Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018

Hon. Edward Franz Mwalongo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Njombe Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018

MHE. EDWARD F. MWALONGO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa name niweze kuchangia Kamati mbalimbali ambazo zimewasilisha taarifa zake leo ikiwemo Kamati ya UKIMWI, ambayo mimi pia ni Mjumbe katika Kamati hiyo. Awali ya yote nimpongeze sana Mwenyekiti wangu, kwa wasilisho lake lililo zuri kabisa.

Mheshimiwa Spika, mapambano dhidi ya UKIMWI yana utata mwingi sana, lakini sisi kama nchi, nadhani sasa imefika wakati tuweze kuona kwamba ni nini tufanya ili tuweze kupambana na UKIMWI vilivyo. Kwanza kabisa nianze na jambo moja, uko ukinzani wa kisheria ambao unatuletea shida sana katika mapambano dhidi ya UKIMWI.

Mheshimiwa Spika, Sheria ya Ndoa, inasema, mtoto anaweza akaolewa kwa ridhaa ya mzazi, akiwa na miaka 14, lakini Sheria ya UKIMWI inamtaka mtoto huyu apime kwa hiyari vizuri vya UKIMWI akiwa na miaka 18. Maana yake nini? Maana yake binti au kijana au hawa wanandoa, wakitaka kupima na hata kama wameshaoana, maana yake wafunge safari warudi kwa wazazi, wakawaambie wazazi wao kwamba sasa tunaomba mtusindikize Hospitali au kwenye kituo cha kupima, tukapime UKIMWI. Ni jambo ambalo linaleta utata sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba sana Serikali iangalie tufanye nini haraka iwezekanavyo ili hizi sheria zisikinzane. Haiwezekani mtoto huyu mwenye miaka 14 aende kwa mzazi akaombe kwenda kupima. Kwa hiyo, nayo inaleta shida katika mapambano dhidi ya UKIMWI.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo linaleta shida katika mapambano dhidi ya UKIMWI, liko tatizo kubwa sana, ukisoma kwenye bajeti za Wizara UKIMWI ipo kwenye kipaumbele. Hata ukienda kwenye Halmashauri, mapambano ya UKIMWI yako kwenye kipaumbele, lakini ikija kwenye utekelezaji, liko tatizo kubwa. Ni kwamba haya mambo yanapitishwa na Bunge hapa, bajeti inatengwa, lakini ikifika kule Wizarani au ama kwenye Taasisi za Umma inawekwa tu, hakuna anayeifanyia kazi.

Mheshimiwa Spika, tumeshuhudia kwenye Kamati yetu ya UKIMWI, tukiita Taasisi za Umma, kuja kueleza afua za UKIMWI mahala pa kazi, unakuja kuta ndiyo Kamat imeundwa. Maana yake ni nini? Wito wa Bunge kuja kujibia afua za UKIMWI kwenye Taasisi zao za Umma ndiyo imewafungua macho kwamba kumbe liko jambo tunatakiwa kulijadili katika ngazi ya Wizara au kwenye ngazi ya Taasisi yetu ya Umma.

Mheshimiwa Spika, Taasisi nyingi kwa lugha ya kawaida hazikuweza kufika kwa wakati kwa sababu hazikuwa na cha kusema mbele ya Kamati. Kwa hiyo, wanakwambia tumeunda Kamati na ndiyo tumeanza. Unauliza Wizara nzima, kuna Watumishi wangapi kwa hiyari yao wamesema wao wana virusi vya UKIMWI, wanakwambia mmoja; wengine wanasema hakuna. Kwa hiyo, unaona kabisa kwamba kumbe jambo hili katika jamii linazoeleka na linaonekana ni jambo la kawaida. Kama linazoeleka na linakuwa jambo la kawaida madhara yake ni kwamba mapambano haya hatutafanikiwa. Kwa sababu hatuchukulii kama ni jambo hatari na linahatarisha maisha yetu.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, napenda kutoa wito kama Mjumbe wa Kamati ya UKIMWI kwamba Wizara na Taasisi za Umma zote mahala pa kazi, zihakikishe kwamba suala la UKIMWI, linajadiliwa na wale wote ambao wanaohusika wapime na waweze kupata majibu kujua kwamba hali zao za afya zikoje? Baada ya kujua hali zao za afya, basi waanze kufuata hizo afua za UKIMWI.

Mheshimiwa Spika, tatizo lingine ambalo linatusumbua sana kwenye mapambano dhidi ya UKIMWI ni usiri. Usiri ndiyo unaoathiri sana katika mapambano dhidi ya UKIMWI. Usiri huu sasa hivi inaelekea umetengenezwa na Taasisi zinazotoa huduma za Afya. Zamani hapo ilikuwa kuwawekea wagonjwa wa UKIMWI mahali maalum pa kutibiwa, pa kuchukua dawa na Mganga Maalum, ilikuwa ni jambo linaloonekana ni jambo la faragha na jambo linalowasaidia wagonjwa wa UKIMWI. Leo, hali hiyo imebadilika imekuwa sasa huo ndiyo unyanyapaa wenyewe, kwamba mtu hayuko tayari kwenda kule kwenye kituo cha kutolea huduma za dawa na vipimo, CTC.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naishauri sana Serikali, hebu tuufute ule utaratibu wa CTC, wagonjwa wote sasa waende kwenye huduma ya kawaida; tukikaa kwenye mstari pale hospitalini, mimi mwenye virusi na mwingine asiye na virusi tukae pale tumwone Mganga huyo huyo, tutibiwe tuondoke. Tuache ile kwenda kuwaficha wagonjwa wa virusi mahali kwenye CTC na kuwapangia siku maalum, kwa sababu hiyo inasababisha sasa watu wengi zaidi; moja, waende hospitali za mbali sana kutafuta huduma, au vituo vya mbali sababu ya aibu, lakini pili, akikosa nauli ama uwezo wa kwenda huko mahali, matokeo yake anakuwa hawezi kwenda kupata zile dawa na anaacha kutumia dawa. kwa hiyo, nafikiri, tuondoe huo usiri na ugonjwa wa UKIMWI tuuone ni ugonjwa wa kawaida. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hali za afua za UKIMWI zilipofikia sasa, zimefanya ugonjwa wa UKIMWI uonekane wa kawaida kabisa. Nampongeza sana Dkt. Maboko na Taasisi yake ya TACAIDS wanajitahidi sana kufanya vizuri na wanatoa elimu vizuri, lakini kikubwa hali ya bajeti ya Taasisi hii iko chini sana. Kwa hiyo, hiyo nayo itakuwa ni kikwazo kwa maana ya mapambano dhidi ya UKIMWI.

Mheshimiwa Spika, suala la madawa ya kulevya; Taasisi ya Kupambana na Madawa ya Kulevya katika nchi yetu kwa kweli imefanya kazi kubwa sana, chini ya Dkt. Sianga. Tunatakiwa wote kama Watanzania tuwapongeze, lakini vile vile tuwaunge mkono. Hali tuliyokuwa tunaenda nayo kama nchi ilikuwa ni mbaya sana. Ilikuwa kila mahali unapokwenda, hukosi wanaoitwa mateja, lakini leo hii kumkuta teja ni kazi ngumu kidogo. Kwa hiyo, hii ni dalili kwamba Taasisi hii inafanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hii maana yake nini? Maana yake ni kwamba Taasisi ya Kupambana na Madawa ya Kulevya peke yake, haiwezi. Sisi kama Watanzania, kama Wabunge ni lazima tuisaidie hii Taasisi. Serikali nayo iwekeze katika miundombinu ya kisasa ya kuhakikisha kwamba vifaa vya kisasa vya kupima na kutambua madawa ya kulevya vinakuwepo ndani ya nchi na vinaweza kusaidia Taasisi hii, kuweza kufanya kazi vizuri. (Makofi)

Mheshimiwas Spika, jambo lingine ambalo ningeweza kuliongelea ni suala la elimu. Tunafahamu kabisa kwamba sasa tunatekeleza elimu bila malipo, lakini suala hili bado lina mkanganyiko mkubwa sana katika jamii yetu. Utakuta kwamba miundombinu mingi wananchi wamejenga; wamejenga madarasa, wamejenga mabweni kwa ajili ya wanafunzi, lakini hayana samani mle ndani. Linapokuwa suala la samani inakuwa ni shida sana. Naomba sana Serikali itoe muongozo vizuri. Nafahamu kabisa kwenye mwongozo uliotolewa mara ya mwisho juu ya elimu bila malipo ilieleza kabisa kwamba jukumu la miundombinu ni jukumu la wananchi, lakini inapofika mahali fulani kuna mkanganyiko unatokea, baadhi ya sehemu hawatambui kwamba dawati ni sehemu ya miundombinu.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, anapoambiwa mzazi achangie dawati, lakini hapo kunatoa ukinzani; wako Maafisa wa Serikali wanasema hapana, hatakiwi kuchangia. Unajiuliza, mtoto anakwenda shuleni, atakalia nini? Fedha ya dawati iko wapi? Kwa hiyo, naomba sana, hili litolewe ufafanuzi mzuri ili kusudi tusiende kule tukakanyagana kati ya Watendaji na wananchi.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ni suala la Ikama ya Walimu. Hali ya Walimu katika nchi yetu imekuwa mbaya sana. Shule nyingi hazina Walimu. Mimi nafikiri kupanga ni kuchagua. Kama tunaamini kabisa kwamba elimu ndiyo msingi wa kulifanya Taifa letu liwe bora. Naomba sana sasa Serikali ifanye maamuzi magumu kwamba ikamilishe Ikama ya Walimu. Inapokuwa inakamilisha Ikama ya Walimu kwenye shule zetu, vile vile iangalie, liko tatizo linajitokeza, Walimu wanastaafu, kwa sababu tunajua kabisa Mwalimu akistaafu maana yake atakuwa hayuko kwenye Utumishi, pale panakuwa na pengo.

Mheshimiwa Spika, katika Halmashauri inafika mahali wanastaafu Walimu zaidi ya 30, hakuna hata Mwalimu mmoja anayeajiriwa katika Halmashauri ile. Mara ya mwisho tukaambiwa kwamba ikiwa waliopatikana na vyeti bandia, walikuwa 15, basi Halmashauri hiyo inarejeshewa Walimu 15. Kwa uhakika kabisa katika Halmashauri yangu ya Njombe Mjini, hilo halikufanyika. Walitolewa Walimu kati ya 15 na 18 lakini walioletwa ni Walimu wanne, kitu ambacho nimejaribu kuulizia na kufuatilia imeonekana ni tatizo kabisa.

Mheshimiwa Spika, shida ya Walimu ni kubwa sana na ni shida ya nchi nzima. Kwa hiyo, naomba sana, tukamilishe idadi ya Walimu katika shule zetu, kwa sababu wananchi wanajenga miundombinu, wanajitahidi.

Mheshimiwa Spika, upande wa Sekondari hakuna shida kubwa sana, shida tu kwa Walimu wa Sayansi, hasa Shule za Msingi kuna shida kubwa sana. Inafika mahali ambapo wananchi wanaambiwa jamani, sawa mmeleta watoto shuleni, liko Darasa la Awali, hili darasa sasa hatuna Mwalimu, tunajadiliana sisi kama wazazi tunafanyaje? Sasa kunatokea upinzani, wengine wanasema ni elimu bure, wengine wanasema tuchangie jamani watoto wasome, mazingira kama hayo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naomba sana Ikama ya Walimu iangaliwe sana na Serikali.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)