Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Shabani Omari Shekilindi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lushoto

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. SHAABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa nafasi hii ili niweze kuchangia hotuba ya Mheshimiwa Waziri ambayo ndiyo iko mbele yetu. Kwanza kabisa, nimpongeze Mheshimiwa Waziri Mkuu pamoja na timu yake, Mheshimiwa Jenista pamoja na Mheshimiwa Mheshimiwa Kairuki kwa kazi kubwa wanayoifanya, hakika mwenye macho haambawi tazama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja kwa moja niende kwenye suala zima la afya. Kwanza niendelee kuipongeza Serikali yangu inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa kazi kubwa wanayoifanya kwani hivi karibuni tumeshuhudia karibia Hospitali za Wilaya 67 zimekarabatiwa. Sambamba na hayo, Hospitali yangu ya Wilaya ya Lushoto sijaiona na hospitali ile ni kongwe, ni ya zamani sana. Hospitali ile inachukua karibia Wilaya tatu ambazo zimezunguka pale, naamini inahudumia takribani watu 500,000. Niiombe sasa Serikali yangu Tukufu watakapokuja ku-windup basi waingize hospitali hii iweze kukarabatiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo, kama nilivyokwishasema hospitali hii ni kongwe lakini pamoja na ukongwe wake majengo pia ni ya zamani sana, hayaendi na wakati, inapitwa mpaka na kituo cha afya. Kwa hiyo, niiombe Serikali yangu Tukufu sasa itengee fedha kwa ajili ya Hospitali hii ya Wilaya ya Lushoto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia hospitali hii haina X-Ray kwa muda mrefu, sasa hivi ni takribani miezi sita. Hata Mheshimiwa Waziri Mkuu ni shahidi wakati anakuja Lushoto nilimlalamikia kuhusu X-Ray hii. Kwa hiyo, niiombe sasa Serikali yangu Tukufu iweze kupeleka X-Ray ile wananchi wangu waweze kupata huduma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna vituo vya afya ambavyo vinaendelea kujengwa. Niishukuru Serikali yangu Tukufu inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwani tumepewa Kituo cha Afya kimoja cha Mlola, tumepewa takribani shilingi milioni 700; shilingi milioni 400 kwa ajili ya majengo na shilingi milioni 300 kwa ajili ya vifaa tiba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nguvu za wananchi tumeshajenga vituo vya afya viwili ambavyo viko hatua tofauti tofauti. Kituo cha Afya Gare tayari kina maboma zaidi ya matatu na vyumba zaidi ya 20. Kama ilivyoahidi au kama ilivyo ada wananchi wanapojenga maboma yale basi Serikali inamalizia maboma yale, kwa hiyo, niiombe Serikali yangu Tukufu ipeleke fedha tuweze kumalizia maboma yale na wananchi wa Gare na wa Lushoto kwa ujumla waweze kupata huduma hiyo na kupunguza msongamano ambao upo katika Hospitali ya Wilaya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna Kituo cha Afya Ngwelo tunaanza kukijenga na kiko hatua ya lenta kwenye OPD. Kwa hiyo, niiombe pia Serikali yangu Tukufu kwamba ipeleke fedha pale tuweze kukamilisha kituo kile cha afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna zahanati kama Ilani yetu ya Chama cha Mapinduzi inavyosema kwamba kila kijiji kitajengwa zahanati. Wananchi wa Lushoto kwa nguvu zao wamejenga zaidi ya zahanati 12. Zahanati sita ziko tayari zinahitaji vifaatiba na watumishi, zahanati sita ziko kwenye lenta. Kwa hiyo, niombe Serikali yangu kama ilivyoahidi au kama Ilani ya Chama cha Mapinduzi inavyosema kwamba mnapofikisha kwenye mitambaa ya panya basi Serikali itachukua. Niombe sasa Serikali iwaunge mkono wananchi wa Jimbo la Lushoto ili waweze kumalizia zahanati zile ambazo zimebaki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye suala la TARURA. Kwa kweli TARURA ni watu wazuri sana na wanafanya kazi kubwa sana ambayo kwa kweli inafaa kuigwa lakini haina fedha za kutosha. Kama unavyofahamu Lushoto ni ya wakulima wa mbogamboga na matunda na kahawa lakini wanapata hasara kubwa sana hususan mvua zinaponyesha mazao yao huwa yanaozea shambani kwa sababu ya kukosa miundombinu ya barabara. Niiombe Serikali yangu Tukufu iangalie namna ya kuiwezesha TARURA waweze kupata fedha nyingi ili waweze kutengeza barabara zile za Lushoto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna barabara ambazo ni critical issue, mfano barabara ya kutoka Mlalo – Ngwelo – Mlola – Makanya - Milingano – Mashewa. Barabara hii ni ya kiuchumi na kila siku, kila mwaka na kila wakati naisemea lakini mpaka leo haijatengezwa. Kwa hiyo, niombe Serikali yangu Tukufu kwamba barabara ichukuliwe na TANROADS kwa sababu inaunganisha wilaya hadi wilaya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Lushoto kuna barabara moja kuu tu ambayo inatoka Mombo - Soni – Lushoto, kwa hiyo, Wilaya nzima ya Lushoto barabara ya kuingia Wilayani ni moja tu. Kuna barabara moja ya mchepuko ambayo inatoka Dochi - Ngulwi - Mombo, hii ni barabara muhimu sana na kwa kweli itaenda kutatua kilio cha wananchi wa Lushoto kwa sababu ni njia fupi, ni kilometa 16 tofauti na barabara ya kutoka Mombo - Soni - Lushoto ambayo ni kilometa 32, ni nusu ya barabara hiyo. Niiombe Serikali kutenga fedha ili barabara ile iweze kutengenezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, twende kwenye suala zima la umeme, kwa kweli tumekuwa tunajibu maswali magumu sana ambapo na sisi tunashindwa kuyajibu. Niiombe sasa Serikali yangu Tukufu, dada yangu Mheshimiwa Subira Mgalu na Mheshimiwa Medard ameshafika Lushoto na ameona hali halisi ilivyo, ameona jinsi wananchi wa Lushoto wanavyopenda umeme na anajua kabisa Lushoto hakuna nyumba ya nyasi hata moja na wananchi wa Lushoto tayari wameshafanya wiring kabla hata hawajatangaziwa mambo ya umeme. Kwa hiyo, niiombe sasa Serikali ipeleke umeme kwa wananchi wangu wa Lushoto. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, twende kwenye suala la kilimo, Lushoto kuna zao moja la kahawa ambalo hata wadau wa mkutano juzi walikaa pale LAPF wakasema kahawa ya Lushoto ni bora kuliko kahawa ya sehemu nyingine. Kwa hiyo, niombe sasa Serikali yangu ipeleke pembejeo na miche kwa ajili ya kupanda kahawa katika milima ile ya Usambara ili tuweze kupata kahawa bora tuweze kuimarisha kilimo chetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla ya kumalizia niongelee uwekezaji. Hebu tuangalie ni namna gani ya kuondoa changamoto zinazowakwaza wawekezaji wetu. Mheshimiwa Kairuki naamini ni jembe, unafanya kazi iliyotukuka, kuna Kiwanda cha Sementi kule Mkinga, mwekezaji yule anaweka shilingi trilioni 7.7 lakini leo hii ni mwaka wa tatu hajafanikiwa. Naomba Mheshimiwa Kairuki kwa sababu Wizara hii umeshakabidhiwa naomba kabisa uanze na hili tuhakikishe mwekezaji anafungua kiwanda kile. Kiwanda kikishashafunguliwa inamaana wananchi watapa ajira, uchumi wa Taifa utakua na mambo mengine yataenda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe Serikali yangu Tukufu Uwanja wa Ndege Tanga sasa upanuliwe ukizingatia sasa hivi tuna bomba la mafuta kutoka Hoima Uganda. Tanga sasa inaku,a tunaongeza kina cha bahari, ina maana wawekezaji na wanachi wengi watakuja kwa ajili ya fursa zilizopo Tanga. Kwa hiyo, niombe Serikali yangu Tukufu iweze…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Shekilindi.

MHE. SHAABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. (Makofi)