Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Anthony Peter Mavunde

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Dodoma mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, (KAZI, VIJANA NA AJIRA): Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nami napenda nichukue fursa hii kwanza kabisa kumshukuru sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa heshima kubwa aliyonipa kuendelea kuhudumu katika eneo hili na imani kubwa aliyonionesha katika eneo hili ambalo mpaka hivi sasa nalihudumu kama Naibu Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia namshukuru sana Makamu wa Rais, pamoja na Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa miongozo yao, lakini kipekee kabisa niwashukuru sana Mawaziri, mama zangu wapendwa kabisa, mama Jenista Mhagama na dada Angella Kairuki kwa namna ambavyo wameendelea kunipa ushauri na kuniongoza na upendo wao wa dhati kwangu. Mwenyezi Mungu awabariki sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri mwenzangu Mheshimiwa Ikupa Stella Alex kwa ushirikiano mkubwa anaonipa katika kutimiza majukumu yangu kama Naibu Waziri. Tunafanya kazi kwa ushirikiano na upendo mkubwa sana, nakushukuru sana dada Ikupa. Niwashukuru vile vile Makatibu Wakuu wote, ambao siwezi kuwataja lakini nawashukuru wote chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu, niwashukuru Watendaji wa Wizara, lakini mwisho niwashukuru sana wananchi wa Jimbo la Dodoma Mjini ambao walinionesha imani ya kuwa Mbunge wao, nawashukuru sana kwa upendo wao na naendelea kuwafanyia kazi ya kuwatumikia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hapo sasa naomba nijielekeze katika kujibu na kufafanua hoja ambazo zimeletwa na Waheshimiwa Wabunge. Hoja ya kwanza ambayo nitaanza nayo, ni hoja ya ujumla juu ya miradi ya kukuza ujuzi ambayo inatekelezwa chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu. Waheshimiwa Wabunge wanaonesha namna ambavyo pia Serikali tuwashirikishe katika utekelezaji wa miradi hii ili wapate uelewa, lakini vilevile, wawe wanai-own wenyewe kwa maana ya nafasi zao za uwakilishi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli; chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu tunatekeleza miradi ya ukuzaji ujuzi hasa kwa vijana na ambao katika mradi mmoja tulioanza nao hivi sasa mkubwa kabisa, ni mradi wa kitalunyumba ambao utakwenda kuwagusa vijana 18,800 nchi nzima. Mradi huu wa ukuzaji ujuzi, ni mradi ambao utakwenda kuifikia kila halmashauri vijana 100, ambapo vijana 80 watafundishwa kulima kupitia kitalunyumba, na vijana 20 watafundishwa kutengeneza kitalunyumba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika awamu ya kwanza tunafarijika kusema kwamba, wale vijana walioanza katika awamu ya kwanza hivi sasa wameshapata ujuzi wa kutengeneza vitalunyumba na wameanza kuaminiwa na kupata ajira katika baadhi ya makampuni hapa nchini. Katika utekelezaji wa mradi huu, kama Waheshimiwa Wabunge walivyosema, utaratibu ni kwamba, Ofisi ya Waziri Mkuu iliandika mkoani na baadaye, mkoani walitoa taarifa katika wilaya, lakini kwa maelekezo ya Mheshimiwa Waziri Mkuu ambao pia alielekeza kwa Waziri wetu, ambaye pia ameshusha kwetu, Mheshimiwa Jenista Mhagama, kwamba hivi sasa miradi hii yote katika awamu ya pili ya utekelezaji tunaandaa utaratibu maalum wa kuhakikisha kwamba kila Mbunge katika eneo lake anafahamu mradi unavyotekelezwa na atapewa taarifa za awali. Tumeanza katika kutoa semina na kuelimisha Waheshimiwa Wabunge juu ya utekelezaji wa mradi huu, ambao naamini kabisa utakwenda kukidhi mahitaji katika kutatua changamoto za ukosefu wa ajira na ukosefu wa ujuzi kwa vijana wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja ya pili ambayo ilizungumzwa hapa, ni hoja ya mkakati wa kusaidia ajira kwa vijana hasa vijijini. Ni hoja ambayo Wabunge wengi wameisema na wanataka kusikia mkakati wa Serikali. Mkakati wa kwanza wa Serikali katika kuhakikisha tunatatua changamoto ya ajira hasa kwa vijana. Eneo la kwanza tunalolifanya ni katika kutoa elimu hasa katika kundi hili kubwa la vijana, kwanza kabisa kwenye tafsiri ya neno ajira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa Sera ya Ajira, ya mwaka 2008, ajira ni shughuli yoyote halali inayomuingizia mtu kipato. Kwa hiyo, tunaanzia hapo kwanza kuwafanya vijana wetu na wananchi wote kwa ujumla kuelewa nini maana ya ajira kwa sababu kumekuwepo na dhana kwamba, ili mtu aonekane ameajiriwa lazima awepo ofisini tu. Kwa hiyo tumeanza na eneo hilo la kwanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili, tunafahamu haiwezekani na katika hali ya kawaida watu wote kuweza kupata ajira katika mfumo rasmi. Kwa hiyo katika hili pia tunachokifanya ni kuelezea fursa zilizopo katika sekta isiyo rasmi ambayo pia itawezesha watu wengi zaidi waweze kupata ajira. Kwa hiyo, katika eneo hili, mkakati wetu ni kwamba hivi sasa kama Serikali kupitia azimio la mwaka 2014, ambalo lilikuwa ni chini ya aliyekuwa Waziri Mkuu wakati huo, Mheshimiwa Mizengo Kayanza Peter Pinda, ilifanyikia Dodoma la Wakuu wa Mikoa wote kutenga maeneo maalum kwa ajili ya shughuli za uzalishaji mali kwa ajili ya vijana. Mpaka ninavyozungumza hivi sasa, tayari yametengwa maeneo ya takribani ekari laki mbili kumi na saba elfu, mia nane na themanini na mbili nchi nzima kwa ajili ya shughuli za vijana za uzalishaji mali. Kwa hiyo lilikuwa ni eneo la kwanza katika mkakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili ni eneo la uwezeshaji, uwezeshaji wetu unafanyika kupitia Mfuko wa Maendeleo wa Vijana ambao mpaka hivi sasa tayari tumeshavifikia vikundi takribani 755 na tayari bilioni 4.5 zimetoka kwa ajili ya kuwawezesha vijana. Katika eneo hili fedha zinazotumika ni zile asilimia 10 ya mapato ya ndani ya halmashauri ambazo pia zinatumika kama sehemu ya kuwawezesha vijana kwa ajili ya kupata mitaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunayo Mifuko ya Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi ambayo ipo zaidi ya 19 ambayo ukiiunganisha kwa pamoja ina ukwasi wa kiasi cha shilingi trilioni 1.3 kwa pamoja yake, pamoja na benki ya kilimo ambayo ipo maalum kwa ajili ya kuwawezesha vijana na makundi mengine katika jamii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, katika eneo hilo la uwezeshaji pia, tunaendelea kuhakikisha kwamba vijana wengi zaidi wanapata fedha za mikopo ili wafanye shughuli za kiuchumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumetambua moja ya mkakati mwingine wa kusaidia na kutatua changamoto ya ukosefu wa ajiri ni kwenye eneo la ujuzi. Kwa mujibu wa tafiti ya mwaka 2014, ambayo inaitwa, Intergrated Labour Force Survey inasema nchi yetu ya Tanzania ina takribani watu wenye uwezo wa kufanya kazi milioni 22.3. Changamoto kubwa iliyokuwepo ni katika eneo la ujuzi, ambapo watu wenye ujuzi wa juu kabisa ni asilimia 3.6, watu wenye ujuzi wa kati ni asilimia 16.5 na watu wenye ujuzi wa chini ni asilimia 79.9. Ili kwenda kuwa nchi ya kipato cha kati, ifikapo mwaka 2025 viko vigezo vimewekwa na moja ya kigezo kilichowekwa, ni katika eneo la nguvu kazi, lazima uwe una nguvu kazi yenye ujuzi wa juu kabisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nchi yetu ya Tanzania hivi sasa, tunatekeleza mradi chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu ambao lengo lake ni kuwajengea ujuzi vijana wetu wapate nafasi ya kuweza kujiajiri wenyewe kupitia ujuzi wao. Ninavyozungumza hivi sasa, tuna mradi ambao unaitwa ni Mradi wa Kurasimisha Ujuzi kwa Vijana, ambao wana ujuzi lakini hawajapitia mfumo rasmi wa mafunzo. Hivi sasa wataalam wetu na wakufunzi wa VETA, wanawapitia vijana hawa mtaani, ukienda leo mtaani, kuna kijana anajua kuchonga vitanda vizuri, anajua kupaka rangi vizuri, ni fundi mzuri wa magari, hajawahi kusoma VETA, hajawahi kusoma Don Bosco.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inachokifanya ni kurasimisha ujuzi wake, tunakwenda mtaani na wakufunzi wa VETA wanakaa nae, wana-address upungufu alionao then tunampatia cheti cha VETA cha ufundi pasipo yeye kwenda kusoma VETA. Mradi huo kwa mwaka huu utawafikia takribani vijana elfu kumi. Waheshimiwa Wabunge katika maeneo yao wajiandae tutawafikia kwa ajili ya kuwawezesha vijana wao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia, tunao mradi wa mafunzo ya ufundi stadi ambao tunautekeleza chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu, ambapo Ofisi ya Waziri Mkuu inagharamikia mafunzo na fedha ya kujikimu kwa vijana hawa wa Kitanzania ambao tunawafundisha ufundi mbalimbali; kujenga, umeme, ushonaji, masuala ya kompyuta na fani zinginezo. Katika eneo hili tumepiga hatua kubwa sana, tumeshawasomesha vijana zaidi ya 2,278 katika awamu ya kwanza na itaendelea, lakini asilimia kubwa tayari wameshapata kazi na wengine wamejiajiri wenyewe. Kwa hiyo, ni dhahiri kuonesha kwamba program hizi za ukuzaji ujuzi zitasaidia sana katika kutatua changamoto katika eneo hili la vijana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja nyingine ambayo ilisemwa hapa, ni kuhusu mikopo ya asilimia 10 ya Halmashauri lakini vile vile na Mfuko wa Maendeleo ya Vijana namna ambavyo inachelewa kurejeshwa katika kundi hili kubwa la vijana.

Ni kweli kulikuwa kuna changamoto hiyo lakini Serikali hivi sasa kwa kushirikiana na halmashauri tumeendelea kufanya ufuatiliaji ili fedha hizi za mikopo katika makundi haya ya vijana, zirudishwe kwa maana ya Mfuko ule ambao ni revolving ili vijana wengine waweze kukopeshwa. Mpaka hivi sasa takribani shilingi milioni 356 zimerejeshwa kama sehemu ya marejesho ya mkopo ambapo vijana wengine pia watapata fursa ya kupata mkopo huo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, imejitokeza hoja nyingine hapa kuhusu vibali vya kazi na imezungumzwa na Wabunge wengi sana. Mwaka 2015 Bunge hili tukufu lilitunga Sheria Na.1 ya Uratibu wa Ajira kwa wageni hapa nchini. Kwa mujibu wa sheria ile, kifungu 11 kinatamka bayana mtu mwenye mamlaka ya kutoa kibali cha kazi ni Kamishna wa Kazi ambapo mpaka atoe kibali lazima ajiridhishe kwamba kazi inayoombwa hatuna ujuzi wa namna hiyo ndani ya nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi ndivyo sheria inavyosema iliyotungwa na Bunge. Kamishna anachokifanya ni kusimamia sheria. Kamishna huyu tuliyenaye hivi sasa, Wakili Msomi Gabriel Malata anafanya kazi yake vizuri sana, ameonesha usimamizi uliotukuka na si kweli kwamba ni Mungu mtu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa sheria hii, mtu akipeleka maombi ya kibali cha kazi inapaswa apewe ndani ya siku 14. Hivi sasa vibali vya kazi vinatoka ndani ya siku saba. Sisi tunaamini kabisa kwamba Tanzania siyo kisiwa, hatuwezi kuishi wenyewe. Tunapenda pia kupata wageni kwa ajili ya watu wetu kupata ujuzi lakini tunachokisema pamoja na hayo yote sheria yetu pia na yenyewe ichukue nafasi yake kwa maana ya vile vigezo vilivyowekwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika eneo hili najua kumekuwa na kelele nyingi sana ya baadhi ya wadau ambao wengi pia hawasemi ukweli. Kamishna anachokifanya ni kuangalia vigezo mbalimbali katika utoaji wa vibali lakini hajiongozi mwenyewe kwa mapenzi yake na nafsi yake, ni sheria ndiyo inamtaka afanye hivyo. Kuna baadhi ya maeneo kuna udanganyifu kiasi kwamba Kamishna akiachia tu kila mtu aje afanye kazi hapa, vijana wetu pia na wenyewe watakosa fursa ya ajira kama ambavyo Ibara ya 173 ya Chama cha Mapinduzi imeeleza katika Ilani ya Uchaguzi, kinachofanyika hapa ni utekelezaji wa sheria. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia sisi Ofisi ya Waziri Mkuu siyo robot kwamba hatuwezi kuangalia mazingira ya dunia ya leo, tunahitaji na tunawapenda wawekezaji. Hivyo, nitoe rai kwa wawekezaji wote nchini, kumekuwepo na tatizo la wawekezaji hawa katika ufuatiliaji wa vibali kuwatumia watu wa kati ambao wamekuwa wakileta shida.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ofisi yetu hivi sasa tumeunganishwa katika mfumo ambapo sasa tutatoa vibali vya electronic ambavyo vitapunguza urasimu. Mimi nataka mwekezaji mmoja aje anitolee mfano kwamba amewahi kuleta maombi yamekaa miezi sita hajawahi kujibiwa. Hivi sasa jambo hilo hakuna katika Ofisi ya Waziri Mkuu. Mtu akileta maombi leo, kama yamekamilika ndani ya siku saba anapata kibali chake, provided awe amekidhi matakwa yote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi sasa tunakwenda katika mfumo mzuri zaidi, kibali kitatoka chini ya siku saba kama mtu akikamilisha nyaraka zake. Tunaunganisha sasa mfumo wa vibali vya kazi na residency permit. Hivi sasa ndiyo tunakwenda katika utekelezaji wa programu hiyo, mtu akiomba kibali Kamishna wa Kazi atakiona na Uhamiaji wataona katika mfumo hapo hapo, Kamishna akimkubalia dakika hiyo hiyo Uhamiaji kule wataona wata-issue residency permit. Kwa hiyo, tunatoka kwenye mfumo wa siku saba mpaka siku moja ikiwezekana katika utoaji wa vibali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini tumekwenda mbali zaidi, kwenye eneo la rufaa, mimi ndiyo nashughulikia rufaa zote za vibali vya kazi. Hivi sasa rufaa zinazotoka TIC kwa mfumo tuliouweka hata nikikaa hapa ndani ya Bunge najibu rufaa zingine kupitia simu. Ni utaratibu ambao tumeuweka kwamba rufaa yoyote itakayoingia ili tusiwacheleweshe wawekezaji naiona moja kwa moja naijibia hapa hapa na kutoa maamuzi kama imekubaliwa au amekataliwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho kwenye eneo hili. Eneo hili lina changamoto kubwa sana na maneno huwa yanakuwa mengi sana. Katika eneo hili nataka niwaambie ndugu zangu Watanzania na Waheshimiwa Wabunge ambao mko hapa, hatufanyi kazi kwa kumuonea mtu, hatufanyi kazi kuwafukuza wawekezaji, mimi nasimamia tena eneo la ajira nafahamu maana ya uwekezaji. Mwekezaji mmoja akija hapa akiwekeza tunapata fursa za ajira, vijana wengi zaidi watapata ajira. Nitakuwa mtu wa ajabu kuwa mtu wa kwanza kuwafukuza wawekezaji kupitia sharia. Nachokisema taratibu pia zifuatwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi kweli Waheshimiwa Wabunge, atoke mtu Pakistan aje kuunga nyaya hapa na mimi nitoe kibali cha kazi? Tuwaache vijana wa VETA, Don Bosco, tumchukue mtu wa Pakistan aje kuunga nyaya Tanzania? Haiwezekani!

Kwa hiyo, tunachokifanya ni kusimamia sheria, naomba mtuunge mkono na mumpe moyo Kamishna huyu, anafanya kazi kubwa sana. Mkianza kumzonga na maneno hapa ndugu zangu mtamfifisha moyo, mpeni moyo, kazi yake ni kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. (Makofi)