Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Augustino Manyanda Masele

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbogwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. AUGUSTINO M. MASELE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nichukue fursa hii kukupongeza kwa kunipatia nafasi ili niweze kuchangia hotuba nzuri ya Waziri wetu Mkuu, Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa. Hotuba yake inaweka msingi wa bajeti ya Serikali itakayojadiliwa hapa Bungeni kwa kipindi cha miezi mitatu kamili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijaendelea mbele, naomba niunge mkono hoja hotuba ya Waziri wetu Mkuu kwa asilimia mia moja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waziri Mkuu wetu alifanya ziara katika Mkoa wetu wa Geita na alifika pia katika Wilaya yetu ya Mbogwe akikagua miradi mbalimbali ya maendeleo ambayo imetekelezwa na Serikali yetu ya Awamu ya Tano. Niseme tu kwamba Serikali yetu ya Awamu ya Tano imejipambanua kuwa ni Serikali ya viwanda; na pia inaendena na kauli mbiu ya Chama chetu cha Mapinduzi inayosema ya kwamba, “Tanzania mpya na CCM mpya na CCM mpya ni Tanzania mpya.” Kwa sababu mambo mengi ambayo yanatendwa na Serikali hii yanatia moyo na yanaonyesha kwamba kweli tunakokwenda ni Tanzania mpya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ipo miradi mbalimbali ambayo inatekelezwa na Serikali yetu ya Awamu ya Tano, zipo sekta mbalimbali muhimu ambazo Serikali yetu imezitilia mkazo ikiwemo sekta ya elimu. Sekta ya Elimu ni sekta nyeti na Serikali yetu imeweka msimamo mzuri wa kuweka elimu bila malipo kuanzia darasa la kwanza mpaka kidato cha nne. Hongera sana Serikali ya Chama cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikija katika Sekta ya Afya, sisi sote ni mashahidi ya kwamba Serikali yetu imejenga Vituo vya Afya vingi katika sehemu mbalimbali za nchi hii ikiwemo katika Wilaya yangu ya Mbogwe. Tumepewa vituo vya Afya viwili; Kituo cha Afya cha Iboya na Kituo cha Afya cha Masumbwe. Vituo hivi vyote kwa pamoja vimepewa jumla ya shilingi milioni 800 na kwa kweli utekelezaji wake kwa kutumia ile force account, tumeweza kuyaona manufaa ambayo yamepatikana baada ya kuwa tumepata majengo mazuri. Ukifika kwenye Kituo cha Afya utajua kabisa kwamba kwa kweli mgonjwa akifika hapo hata kama alikuwa na hali mbaya anarejeshewa matumaini ya kuishi tena.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niipongeze Serikali yetu ya Chama cha Mapinduzi kwa kututengea awamu hi shilingi milioni 500 za kuanza ujenzi wa hospitali yetu ya Wilaya ya Mbogwe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mambo mengi yanaendelea kufanyika katika Wilaya yetu ya Mbogwe ikiwemo ujenzi wa Makao Makuu ya Halmashauri yetu. Tuipongeze kabisa Serikali kwa sababu hatua za ujenzi zinaendela vizuri, miradi mbalimbali ya maji pia inaendelea kufanyika. Upo upanuzi wa mradi wa maji wa Nyakafuru, upo mradi wa Mbogwe, upo mradi wa Uhala katika Kata ya Lugunga. Yote haya wana Mbogwe tunasema ahsante sana kwa Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nije katika suala zima la ujenzi wa reli ya standard gauge. Ujenzi huu ni hatua ya maendeleo ya hali ya juu sana. Nchi yeu tumeshuhudia Serikali ikitekeleza mradi huu kuanzia Dodoma mpaka kule Dar es Salaam, ujenzi unaendelea vizuri. Tunayo matumaini makubwa kwamba ujenzi huu utaendelea mpaka kufika Kigoma na Mwanza na hata ile reli ya kutoka Isaka kwenda Kigali tunaamini Serikali yetu kwa kushirikiana na wenzetu wa Rwanda tutaishuhudia ikitekelezwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa maslahi mapana ya kulinda muda, niipongeze sana Serikali kwa ujasiri wake mkubwa wa kuanza na kuendelea kujenga mradi wa uzalishaji umeme wa maji katika mto Rufiji maarufu kama Stiegler’s gauge. Sisi sote ni mashahidi ya kwamba hapa zitapatikana Megawatts 2100 ambazo aitaingizwa katika gridi ya Taifa. Ninaamini ya kwamba, Tanzania ya viwanda bila ya umeme isingewezekana lakini kwa kufuatana na juhudi mahususi za Serikali jambo hili limetiliwa mkazo na ninaamini ya kwamba itakapofika mwaka 2020 tutakuwa na uwezo mkubwa wa kuweza kui-supply Tanzania umeme vijiji vyote na vitongoji vyote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninyi wote Waheshimiwa Wabunge mtakuwa ni mashahidi wa namna ambavyo Wakandarasi mbalimbali wameendelea kutekeleza miradi ya usambazaji wa umeme vijijini kupitia Wakala wa Umeme Vijijini (REA). Jambo hili linafanyika katika maeneo mbalimbali ikiwemo katika Wilaya yangu ya Mbogwe. Naiomba tu Wizara ya Nishati iendelee kumsukuma Mkandarasi ili aweze kumaliza mradi huu wa awamu ya tatu ya REA ili kwamba Watanzania wengi wa Mbogwe waweze kupata huduma hii muhimu ya umeme.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nije katika sekta ya barabara. Serikali yetu ya Awamu ya Tano pamoja na Awamu ya Nne wagombea wake waliwahi kuahidi ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami katika Mji wangu wa Masumbwe, tuliahidiwa kupatiwa lami kilometa tatu. Kwa maana hiyo, naishaurri tu Serikali katika bajeti yake ya mwaka huu ikumbuke kuzitimiza hizi ahadi za viongozi wetu wakuu wa Serikali katika maeneo mbalimbali ambako tunaamini ahadi hizi ziliwekwa na nitilie tu mkazo ujenzi wa barabara…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Masele kwa mchango wako.

MHE. AUGUSTINO M. MASELE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga hoja mkono kwa asilimia mia kwa mia. (Makofi)