Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Prof. Joyce Lazaro Ndalichako

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Kasulu Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu

WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti nashukuru kwa kunipatia nafasi ya kuchangia hoja iliyopo mbele yetu. Ningependa kuanza kwanza kabisa kwa kusema naunga mkono hoja hii na napenda kuipongeza Ofisi ya Waziri Mkuu kwa kazi kubwa ambayo wanafanya katika kuratibu shughuli za Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa kuchangia katika maeneo machache. Kwanza kuna suala la mafunzo ya ufundi stadi ambalo limeongelewa na Waheshimiwa Wabunge wameonesha dhamira au nia ya kuona elimu ya mafunzo ya ufundi stadi inaendelea kuimarishwa katika maeneo yao. Niseme tu kuwa Serikali imeendelea kuhakikisha kwamba inaongeza fursa na nafasi za mafunzo ya ufundi stadi na kama ambavyo wiki iliyopita tulikuwa na Mheshimiwa Rais kule Namtumbo tunazindua Chuo cha Mafunzo ya Ufundi Stadi Namtumbo. Pia kuna chuo vingine vya ufundi stadi ambavyo tunaendelea na ujenzi katika maeneo mbalimbali ikiwemo Wilaya ya Ileje, Chato.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile tunaendelea na ujenzi wa VETA za Mikoa; Mkoa wa Kagera, Simiyu, Mkoa wa Njombe pamoja na Mkoa wa Geita. Pia Serikali imefanya ukarabati wa Vyuo vya Maendeleo ya Wananchi (FDCs) na mpaka sasa tumeshafikia vyuo 20 kati 34 na katika bajeti ya mwaka huu ambapo naamini Waheshimiwa Wabunge wataiunga mkono, tunategemea kufikia vyuo 34 vilivyobaki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo limezungumziwa ni suala la udhibiti ubora wa shule. Ningependa kulihakikishia Bunge lako Tukufu kwamba Serikali iko makini sana katika suala la udhibiti ubora kwa sababu tunaamini kwamba Wadhibiti Ubora wa Shule ndio jicho la Serikali katika kutuhakikishia kwamba tunafikia malengo yetu katika sekta ya elimu. Kwa hiyo Serikali inaendelea kuiangalia idara hiyo kwa makini zaidi na vile vile tumeendelea kuiimarisha katika kuhakikisha kwamba inapata vitendea kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka wa fedha uliopita, Serikali ilitoa magari 45 kwa ajili ya ofisi mbalimbali za udhibiti ubora wa shule, lakini tumeendelea kuiimarisha katika vitendea kazi kama kompyuta. Pia tumeangalia namna Wadhibiti Ubora wanavyofanya kazi kwa sababu zamani Wadhibiti Ubora walikuwa wamekaa kipolisi polisi zaidi. Wanaenda kuwatisha Walimu badala ya kwenda kuwapa support yaani kwa maana kwamba kuwaonesha upungufu wao na kufanya kazi. Tumebadilisha mfumo na tumetengeneza kiuzi cha udhibiti ubora ambacho lengo ni kwenda kuboresha mifumo ambayo inajitokeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile limezungumziwa suala la vifaa vya kufundisha hasa katika shule za sekondari. Serikali ya Awamu ya Tano imefanya kazi kubwa kuhakikisha kwamba maabara ambazo zilikuwa zimeanzishwa na wananchi zinapata vifaa. Kwa hiyo jumla ya shule za sekondari 1,696 zimeweza kupata vifaa vya kufundishia masomo ya sayansi ambayo yapo kwenye muhtasari kuanzia kidato cha kwanza mpaka kidato cha sita, ni vifaa ambavyo vinajitosheleza. Niendelee kuwahakikishia Wabunge kwamba kwenye sekta ya elimu na hasa kwenye masuala ya Mafunzo ya Ufundi stadi ambayo tunafanya na Ofisi ya Waziri Mkuu, tunakwenda vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho, ningependa kuzungumzia suala la elimu maalum ambalo pia nalo tunalifanya kwa kushirikiana na Ofisi ya Waziri Mkuu. Serikali itaendelea kuhakikisha kwamba wanafunzi wenye mahitaji maalum wanaendelea kupata elimu yao katika mazingira rafiki zaidi. Kwa hiyo, tuna progamu ya kusambaza vifaa na visaidizi kwa ajili ya watoto wenye mahitaji maalum na tutaendelea kufanya hivyo kwa sababu tunaamini kwamba elimu ni haki ya kila mtoto na hata yule ambaye ana changamoto anastahili kupata elimu katika mazingira mazuri.