Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Othman Omar Haji

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Gando

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. OTHMAN OMAR HAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu kusifia maendeleo mazuri ya demokrasia hapa nchini lakini ripoti iliyotolewa na Shirika Huru la Freedom House tarehe 10 Februari 2019 inaeleza kwamba Tanzania inashindana na maeneo yenye hatari kisiasa duniani. Hii ni kutokana na kukamata viongozi wa upinzani, kuzuia maandamano dhidi ya Serikali, kuzuia mikutano ya vyama vya upinzani na sheria ya kuimarisha chama tawala na kuminya vyama vya upinzani. Ripoti ya Freedom House inaendelea kueleza kwamba Tanzania ni miongoni mwa nchi 10 duniani ambazo zilipata maendeleo ambayo yameathiri mwelekeo wake wa kidemokrasia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na Serikali kuridhika na hamasa za Watanzania katika uwekezaji wa ujenzi wa viwanda page 33, lakini ripoti ya taasisi ya Quantum Global Research Lab ya Machi 2018 juu ya uwekezaji Barani Afrika inaeleza kwamba Tanzania huenda isifikie lengo lake la kujenga uchumi wa viwanda. Hii inatokana na mabadiliko ya sera za usimamizi wa fedha na rasilimali ambazo siyo rafiki kwa wawekezaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, utafiti huu ulihusisha nchi 54 za Afrika ambapo Tanzania ilishika nafasi ya 13 mwaka 2018 kutoka nafasi ya nane mwaka 2017 kwa nchi zenye mazingira mazuri ya uwekezaji. Mabadiliko ya sera za fedha na mazingira magumu ya kuanzisha na kufanya biashara ambayo yanaathiriwa na ongezeko la kodi na upatikanaji wa leseni za biashara ni sababu za mkwamo wa ukuaji wa sekta binafsi na uchumi wa viwanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa Benki ya Dunia (WB) urahisi wa kuanzisha biashara Tanzania uko chini ya wastani unaotakiwa na nchi za Kusini mwa Jangwa la Sahara. Naiomba Serikali kujitahidi kuweka mazingira mazuri ya kuvutia wawekezaji ili iweze kufikia malengo yake ya kufikia uchumi wa kati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vijana wa Kitanzania wamekata tamaa kutokana na tatizo la ajira linalowakabili. Kati ya mwaka 2015 hadi Desemba 2018 jumla ya vijana 594,300 walimaliza vyuoni kati ya hao ni vijana 6,554 sawa na asilimia 1.1 ndiyo waliopata ajira. Hali hii inaonesha kushindwa kwa Serikali ya Awamu ya Tano katika kuwahudumia vijana wa Kitanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo la vijana kukosa ajira baada ya kumaliza masomo yao kunaweza kusababisha madhara ya afya zao. Hivi karibuni Shirika la Afya Duniani (WHO) lilisema karibu vijana milioni 3.7 wanaugua ugonjwa wa sonona (depression) kutokana na ukosefu wa ajira. Niombe Serikali kuhakikisha vijana wanapomaliza masomo yao wanapatiwa ajira ili kuwaepusha na ugonjwa huo wa sonona.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sekta binafsi zinapunguza kasi ya kuajiri na inapunguza wafanyakazi kutokana na mazingira yasio rafiki kwao. Hivyo basi ni jukumu la Serikali kukabiliana na changamoto za ajira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuwasilisha.