Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018

Hon. Dunstan Luka Kitandula

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mkinga

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018

MHE. DUNSTAN L. KITANDULA - MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa hii ya kuhitimisha hoja yangu. Nianze kwa kuwashukuru Waheshimiwa Bunge ambao wamepata fursa ya kuichangia hoja hii na kutoa mchango wa mawazo. Hoja hii imechangiwa na jumla ya Waheshimiwa Wabunge 27, katika hao Wabunge 25 wamechangia kwa kuzungumza na Waheshimiwa Wabunge wanne wamechangia kwa maandishi. Katika hao wanne waliochangia kwa maandishi lakini vilevile walizungumza, kwa hiyo, tunabaki na Waheshimiwa Wabunge wawili ambao walichangia kwa maandishi. Kwa hiyo jumla ni Waheshimiwa Wabunge 27.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kuchangia hoja hizi karibu kila Mheshimiwa Mbunge ameunga mkono hoja ya Kamati yetu. Kwa hiyo, nitumie fursa hii kuwashukuru sana kwa kuunga mkono hoja za Kamati hii. Vilevile kwa niaba ya Kamati, nichukue fursa hii kuwashukuru kwa pongezi mlizotoa kwa kazi iliyofanywa na Kamati, tunawashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile niwashukuru Waheshimiwa Mawaziri ambao wamefanya kazi kubwa ya kujibu sehemu kubwa ya hoja zilizokuwa zimetolewa. Zipo hoja ambazo zilikuwa ni nje ya hoja ya Kamati, kwa hiyo, sitarajii kuzijibu lakini tunazichukua kama rejea ya Kamati kwa ajili ya kuzifanyia kazi kwa siku zijazo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nitajikata katika maeneo manne yaliyojitokeza kwa upana ambayo Waheshimiwa Wabunge kwa uwingi wao waliyagusia. Eneo ya kwanza ni eneo la REA. Waheshimiwa Wabunge wameonesha kwamba Mradi wa kupeleka Umeme Vijijini ni hitaji la kila Mtanzania na kwamba kama Taifa tuna kila sababu ya kuhakikisha tunafanya kila linalowezekana kuhakikisha kwamba tunakamilisha utekelezaji wa miradi hii kwa wakati. Kamati iliainisha changamoto kadhaa ambazo bahati nzuri na Waheshimiwa Wabunge wamezitolea maelezo. Niishukuru Serikali imekubali kufanyia kazi changamoto zote zilizojitokeza upande wa REA. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ni umeme wa Mto Rufiji. Namshukuru Mheshimiwa Waziri ametoa maelezo ya kina sana katika eneo hili. Mradi huu kama tunavyofahamu utachukua miezi 36 ya utekelezaji. Mradi huu ulitiwa saini Desemba, 2018 na baada ya kutiwa saini miezi sita itakuwa ni kipindi cha mkandarasi kuji-mobilize kabla ya kuanza kuutekeleza mradi huu.

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi kama Kamati tunasema mradi huu ni wetu. Kwa hiyo, kama Taifa kwetu sisi mradi huu ni wa kufa na kupona. Tulipofika sasa siyo sehemu tena ya kuzodoana na kurudishana nyuma, tulikofika sasa ni kusema tunafanya vipi vizuri zaidi ili mradi huu, hiki chetu kiweze kufanikiwa vizuri. Ndiyo maana katika mapendekezo yetu kama Kamati tumeiomba Serikali ihakikishe kwamba tunasimamia vizuri utekelezaji wa mradi huu na kwamba fedha za utekelezaji mradi huu zitolewe kwa wakati ili usiweze kukwama. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine linagusa mapendekezo ya wadau wa sekta ya madini. Waheshimiwa Wabunge wengi waliozungumza wameonesha ipo haja kubwa ya kuwawezesha wachimbaji wadogo. Wameonesha nia na matarajio kwamba tukiisimamia vizuri sekta hii basi mchango wake utakuwa mkubwa kwa uchumi wa Taifa letu. Hicho ndicho ambacho sisi katika Kamati tulikiona na ndiyo maana tumependekeza yale mapendekezo yote ya mkutano wa wadau yafanyiwe kazi. Nafurahi kwamba Mheshimiwa Waziri wa sekta husika ameonesha utayari wa kuyafanyia kazi maeneo haya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ambalo limezungumzwa kwa mapana na kwa hisia tofauti ni mradi wa Songas na mikataba yake. Mazungumzo yalivyoendelea hapa ndani yalijikita zaidi kwenye mradi Songas lakini sisi tuliiangalia sekta nzima ya gesi nchini tukifanya rejea ya Kamati ndogo iliyoundwa na Mheshimiwa Spika ya kuishauri Serikali jinsi Taifa linavyoweza kunufaika na mapato ya gesi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika hili tunampongeza sana Mheshimiwa Spika kwa ujasiri na umakini mkubwa alioufanya kwa kuunda Kamati ile. Namshukuru Mungu nilipata fursa ya kupata nafasi ya kuongoza Kamati ile. Ni Kamati iliyokuwa na watu wa makini, ushauri uliotolewa sina hofu na mashaka hata kidogo kwamba ukifanyiwa kazi utatutoa hapa tulipo ili Taifa liweze kunufaika na rasilimali yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, rai yetu kama tulivyoonesha kwenye mapendekezo yetu ni kwamba jambo lile lifanyiwe kazi ili tuweze kurekebisha kasoro zilizojitokeza. Nafurahi kusikia kwamba Serikali inasema imeanza kufanyia kazi jambo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la mwisho, lipo jambo lilijaribu kusemwa mwanzo hapa kwamba taarifa hii pengine siyo matokeo ya kazi ya Kamati. Napenda niwahakikishie taarifa hii ni matokeo ya mchango wa mawazo ya Kamati. Kamati ilikutana tarehe 24 kujadili rasimu ya kwanza ya taarifa ya Kamati, wakatoa mapendekezo. Kamati ilikutana tarehe 25 kujadili mapendekezo waliokuwa wameyatoa mwanzoni. Kumbukumbu za vikao hivyo ninazo hapa, ukihitaji tutaweza kuziweka Mezani. Ndiyo maana hata mapendekezo yaliyotolewa na wasemaji yalishabihiana moja kwa moja na kile ambacho Kamati ilikipendekeza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho, naomba sasa Bunge lako liridhie na kuidhinisha maoni na mapendekezo ya Kamati ili yawe ni maamuzi ya Bunge lako Tukufu.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kutoa hoja. (Makofi)

MHE. ALLY K. MOHAMED: Mheshimiwa Naibu Spika, naafiki.