Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

Hon. Mariamu Nassoro Kisangi

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kujadili hoja hii ya TAMISEMI. Kwanza napenda kuipongeza sana Serikali ya Chama cha Mapinduzi kwa jinsi ilivyoweza kutekeleza Ilani yake ya Chama cha Mapinduzi; kwa kipindi hiki cha miaka mitatu tumefikia asilimia 90, hali ambayo inawafanya wenzetu wa upande wa kule waanze kutetemeka. Nasema Chama cha Mapinduzi kiko vizuri na Serikali ya Chama cha Mapinduzi iliyoko madarakani inafanya kazi nzuri na tutaona 2020 tumejipanga vizuri, Wabunge wa Chama cha Mapinduzi watatawala katika Bunge hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda nipongeze Serikali yangu na nimpongeze Mheshimiwa Rais, Dkt. Magufuli kwa utendaji wake mzuri uliotukuka wa kujali wananchi wake katika maeneo mbalimbali bila kujali jimbo hili ni la nani, jimbo hili ni la Chama cha Mapinduzi, jimbo hili ni la Upinzani, Mheshimiwa Rais wetu anafanya kazi kwa ajili ya wananchi wake bila kuangalia tofauti za chama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niseme nchi yetu, au Serikali yetu ni kweli inaendeshwa katika misingi ya utawala bora, misingi ya utawala bora inazingatiwa na ndiyo sababu tuko hapa. Utawala bora uko katika maeneo mbalimbali; uko katika viongozi lakini uko katika wale wanaoongozwa pia. Ili nchi yetu iwe vizuri, wote tunatakiwa tuendeshe nchi yetu na tuishi sisi kama viongozi kwa kuzingatia misingi, maadili, kanuni na taratibu za nchi yetu, kiongozi ambaye atakwenda tofauti na maadili ya nchi, huyu hatakubalika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nije kwenye hoja ya TAMISEMI; kwanza napenda nimpongeze Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI, Mheshimiwa Waziri wa Utawala Bora, Naibu Mawaziri wote kwa kazi nzuri. Kwa kweli Serikali yetu imefanya kazi nzuri kwenye ujenzi wa hospitali za mikoa na wilaya wameweza kutoa karibu bilioni 1.5 kwa kila mkoa ambao hauna hospitali za mikoa na zile za wilaya. Pia ujenzi wa zahanati na ukarabati wa vituo vya afya Tanzania nzima, karibu vituo 325 ambavyo umegharimu bilioni 184.67, si jambo dogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia katika maboresho ya Jiji la Dar es Salaam kwa kweli Jiji la Dar es Salaam sasa hivi limefanyiwa maboresho makubwa sana, lazima tuseme, ni ukweli usiopingika. Dar es Salaam ukienda kila kona unakutana na ujenzi wa barabara, sio kazi ndogo iliyofanywa na Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kutoa shukrani hizo, sasa nakuja kwenye mchango wangu ambapo nitajikita moja kwa moja katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI, ukurasa wa 29, 83 na 87. Naanza na ukurasa wa 29 wa maboresho ya huduma za afya, kweli hospitali na vituo vya afya zimeboreshwa tena siyo vile vya Serikali tu, Serikali hii ya Chama cha Mapinduzi katika utekelezaji wake wa Ilani kwa kutumia Mfuko wa Bima ya Afya umeweza kukarabari hospitali binafsi pia. Kwa kweli leo hii ukienda zahanati ya binafsi siyo ile iliyokuwa mwaka 47, utakuta ina miundombinu mizuri na iko vizuri kwa kweli zahanati za Mkoa wa Dar es Salaam zipo vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na ukarabati huo, niiombe Serikali iiangalie kwa jicho la huruma Zahanati ya Mbagala Zakhem. Kweli Mbagala Zakhem kuna tatizo la ardhi kwamba eneo ni dogo lakini kama Halmashauri tumeboresha Hospitali ya au Zahanati ya Maji Matibu na Charambe ili kusaidia wale wananchi lakini ukweli utabaki kuwa ukweli jiografia ya Mbagala na jinsi Mji wa Mbagala unavyokuwa kwa kasi Hospitali ya Zakhem iko barabarani hivyo inapotokea majeruhi anapelekwa pale baadaye anapelekwa Temeke. Huwezi ukamtoa mtu Mbagala Zakhem ukamrudisha Mbagala Maji Matitu akatokee wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe sana Serikali, pamoja na mambo yote mazuri tunayofanya tuiangalie hospitali ile kwani kutwa inapokea majeruhi, watu ambao wamejaa pale Mbagala, wafanyabiashara, wajasiriamali na watu wote wanaopata matatizo wanakimbilia pale. Kwa hiyo, Hospitali ile ya Mbagala Zakhem imezidiwa pamoja na kwamba kuna zingine pembezoni lakini ile bado inauhitaji wa aina yake, niombe Serikali iongeze nguvu kusaidia eneo hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nije kwenye ukurasa wa 83, Tume ya Utumishi ya Walimu, niseme ukweli kwamba bado lipo tatizo kwa walimu. Walimu wanadai hela zao za promosheni mpaka wengine wanafikia kustaafu lakini bado wanadai. Pia walimu wanateseka bado wanadai nauli zao. Ninao mfano wa walimu wa Halmashauri ya Temeke, wale ambao wamestaafu mpaka leo hawajalipwa nauli zao na hela zao za promosheni. Walimu wale wanahangaika wakati wameitumikia nchi kwa uadilifu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nikiwa mwalimu ambaye nimetoka kwenye elimu ya msingi, walimu wenzangu wananiuliza yaani wewe umefika huko mjengo unatusahau? Nawaambia sijawasahau na ni wajibu wangu kuwasemea. Niiombe Serikali ichukue hatua na ishuke kwenye Halmashauri iwaulize tatizo ni nini mpaka hawa walimu hata anayemaliza leo na bajeti zipo kwa nini hawalipwi? Nikuombe sana Mheshimiwa Waziri ukaliangalie hilo, walimu ni walezi, wamelea watoto zetu wametulea mpaka wenyewe Wabunge hapa wote tumepitia kwenye elimu, kwa hiyo naomba waendelee kuwajali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nije kwenye ukurasa wa 87, mradi wa DMDP, nitoe shukrani za dhati kabisa kwa Serikali kwa uwezeshwaji wa mradi huu. Mradi huu umeleta maendeleo makubwa katika Jiji letu kwani sasa limebadilika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii Mbagala Kijichi huwezi kudhani kama ni Mbagala ile, barabara zimetawala, soko la kisasa na miradi kadha wa kadha imejengwa. Pia katika maeneo ya Yombo Vituka, Kilakala, Tegeta, Mikocheni, Buguruni, Ilala, Upanga, Temeke, Chang’ombe, barabara ile imepanuliwa kwa mradi wa DMDP, ni jambo kushukuriwa. Vilevile barabara ya Ubungo, Kibamba na Gerezani, zimeshughulikiwa, kwa kweli hali za barabara zetu katika Jiji la Dar es Salaam ni nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulikuwa tunasimama hapa ndani mimi na Mheshimiwa Mnyika tunazungumzia barabara ya Kibwegele – Kibamba, leo hii Mnyika amenyamaza kimya anahangaika tu na mambo yake ya Mahakama. Hii yote ni kutokana na kazi nzuri iliyofanywa na Serikali katika Jimbo la Kibamba na Mkoa mzima wa Dar es Salaam. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa niende kwenye upande wa mabasi yaendayo kasi, kwa kweli niipongeze Serikali sasa mabasi yaendayo kasi mradi ule unatekelezeka. Tayari fidia zimelipwa na unaanza kujengwa kwa mabasi yanayoanzia kutoka Gerezani kwenda Mbagala Rangi Tatu. Tunamshukuru sana Mungu na Serikali yetu kwa kuliwezesha hilo. Mradi ule utakapokuja pale Mbagala Rangi Tatu maeneo ya Mbagala, Charambe, Kiburungwa, Mianzini yatapanda thamani kutokana na miundombinu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini najua penye jambo jema hapakosi changamoto. Kweli mradi wa mabasi ya mwendo kasi hivi karibuni umeleta umeleta changamoto kubwa kwa hasa yale yanayotoka Mbezi, Kimara kwenda mjini, kweli kumekuwa na uhaba. Nikushukuru sana Mheshimiwa Waziri jinsi ambavyo unakwenda kufuatilia kwa karibu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niiulize Serikali ule uhaba wa mabasi unatokana na nini? Niishauri Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam kama ina fedha nyingi pamoja na mabasi yake ya utalii basi yale mabasi ya utalii iongezewe nguvu Halmashauri ya Jiji waweze kununua mabasi ya akiba iwapo kutatokea tatizo lolote basi mabasi yetu wenyewe ya Serikali au Halmashauri ya Jiji yawe yanaingia kwenye miundombinu ya mwendo kasi kuwasaidia wananchi wa Dar es Salaam.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Mariam.

MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja, naipongeza Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi, iendelee hivyo hivyo. Mheshimiwa Rais, Mheshimiwa Waziri Mkuu na Makamu wa Rais wote kwa pamoja pigeni kazi wananchi wanawaamini. (Makofi)