala la upekuzi kwa wale watarajiwa linachukua muda mrefu sana. Kwa hiyo, hili suala la upekuzi kama walivyosema Wajumbe wengine tuliwekee mkakati ili upekuzi ufanyike kwa muda mfupi na wale wenye sifa waweze kuteuliwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. (Makofi)