Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Shamsi Vuai Nahodha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nominated

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. SHAMSI VUAI NAHODHA: Mheshimiwa Spika, kwanza nakushukuru sana kwa kunipa fursa hii ya kuchangia bajeti ya Ofisi ya Waziri Mkuu. Kwanza, napenda kusema naunga mkono hoja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimefanya utafiti wa muda mrefu hivi na nikafanya utafiti wa viongozi wa tatu wa Asia na nikabaini viongozi hawa kuna mambo manne makubwa wameyafanya katika nchi zao halafu baadaye nitalinganisha na kile ambacho kwa mawazo yangu nakiona kinafanyika katika nchi yetu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Viongozi wenyewe ni marehemu Lee Kuan Yew wa Singapore; wa pili ni Mahathir Mohamed wa Malaysia sasa hivi ana awamu pili lakini nitazungumzia awamu ya kwanza; na kiongozi wa tatu anaitwa Deng Xiaoping aliyekuwa Rais wa Taifa la China kuanzia mwaka wa 1978.

Mheshimiwa Spika, yapo mambo manne wameyafanya, la kwanza, hawa viongozi wote niliowataja watatu ni viongozi ambao wana maono na mipango ya muda mrefu. Pili, sifa yao kubwa ni viongozi wa matendo, wanachokisema ndicho wanachokitenda. Tatu, wanapoteua viongozi na watendaji wanateua wenye uweledi, maarifa, ujuzi, na uzoefu. Jambo la nne ambalo walilifanya viongozi hao ni kuwekeza kwenye sayansi na teknolojia.

Mheshimiwa Spika, nikija hapa kwenye nchi yetu kwa nachokiona kwa mawazo yangu kile anachokifanya Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kinafanana sana kwa asilimia mia moja na hiki ambacho kinafanywa na viongozi hawa watatu niliowataja. Kwa maana hiyo basi Taifa letu la Tanzania katika kipindi cha miaka mitano na miaka kumi inayokuja Tanzania itakuwa miongoni mwa mataifa yenye ustawi mkubwa sana wa maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, moja ya hotuba za Rais Magufuli aliwahi kutuambia kwamba anasikitishwa sana kuona Tanzania bado inaendelea kuwa Taifa ambalo linatembeza bakuli na Taifa ambalo yeye anaamini lina uwezo sana wa kuwa Taifa linalotoa misaada. Mimi bila shaka nakubaliana naye kwamba Tanzania ina uwezo mkubwa sana tukifanya kazi kwa bidii na chini ya uongozi wake bila shaka katika kipindi kijacho si kirefu sana Tanzania itaweza kufikia katika ndoto hiyo. Hata kama hatukufikia Taifa ambalo linaweza likatoa misaada lakini bila shaka ni Taifa ambalo tutaweza kujitosheleza kwa asilimia mia moja kwa bajeti yetu, ninaamini hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nirudi kwenye yale mambo manne niliyoyaeleza pale mwanzo. La kwanza, Rais wetu Magufuli ni mtu ambaye ana maono, ana mipango ya muda mrefu ya kuliendeleza Taifa hili. Kama kuna jambo ambalo linawafanya Waafrika wadharauliwe duniani, Wazungu wanasema Waafrika kwa kawaida yao wakipanga mipango yao wanapanga mipango ya muda mfupi, pengine miaka miwili na wamekwenda mbali sana miaka mitano lakini tunachokiona Tanzania sasa hivi, tuna mradi huu wa reli ya kisasa ni mradi ambao ukikamilika utadumu kwa takribani miaka mia moja mpaka mia moja na hamsini kama tutaitunza vizuri. Bila shaka inatuonyesha dhahiri kwamba huyu ni kiongozi ambaye ana maono ya muda mrefu. Mradi mwingine ni mradi wa umeme wa Bonde la Mto Rufiji. Mradi huu utakapomalizika bila shaka tukiutunza vizuri utadumu kati ya miaka hamsini mpaka sabini. Kwa hiyo, tunaona bila shaka ni kiongozi wa namna gani, ni kiongozi ambaye ana maono na mipango ya muda mrefu. (Makofi)

Kwa hiyo, tunaona bila shaka ni kiongozi wa namna gani. Ni kiongozi ambaye ana maono na mipango ya muda mrefu. La pili, nimewahi kusikia mahali watu wakilala wanasema ah, Rais Magufuli bwana, anateua Maprofesa, Madaktari; sasa najiuliza, tulitegemea amteue nani? Kiongozi aliye makini, ana ajenda na anajua kwamba kipindi chake cha Urais ni miaka 10, bila shaka unapaswa kuteua watu unaoamini wana uwezo, weledi na maarifa ili wakusaidie kuikamilisha hiyo kazi katika kipindi kifupi. Maana yake miaka 10 katika uhai wa binadamu ni muda mchache sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sina maana kwamba watu wasio na Shahada za Udaktari wa Maprofesa hawana uwezo, la hasha! Sina maana hiyo. Wapo baadhi ya watu elimu yao ni ndogo sana Mwenyezi Mungu kawajaalia kuwa na uwezo huo na maarifa, bila shaka wakipewa nafasi hizo sina matatizo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la tatu ambalo nataka kulisema ni la Sayansi na Teknolojia. Bila shaka Rais Magufuli amejitahidi sana katika Sekta ya Afya. Tumewekeza sana katika sekta hii ya tiba. Ni mategemeo yangu kwamba katika Sekta ya Kilimo, kile ambacho tunakiona kinafanyika katika Sekta ya Afya, ningetamani sana nikione kinafanyika katika Sekta ya Kilimo kwa sababu mapinduzi ya kweli ya Taifa la Tanzania linategemea sana katika Sekta hii ya Kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, najua Serikali inao Mpango wake wa Maendeleo wa Awamu ya Pili lakini nadhani fedha zilizotengwa siyo haba, lakini kama tunataka kupiga hatua kubwa sana ya maendeleo na hasa kutimiza ndoto yetu ya Tanzania ya Viwanda; na ikiwa kilimo ni sehemu kubwa sana ya maendeleo ya viwanda, naiomba sana Serikali yangu Tukufu ifanye kila linalowezekana tuwekeze sana katika Sekta hii ya Kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwaka 1966 aliyekuwa Waziri Mkuu wa Malaysia aliwahi kusema maneno haya; aliwahi kutembelea Nigeria na Ghana mwaka huo, akasema kwa kile alichokiona Afrika, angepata nafasi ya kuwa mshauri, wa Marais wa Afrika, angewashauri wawekeze kwenye Sekta ya Kilimo. Kwa sababu kilimo ni viwanda na viwanda ni kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tukiwekeza kwenye kilimo, tutapata asilimia 100 ya mahitaji yote tunayohitaji ya kwenye viwanda, tutajitosheleza kwa chakula kwa asilimia 100. Wanasema katika kipindi cha miaka 10 na 20 inayokuja, dunia itakuwa na upungufu mkubwa sana wa chakula. Bila shaka tukiwekeza kwenye kilimo, Tanzania itakuwa ni Taifa la kupigiwa mfano sana. Naishauri sana Serikali yangu Tukufu na Waziri wa Fedha ananisikia, tujinyime tufanye kila linalowezekana hatutakosa kitu tukiwekeza kwenye kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, naomba nirudie tu, nasema kwa kile ninachokiona kinafanywa na Rais Dkt. Magufuli, Tanzania inaweza kuwa moja ya Mataifa ya kupigiwa mfano, siyo katika Bara la Afrika, lakini katika Dunia kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja. (Makofi)