Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018

Hon. Mwita Mwikwabe Waitara

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tarime Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. MWITA M. WAITARA): Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Kwanza naunga mkono hoja za Kamati zote tatu kama zilivyotolewa. Pia nitajairibu kupitia baadhi ya maeneo machache.

Mheshimiwa Spika, la kwanza, nitoe tu taarifa kwamba kwa sababu mambo yamezungumzwa mengi upande wa elimu, niliarifu Bunge letu kwamba Serikali inapeleka fedha nyingi sana katika kuboresha elimu. Tunachoomba Waheshimiwa Wabunge na Watanzania wote na hasa Watumishi wa Umma ni kuhakikisha kila shilingi inapopelekwa, inasimamiwa vizuri ili tuangalie value for money. Hilo ni jambo la msingi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa mfano, ninapozungumza, hii elimu msingi bila malipo, mpaka ninapozungumza hapa, mpaka Desemba, 2018, Serikali ya Awamu ya Tano ya Chama cha Mapinduzi imeshapeleka shilingi bilioni 634,189 ambazo zimeenda kwenye Elimu Msingi bila malipo. Hizo zinakwenda kwenye posho ya madaraka, Maafisa Elimu wale wa Kata, Wakuu wa Shule, motisha na vinginenvyo.

Mheshimiwa Spika, kwenye hoja mbalimbali, imejitokeza hapa hoja ya majengo ambayo yamesimamiwa kwenye ukarabati wa shule kongwe na TBA. Ni kweli, hoja hii ilijitokeza kwenye Kamati ya TAMISEMI ambayo nami nilikuwepo na Mheshimiwa Waziri, Ofisi ya TAMISEMI imeshalipokea hili, inalifanyia kazi, tutapitia mikataba ile na kuchukua hatua maeneo ambayo wameshindwa kufanya kazi vizuri.

Mheshimiwa Spika, ziko shule nyingi kama Ihungo, Kigoma Sekondari, Songea Wasichana, Mirambo, Nangwa, Tosamaganga, Malangaze na nyingine ambazo mpaka leo hazijakamilika. Waheshimiwa Wabunge na Kamati ya TAMISEMI naomba niseme kwamba hili jambo linafanyiwa kazi.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili, ni elimu ya msingi bila malipo, zimejitokeza hoja hapa na michango mbalimbali; Mheshimiwa Waziri wa Elimu yupo anaweza akatoa ufafanuzi zaidi, lakini tunao Waraka hapa Na.3 wa mwaka 2016 ambao unaonesha zoezi la kuimarisha elimu Tanzania ni zoezi shirikishi, ziko kazi ambazo zinafanywa na Serikali na fedha zinapelekwa kama zilivyotajwa, ziko kazi zinafanywa na wazazi, uko wajibu wa wanafunzi wenyewe na wadau mbalimbali wa elimu.

Mheshimiwa Spika, michango kwa elimu na miundombinu inaruhusiwa kwa utaratibu uliowekwa, Wakuu wa Wilaya wameelekezwa kwa kushirikiana na wazazi waunde Kamati mbalimbali wanachangisha wale wanaoweza, ambacho kimeelekezwa ni kwamba kusiwe na michango ambayo ni gandamizi, akinamama kunyang’anywa meza na mitaji yao midogo midogo, lakini michango ya kuchangia elimu na miundombinu yake inaruhusiwa kwa usimamizi wa Wakuu wa Wilaya na Wakurugenzi na kwa vibali maalum, Kwa hiyo, naomba Waheshimiwa Wabunge wasaidie hilo, liendelee kufanyika. Hili linaenda sambamba pamoja na zoezi la kumalizia maboma yaliyopo.

Mheshimiwa Spika, juzi niliulizwa swali hapa juu ya maboma; nikawaambia tunahitaji takribani zaidi ya bilioni 417 kumaliza maboma yote nchi nzima, lakini, tutakuwa tunafanya kwa awamu kulingana na uwezo uliopo, mazungumzo yanafanyika na Wizara ya Fedha, kikao kilimeshafanyika chini ya Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI. Kwa hiyo ina maana muda sio mrefu sana zoezi hili litapunguza idadi ya maboma ambayo yapo katika eneo hilo. Kwa hiyo, tuna uhakika kwamba ndani ya muda mfupi ujao, madarasa yatajengwa na watoto wetu hawataendelea kukaa chini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia niwatoe wasiwasi, wanafunzi wote ambao wamefaulu kwenda kidato cha kwanza mwaka 2019 wote wataingia darasani na watasoma. Mpaka kufikia mwezi wa Tatu kazi nzuri imefanyika na hili jambo linasimamiwa vizuri sana. Kwa hiyo wananchi na Watanzania wasiendelee kuwa na hofu, hili jambo linasimiwa na Serikali ipo kazini, wasiwe na hofu.

Mheshimiwa Spika, kuna hoja imejitokeza hapa ya kuimarisha usomaji, zile KKK (Kusoma, Kuhesabu na Kuandika). Tuna miradi miwili mikubwa, mradi wa kwanza, unaitwa EMIS na tumeenda mbali zaidi na EQUIP ambao mradi huu una fedha nyingi sana zinaenda. Tunafundisha Walimu wa darasa la kwanza na pili, mpaka la tatu na la nne. Tumejenga shule zinaitwa shikizi, ambazo unapunguza umbali kutoka nyumbani kwa mtoto na shule mama na Waheshimiwa Wabunge ni mashahidi tumezikagua zinaendelea. Tumefundisha Kamati za Shule, tumefundisha Walimu, tumetoa tablets. Kwa hiyo mambo mengi makubwa sana yanafanyika katika eneo hilo. Naomba mtuunge mkono tuendelee kufanya kazi hiyo na kila mtu ambaye anaweza kuchangia elimu, achangie elimu lakini kuunga mkono juhudi za Serikali kwa kazi kubwa ambayo Mheshimiwa Rais anaifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ni kweli, baada ya elimu msingi bila malipo, changamoto ni kubwa ufaulu wa wanafunzi umeongezeka, watoto wengi wanaenda mashuleni waliokuwa wanashinda kwenye masoko, sasa hawaendi masokoni wanakwenda shuleni, wale ambao walikuwa wanapiga debe, sasa hawaendi, mtaani watoto hawapo, wote wameenda shuleni. Hili ni jambo kubwa, tumpongeze Mheshimiwa Rais na Serikali ya Awamu ya Tano ya Chama cha Mapinduzi kwa maamuzi thabiti kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la kuweka kumbukumbu hapa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa…

NAIBU WAZIRI, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. MWITA M. WAITARA): Mheshimiwa Spika, dakika moja, tu...

SPIKA: Waitara. (Kicheko)

NAIBU WAZIRI, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. MWITA M. WAITARA): Mheshimiwa Spika, jambo la ufaulu ambapo matokeo yametolewa. Maafisa Elimu wameonesha kwamba shule za private zimefaulu zaidi kuliko shule za Serikali. Serikali inasimamia shule za msingi zaidi ya 16,000, shule za private ni shule 1,413 sawa na asilimia nane tu, lakini hawa wenzetu katika shule zao wanachuja watoto, kuna mitihani ya darasa la nne ya Serikali, ya kidato cha pili na cha nne.

Mheshimiwa Spika, kwa maelekezo ya Serikali kwa Waraka nilionao watoto wakifaulu wa darasa la nne, wakifaulu wa kidato cha pili, hawa wanamaliza mtihani darasa la saba, wamalize na kidato cha nne, wenzetu wanawachuja watoto, wanawarudisha nyumbani. Kwa hiyo wale wote ambao wameanza la kwanza mpaka la saba, la sita wamezuiliwa; wale ambao wameenda form one mpaka three wamerudishwa, sisi Serikali ni kokoro, wote tunawapokea, wanafanya mitihani, asilimia nane huwezi kulinganisha na asilimia 92.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa muda ulionipa. (Makofi)