Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Dr. Hamisi Andrea Kigwangalla

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nzega Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu

WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu pamoja na Mawaziri; Mheshimiwa Jenista Joakim Mhagama na Mheshimiwa Angella Jasmine Kairuki, Naibu Mawaziri pamoja na Watendaji wote wa Ofisi hii ya Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kupongeza hotuba nzuri iliyotolewa na Mheshimiwa Waziri Mkuu, naomba kutoa ufafanuzi kwenye maeneo machache ambayo Waheshimiwa Wabunge waligusia katika sekta ya maliasili na utalii na kwa kuwa muda hautoshi naomba nijibu bila kuwatambua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la kwanza ni eneo la migogoro ya ardhi. Msimamo wa Serikali kwa sasa kwa migogoro yote ya mipaka, matumizi maeneo ya hifadhi ambayo yapo chini ya Wizara ya Maliasili na Utalii tupo katika Kamati ambapo Januari 15 mwaka huu Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliunda Kamati ya Mawaziri kutokana Wizara nane ambao wamepita maeneo yenye migogoro, wamechambua taarifa mbalimbali na sasa tuko katika hatua za mwisho za kuandaa ushauri ambao tutaufikisha kwa Mheshimiwa Rais. Pindi atakapotoa maagizo yake tutarudi kinyumenyume kurekebisha mipaka accordingly ili kutatua migogoro hiyo na huo ndio mtazamo wetu. Kuna maeneo yamezungumziwa ya Kilombero, Serengeti, Grumet, kuna pembeni ya Mto Rubana, yote kwa ujumla wake jibu letu ni hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo ningependa kuzungumzia ni kukuza utalii wa fukwe. Limezungumziwa jambo hili kwa kiasi kikubwa; Mheshimiwa Mbaraka Dau na wengine, naomba niwahakikishie kwamba Serikali ya Awamu ya Tano kwa sasa imejipanga ipasavyo kukuza utalii wa fukwe na tutaanza kwa kuwekeza katika maeneo ya Ziwa Victoria, eneo la Chato, lakini pia fukwe za Bahari ya Hindi eneo la Saadan likihusianisha visiwa vilivyopo katikati ya Bahari ya Hindi, lakini pia kisiwa cha Mafia. Mafia kuna vivutio vya pekee kuna whale sharks ambacho ni kivutio cha Kimataifa na watalii ambao ni high end wanapenda kuogelea pamoja na hao papa nyangumi ambao wanapatikana sehemu mbili tu duniani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunapaangalia Mafia kwa jicho la kipekee na tunakusudia kuweka mkakati mahususi sambamba na kujenga maeneo ya vivutio vya fukwe, vivutio vya mikutano yaani kwa ajili ya kuendeleza conventions tourism lakini vivutio vya michezo kwa maana kuendeleza sports tourism. Michezo tunayoingalia kwa sana ni michezo kama ya gofu, tennis, michezo ya baiskeli ya kimataifa ambayo tunaamini kwa pamoja itakuza sana utalii wa fukwe ukilinganisha na utalii wa mikutano.

Sambamba na hilo tumetengeneza maeneo matatu ya kukuza utalii, hivyo kama nilivyosema eneo la Chato ambapo hifadhi za Taifa ambazo Bunge hili Tukufu katika Mkutano uliopita wa Bunge lilipandisha hadhi hifadhi za Burigi, Biharamulo na Kimisi pamoja na nyingine, eneo lile tunakushudia kuendeleza utalii wa fukwe pamoja na utalii wa mikutano. Eneo lingine ni hili la Saadan, pamoja na ufukwe wote Bagamoyo, Pangani mpaka Tanga na ukiunganisha na hivyo visiwa nilivyovitaja. Eneo lingine ni hili la Kilwa tukiunganisha Kilwa Kisiwani pamoja na ufukwe wote kuanzia Kilwa mpaka Mtwara. Kwa hivyo eneo la utalii wa fukwe kwenye bajeti yetu tutakayoisoma hapa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Waziri kwa mchango wako.

WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.