Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Stella Ikupa Alex

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU (WENYE ULEMAVU): Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipatia nafasi. Awali ya yote, naomba nitumie nafasi hii kumshukuru sana Mwenyezi Mungu ambaye ameniwezesha tena siku ya leo kuwa mbele ya Bunge lako Tukufu ikiwa ni mwaka 2018 nilipochangia bajeti ya Ofisi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu. Ninamshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naomba nitumie nafasi hii kuendelea kumshukuru sana Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa miongozo na maelekezo ambayo ameendelea kunipatia katika nafasi hii ambayo ninahudumia kama Naibu Waziri ambaye nashughulikia masuala ya watu wenye ulemavu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru sana Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa miongozo ambayo imeniwezesha na imeendelea kuwezesha kundi hili la watu wenye ulemavu mahitaji yao kuweza kutekeleza vizuri. Pia naomba nitumie nafasi hii kumshukuru sana Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Sera, Bunge, Kazi Vijana, Ajira na Watu Wenye Ulemavu, Mheshimiwa Jenista Mhagama, dada yangu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Jenista ni mama, ni mlezi. Kwa kweli ninakushukuru sana Mheshimiwa Jenista kwa upendo wako, lakini pia kwa miongozo na maelekezo ambayo umeendelea kunipatia. Kwa kweli nashindwa nitumie lugha gani rahisi kuweza kumwelezea Mheshimiwa Jenista. Amekuwa ni rafiki wa karibu, amekuwa ni dada na mama, yaani amevaa nafasi zote kwa nafasi hii ninayoitumikia katika Ofisi hii ya Waziri Mkuu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia napenda kumshukuru sana Mheshimiwa Angellah Kairuki dada yangu, kwa muda mfupi ambao nimekuwa naye katika Ofisi ya Waziri Mkuu ameendelea kunielekeza na kunipatia maelekezo ambayo yanaendelea kunisaidia katika utendaji wangu. Pia naomba nitumie nafasi hii kumshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri mwenzangu Mheshimiwa Antony Peter Mavunde kwa ushirikiano ambao ameendelea kunipatia. Ni ushirikiano mkubwa, sisi ni marafiki. Namshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri Antony Mavunde kwa ajinsi ambavyo ameendelea kunipatia ushirikiano mkubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nitumie nafasi hii kuwashukuru sana Makatibu Wakuu wote watatu kwa majina yenu, kwa sababu ya muda naomba nisiyataje kwa jinsi ambavyo mmendelea kunifanya niweze kutekeleza majukumu yangu katika Ofisi hii ya Waziri Mkuu. Vile vile nawashukuru Watendaji wote wa Ofisi ya Waziri Mkuu wakiwemo watumishi wa Kitengo cha Watu Wenye Ulemavu. Naomba niseme kwamba nawashukuru sana kwa jinsi ambavyo mnaniwezesha kutekeleza majukumu yangu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja kwa moja kwa sababu ya muda, naomba niende kwenye ufafanuzi wa hoja ambazo zimetolewa na Waheshimiwa Wabunge, pamoja na Kamati yetu ya kudumu ya masuala ya Katiba na Sheria.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa kuna hoja kwamba Serikali iweze kuimarisha kitengo kinachohudumia masuala ya watu Wenye Ulemavu. Ushauri huu wa Kamati ni ushauri mzuri na ndani ya Serikali tayari tumeshaanza kuona ni jinsi gani tunaweza tukaongeza watumishi katika kitengo kinachohudumia na kuratibu masuala ya watu wenye ulemavu. Kuongezeka kwa watumishi hawa kutawezesha usimamizi na uratibu kuweza kufanyika kama inavyotakiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, katika mwaka huu wa fedha kifungu cha Kitengo cha Watu Wenye Ulemavu kimeweza kuanzishwa ambacho ni Kifungu Na. 2034 na kupitia kifungu hiki, pia tunaona masuala mengi ya watu wenye ulemavu yataweza kufanyika vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, katika kuendelea kuimarisha Kitengo hiki cha Watu Wenye Ulemavu, Serikali tunaona kwamba iko haja ya kuwajengea uwezo watumishi wa kitengo hiki kwa sababu masuala ya watu wenye ulemavu yako mengi, lakini pia yanaibuka kila kukicha. Kwa hiyo, uko umuhimu wa kuwajengea uwezo watumishi hawa na tumekuwa pia tukifanya hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile kuna suala la Baraza la Ushauri kwa Watu Wenye Ulemavu. Baraza hili, nilihakikishie Bunge lako Tukufu kwamba litatangazwa hivi karibuni, muda siyo mrefu. Litakapokuwa limetangazwa baraza hili, basi tunaamini kwamba litatekeleza majukumu yake kwa mujibu wa sheria inavyoitaka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kulikuwa kuna hoja ya Mfuko wa Taifa kwa Watu Wenye Ulemavu. Sheria yetu inatuongoza kwamba tunatakiwa kuwa na Mfuko huu wa Taifa kwa Watu Wenye Ulemavu. Maandalizi ya Mwongozo yanaendelea kukamilika na tayari kwa mwaka wa fedha ujao 2019/2020 tumetenga fedha zipatazo shilingi milioni 103 ambazo ni mbegu kwa mfuko huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile nitoe rai kwa wadau mbalimbali kuweza kuchangia mfuko huu kwa sababu una matumizi mengi kwa kundi hili la watu wenye ulemavu. Ruzuku za Vyama vya Watu Wenye Ulemavu zinategemea mfuko huu na pia elimu na mafunzo vinategemea mfuko huu. Pia, tafiti mbalimbali ambazo zinahusiana na masuala ya watu wenye ulemavu yanategemea mfuko huu. Pia kuna masuala ya Utengemano kwa Watu Wenye Ulemavu yanategemea mfuko huu. Kwa hiyo, ni rai yangu kwamba Serikali tumeshaanza kwa kutenga hiyo fedha, basi na wadau mbalimbali waendelee kujitokeza kuchagia mfuko huo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa pia kuna hoja ya kwamba, Serikali ihakikishe kwamba inatatua migogoro mbalimbali ambayo inajitokeza kwenye Vyama vya Watu Wenye Ulemavu. Serikali imekuwa ikifanya hivyo kwa kushirikiana na Msajili wa Vyama vya Kiraia lakini pia kwa kushirikiana na Shirikisho la Vyama vya Watu Wenye Ulemavu. Ni kweli kuna migogoro ambayo imekuwa ikijitokeza na Ofisi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu mara kadhaa imeweza kuwaita wahusika wa vyama hivi na kuweza kutatua migogoro ambayo imekuwa ikiendelea. Sambamba na hilo, tumekuwa tukihakikisha kwamba chaguzi zinakuwa zinafanyika na mikutano inakuwa inafanyika kwa mujibu wa katiba na sheria ambavyo inataka ifanyike.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kitengo cha Watu Wenye Ulemavu sasa hivi kinaendelea kushughulikia kuhakikisha kwamba Mkutano Mkuu unaitishwa na Chama cha Watu wenye Ulemavu wa Viungo Tanzania (CHAWATA) na kuweza kufanya mkutano ambao imekuwa ni changamoto kubwa kwa chama hiki kwa muda mrefu. Kwa hiyo, Ofisi ya Waziri Mkuu inalishughulikia hili kwa kushirikiana na Chama cha Watu Wenye Ulemavu wa Viungo Tanzania kuona kwamba, mkutano unaitishwa na hatimaye uchaguzi ule unaweza kufanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa kuna hoja ya miundombinu ambayo inakuwa ni rafiki kwa watu wenye ulemavu. Serikali ihakikishe kwamba miundombinu inakuwa ni rafiki kwa watu wenye ulemavu. Serikali yetu inazo sheria ambazo zinaelekeza kabisa kwamba, miundombinu inatakiwa iweje ili iweze kuwa jumuishi kwa watu wote. Niendelee kutoa rai kwa mamlaka ambazo zinahusika na upitishaji wa michoro mbalimbali katika miji yetu, kuhakikisha kwamba inazingatia hii sheria, kwamba isipitishe michoro ambayo inakuwa haijaonesha ni jinsi gani miundombinu itakuwa ni rafiki kwa watu wenye ulemavu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo Serikali imeendelea kutoa elimu kwa mamlaka mbalimbali lakini pia hata kwa jamii zetu kuelekeza kwamba ni jinsi gani basi miundombinu inafaa kuwa rafiki kwa watu wenye ulemavu. Waheshimiwa Wabunge, hata nyumba ambazo tunakuwa tunajenga tuweze kuona kwamba ni jinsi gani zinakuwa ni rafiki kwa makundi yote. Mimi huwa nakuwaga na msemo kwamba; sipendi sana kusema kuwa kila mtu ni mlemavu mtarajiwa, lakini napenda kusema kila mtu ni mzee mtarajiwa. Kwani hata uzee hatuutaki, si kila mtu anapenda awe mzee, kwa hiyo kama unapenda kuwa mzee, kuna miundombinu ambayo itafika mahali haitakufaa utakapokuwa mzee. Kwa hiyo suala la miundombinu ni suala ambalo ni jukumu la kila Mtanzania kuhakikisha kwamba, miundombinu inakuwa ni rafiki kwa makundi yote. (Makofi).

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kulikuwa kuna hoja ya kwamba, Serikali iwasaidie watu wenye ulemavu wanapokuwa wanapatikanika ama wanapokuwa na kesi zao. Serikali imekuwa ikihakikisha kwamba, haki za watu wenye ulemavu zinafuatwa kwa kutumia Ofisi zetu za Ustawi wa Jamii, lakini pia niendelee kutoa rai kwa asasi mbalimbali ambazo zinashughulika na masuala mbalimbali ya kisheria, kuona kwamba ziweze kuzingatia masuala mbalimbali yanayohusiana na watu wenye ulemavu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wako wanasheria ambao wamekuwa wakijitolea katika eneo hili pia, niendelee kuwapongeza na kuwashukuru na wamekuwa wakijitangaza kwamba wanaweza wakasaidi kundi hili la watu wenye ulemavu wanapokuwa wanapatikanika na kesi. Pia sisi kama Serikali tumekuwa tukifanya hivyo mara kadhaa hata mimi mwenyewe nimeweza kuwaunganisha watu wenye ulemavu na Wizara ya Katiba na Sheria na wamekuwa wakisaidika. Kwa hiyo, ushauri huu mzuri tumeupokea na tutaendelea kuutekeleza kama ambavyo inatakiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa kuna hoja ya kusimamia na kudhibiti ile asilimia mbili ambayo inatolewa na halmashauri. Niseme kwamba, Serikali tumepokea ushauri huu mzuri, lakini pia tumeanza kuandaa kanuni kwa kushirikiana na Ofisi ya Mheshimiwa Rais, TAMISEMI kuandaa mwongozo na kanuni ambazo zitawezesha utolewaji na usimamizi wa hii asilimia mbili ambayo inatolewa na halmashauri zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa kuna hoja ama ushauri ambao ulitolewa kwamba Serikali ihakikishe inashughulikia ama kutatua changamoto mbalimbali ambazo zinahusiana na watu wenye ulemavu, kwa maana ya kwamba kuweka uratibu mzuri kwa masuala ya watu wenye ulemavu. Serikali imeendelea kufanya hivyo na kwa kuliona hilo tumeweza kuanzisha madawati katika Wizara zetu zote, pamoja na taasisi, madawati ambayo yanashughulikia masuala ya watu wenye ulemavu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali pia tumeweza kufanya warsha mbalimbali kwa sababu tunatambua kwamba, ajira imekuwa ni changamoto kubwa kwa watu wenye ulemavu. Tumeweza kuandaa warsha mbalimbali ambazo Serikali kwa kushirikiana na CCBRT, tulifanya warsha ambayo iliwahusisha waajiri na kupitia hapo tukawaomba waajiri kwamba waweze kuendelea kuwaajiri watu wenye ulemavu. Kupitia warsha ile, kuna waajiri ambao pale pale waliweza kujitolea kwamba, wataajiri watu wenye ulemavu kadhaa, pale kadhaa, pale kadhaa.

Kwa hiyo, ilikuwa ni warsha nzuri ambayo iliendelea kuwa na mafanikio. Niendelee kutoa rai kwa waajiri wote kuendelea kutenga nafasi katika ofisi zao kwa ajili ya kuajiri watu wenye ulemavu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, yako mengi ambayo yamefanywa na Serikali, lakini naona tayari nimeshagongewa kengele ya kwanza, pia sambamba na hilo tumeweza kufanya semina kwa wajasiriamali wenye ulemavu na hii ilikuwa ni kwa ajili ya kuwaonesha fursa ambazo zinapatikana ndani ya Serikali yetu sikivu ambayo inaongozwa na Mheshimiwa Rais wetu, ambaye amejipambanua kwa vitendo kuendelea kulijali na kulipenda kundi hili la watu wenye ulemavu. Semina hii pia ilikuwa na mafanikio makubwa kwa sababu wajasiriamali wale wenye ulemavu waliweza kufahamu fursa mbalimbali ambazo wanaweza wakazitumia ndani ya Serikali yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda kwenye masuala yanayohusiana na UKIMWI, kulikuwa kuna hoja ya Kamati ambayo iliweza kusema kwamba, Serikali iweze kukamilisha mwongozo wa namna ya kamati zile ambazo zilikuwa zinatumika na masuala ya UKIMWI, basi ziweze kushughulikia masuala ya dawa za kulevya. Serikali yetu imepokea ushauri huo na tayari Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya imekwishakasimu mamlaka ama shughuli za kupambana na dawa za kulevya kwa hizi Kamati za UKIMWI kwenye mamlaka za Serikali za Mitaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile kulikuwa kuna hoja ya kwamba, Serikali iweze kuona umuhimu wa kutenga fedha zake za ndani za maendeleo angalau asilimia 75, kwa ajili ya masuala ya UKIMWI kutekeleza hizi afua za UKIMWI.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme kwamba ushauri huu mzuri pia umepokelewa na tayari Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na UKIMWI imeandaa mkakati wa jinsi gani itaweza kukusanya fedha na pia umeweza kuonesha ama kuainisha vyanzo vya mapato vya ukusanyaji wa fedha hizo. Tunaamini kwamba kupitia mkakati huu, tutaweza kuondokana na utegemezi wa kutegemea ufadhili kutoka nje na hasa tukizingatia kwamba, Mheshimiwa Rais wetu ni Rais ambaye anapenda sisi kama Taifa tuweze kujitegemea kwa mapato ama kwa fedha zetu ambazo tunazipata ndani ya nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa kuna hoja ya Kamati kwamba Serikali iweze kuanzisha chanzo maalum ama mahususi ambacho kitawezesha kutunisha fedha ya Mfuko wa UKIMWI. Hii walipendekeza kwamba, iwe ni tozo labda kutoka kwenye maji na vitu kama hivyo. Ushauri huu pia ni mzuri sana na utawezesha kiukweli kwamba tutaweza kuendelea kujitegemea. Serikali imepokea ushauri huu na inaendelea kuufanyia kazi kuona ni jinsi gani tunaweza tukaanzisha tozo hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa pia kuna hoja ya kwamba Serikali iweze kubuni uwekezaji katika kutekeleza afua za UKIMWI kwa kushirikiana na sekta binafsi. Hoja hii pia ni nzuri na imepokelewa, lakini pia niweze kuliarifu Bunge lako Tukufu kwamba Bodi ya Mfuko wa Udhamini wa UKIMWI tayari ipo katika hatua za mwisho za kuajiri mtaalam ambaye atasaidia katika upatikanaji ama ni jinsi gani sasa fedha zipatikane. Sambamba na jukumu hilo, atafanya na jukumu hili la kuhakikisha kwamba basi, hizi sekta binafsi zinaweza kushirikishwa na hatimaye kuweza kufikia lengo ambalo limetarajiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kulikuwa kuna hoja ya kwamba Serikali kwa ku… (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa.

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU (WENYE ULEMAVU): Mheshimiwa Mwenyekiti baada ya kusema haya, nami naomba niunge mkono hoja ya Ofisi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu. (Makofi)