Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

Hon. Felister Aloyce Bura

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

MHE. FELISTER A. BURA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia na nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa uhai ambao ametupatia siku ya leo sisi Wabunge kwa ajili ya uwakilishi wa wananchi waliotuchagua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii kumpongeza sana Rais wetu Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa mambo makubwa anayowafanyia Watanzania. Kuna msemo unaosema Nabii hakubaliki kwako lakini kuna nchi wanazotamani Magufuli awe Rais wao kwa utendaji na utekelezaji mzuri wa Ilani ya Chama cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndugu zangu tuwaombe viongozi wetu Mungu awape afya njema na waendelee kutawala kwa hekima na maarifa itokayo kwa Mungu. Wanafanya kazi nzuri, tuwa-support kwa jinsi wanavyofanya kazi nzuri. Sisi wananchi wa Dodoma tupo pamoja nao, tunawaombea kwa Mwenyezi Mungu lakini zaidi ya yote tunafanya kazi. Wabunge wa Dodoma tunafanya kazi kuonyesha kwamba tunamuunga mkono Rais wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi tumefanyiwa mambo mengi sana na Serikali ya Awamu ya Tano. Serikali ya Awamu ya Tano imefanya mambo makubwa sana kwa Mkoa wa Dodoma. Kwa hiyo, tutamuunga mkono Rais wetu, treni ile iliyokuwa ya Mwakyembe Dar es Salaam utaikuta Dodoma, barabara za mizunguko utazikuta Dodoma, soko la kimataifa na standi ya kimataifa utavikuta Dodoma. Niwaambie Waheshimiwa Wabunge usipojenga Dodoma utajutia maisha yako na familia yako itakulaani kwa nini hujajenga Dodoma kwa sababu Geneva ya Tanzania inakuja kuwa Dodoma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuendeleza mji kuna mambo, kuna utwaaji wa ardhi na shughuli mbalimbali za maendeleo zinazoendeleza. Wananchi wangu wa Dodoma wa Msalato pale ambapo uwanja wa Kimataifa unajengwa kuna wanaodai fidia. Niombe Serikali iwalipe wananchi wale fidia ili wakianza kujenga kusiwepo na malalamiko ya wananchi. Eneo la Ihumwa limechukuliwa kwa ajili ya bandari kavu, niiombe Serikali sasa wale wananchi walipwe fidia ili wasiendelee kuidai Serikali. Tunajua Serikali inafanya kazi kubwa lakini pia niombe kwamba malalamiko haya madogo sasa yasiwepo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na ongezeko la watu Dodoma, shule sasa zimejaa sana watoto; shule za msingi na sekondari. Mwaka huu tumeandikisha watoto shule za awali 15,000, watoto wa darasa la kwanza tumeandikisha 11,979, hawa si wachache. Tumejikita sana kwenye ujenzi wa shule za sekondari tukasahau kwamba watoto wa shule za msingi wanahitaji pia madarasa, wanavyoongezeka madarasa hayatoshi. Utafiti ufanyike kuona kwamba hawa watoto wanaoanza shule, kwa mfano hawa 15,000 shule ya msingi watakwenda wapi, madarasa hayatoshi. Tumekazania kujenga shule za sekondari lakini za msingi je? Madarasa ya shule za msingi hatujaongeza muda mrefu, Serikali iangalie suala hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini sisi Dodoma tulitoa ardhi kwa Serikali kwa ajili wa ujenzi wa shule nyingine, shule ya kitaifa badala ya Shule ya Sekondari ya Mazengo. Tulitoa ardhi na Waziri wa Elimu alipewa ile ardhi kwa ajili kujenga shule ya kifaifa badala ya Shule ya Mazengo iliyorudishwa kwa waliokuwa wamiliki wa Kanisa la Anglikana. Sasa eneo lile tulilolitoa kwa ajili ya ujenzi wa shule ya kitaifa mpaka sasa haijajengwa mwishowe wananchi watavamia lile eneo halafu tutaanza sasa suala la ulipaji fidia. Niombe sasa Wizara ikachukue eneo lile kwa sababu shule inayojengwa pale ni ya kitaifa itachukua wanafunzi Tanzania nzima basi waanze suala la ujenzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lile tulilolitoa kwa ajili ya Shule ya Kitaifa halijajengwa mpaka sasa, mwisho wananchi watavamia lile eneo halafu tutaanza sasa suala la ulipaji fidia. Naomba Wizara ikachukue lile eneo kwa sababu shule inayojengwa pale ni ya Kitaifa, itachukua wanafunzi Tanzania nzima, basi waanze suala la ujenzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba Walimu 656 wa shule za msingi kwa shule za Dodoma za pembezoni. Dodoma Jiji kuna mahali ikama ni Walimu 10 lakini utakuwa Walimu wako watatu tu. Naiomba Serikali ya Mheshimiwa Dkt. Magufuli, Serikali Sikivu, Serikali inayowajali wanyonge, Serikali iliyoamua kwamba kila mtoto apate elimu. Mtoto atapata elimu nzuri tu kama Walimu wako shuleni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba maeneo yote na siyo Dodoma tu, naombe maeneo mengine ambayo Walimu hawatoshelezi tuletewe Walimu wa kutosheleza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunataka Serikali ya viwanda, yaani tunataka kujenga viwanda; hatuwezi kujenga viwanda kama hatuna wanasayansi na Walimu wa Sayansi ndio hawatoshi katika maeneo yetu. Naiomba Serikali yangu, wako Walimu waliomaliza Elimu ya Vyuo Vikuu na walisoma masomo ya sayansi, tuombe sasa katika ugawaji wa Walimu wa Shule za Sekondari, tupeni hao Walimu ili tuwapate watoto watakaotumika viwandani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kumaliza suala la elimu, niombe sasa, katika Jiji letu tuna vijiji 34 ambavyo tunavihesabu kama ni mitaa. Wawekezaji wako wengi lakini hatuna umeme, vijiji hivyo vipate umeme.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru sana na kumpongeza Mheshimiwa Joel Mwaka amezungumzia suala la hospitali ya Uhuru na pesa za kujenga hospitali ya Uhuru ilitokana na maadhimisho ya Desemba 9, Mheshimiwa Rais akaamua hizo fedha zijenge Hospitali ya Uhuru Wilayani Chamwino. Mpaka leo fedha hizo hazijafika katika Halmashauri ya Wilaya ya Chamwino ili zijenge hiyo hospitali. Naiomba Serikali, katika bajeti hii hizo fedha zije na kama zilishatengwa na Mheshimiwa Rais alitamka, tupeni hizo fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jengo la Halmashauri ya Wilaya ya Chamwino ina miaka zaidi ya kumi wamehamia lakini wamehamia floor ya chini, lile jengo halijaisha. Tumeomba shilingi milioni 900 ili tujenge jengo lile la Halmashauri. Tunawashukuru kwamba mmetupa shilingi bilioni tatu kwa ajili ya ujenzi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, hizo fedha zije sasa ili Mkuu wa Mkoa awe na ofisi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru Mheshimiwa Mariam amezungumzia suala la mabasi ya mwendokasi. Tunaishukuru Serikali na kuipongeza kwamba sasa hivi usafiri wa Dar es Salaam ni wa haraka, lakini mabasi yale mengi yameharibika, yatengenezwe sasa. Miundombinu ya mwendokasi imechukua pesa nyingi za Watanzania, Serikali ikubali kwamba yeyote mwenye uwezo wa kuendesha njia ya mwendokasi, basi waweke magari pale yaweze kuwahudumia Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado tuna maboma ambayo hayajakamilishwa au kuna maeneo ambayo vituo vya afya havijafika. Naomba Kata ya Kolo Wilayani Kondoa, wananchi wanatembea kilometa 30 kwenda kutafuta huduma ya afya. Naomba sana, Serikali itusaidie Kituo cha Afya pale Kondoa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Posho ya Madiwani; Madiwani ni watu muhimu katika Taifa hili, wanafanya kazi kubwa. Madiwani wafikiriwe, wanafanya kazi kubwa, lakini posho inayotolewa kwa Madiwani haitoshi, kidogo mno; na wakati mwingine wanakaa hata miezi mitatu hawajapata posho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Serikali yangu sikivu inayowajali wananchi wake, Posho za Madiwani zikafanyiwe ufumbuzi sasa ili Madiwani wafanye kazi kwa moyo mmoja.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Felister.

MHE. FELISTER A. BURA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naunga mkono hoja.