Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018

Hon. Lolesia Jeremia Maselle Bukwimba

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Busanda

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018

MHE. LOLESIA J. BUKWIMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia taarifa ya Kamati ya Nishati na Madini kwa mwaka huu uliopita. Kipekee kabisa nimpongeze Mwenyekiti wa Kamati pamoja na Wajumbe kwa jinsi ambavyo wameweza kuandika ripoti nzuri nimeisoma, kwa kweli na ushauri ambao wameutoa ni ushauri muhimu sana katika sekta hii kwa ajili ya kuipeleka mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitaanza na Sekta ya Madini, nianze kipekee kabisa kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa aliyoifanya kwa miaka mitatu, lakini kikubwa zaidi tarehe 22 Januari, 2019 ambapo aliweza kukaa na wadau wa madini Mkoani Dar es Salaam, kwa kweli inaonyesha nia ya dhati kabisa kuweza kuondoa changamoto na kero mbalimbali zilizopo kwa wananchi hasa wachimbaji wa madini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kipekee kabisa niunge mkono kabisa Kamati ambayo imependekeza kwamba yale mapendekezo ya wachimbaji wadogo walivyokutana kule Dar es Salaam, Serikali iweze kuyachukua na kuweza kuyafanyia kazi. Kwa kunukuu yanapatikana katika ukurasa wa 32, 33 na 34. Kwa msisitizo zaidi nikianza na pendekezo la pili ambalo ni kuondoa baadhi ya kodi tumegundua kwamba wachimbaji wadogo na wachimbaji wanazo kodi nyingi ambazo wakati mwingine zinawarudisha nyuma kabisa katika shughuli zao za uchimbaji wa madini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo kutokana na ushauri ambapo wachimbaji wadogo wenyewe wadau wa wachimbaji walivyokutana, nilikuwa naishauri Serikali kipekee kabisa iweze kuangalia na kupunguza hizi kodi ambazo zinakuwa ni kodi zinazokandamiza wachimbaji wadogo wa madini na wachimbaji wakubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kuna ushauri ambao aliutoa kwamba wanahitaji kuanzisha benki ya madini, niunge mkono kabisa kwamba Serikali iangalie namna ya ku-support kuweza kuanzisha benki ya madini ili wachimbaji hasa wale wadogo ambao hawana uwezo wapate fursa ya kuweza kukopeshwa yaani kwa riba nafuu ili waweze kumudu shughuli zao za uchimbaji wa madini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile kuna eneo ambalo pia walizungumzia kwamba katika maeneo mengi ambayo yamepewa leseni za utafiti wa madini unakuta maeneo mengi sana yanachukuliwa kwa ajili ya utafiti wa madini. Lakini maeneo hayo wachimbaji wanakuwa hawaruhusiwi kufanya shughuli zao zozote zile. Kwa hiyo, niunge mkono mapendekezo hayo kwamba Serikali iangalie maeneo haya ambayo mengi yalikuwa yamepewa kwa ajili ya shughuli za utafiti wepewe wachimbaji hasa wadogo waweze kufanya shughuli za kiuchumi hatimaye waweze kuchangia pato la Taifa. Kwa sababu wachimbaji hawa watakapoweza kufanya shughuli zao za uchimbaji wataweza kupata fedha na mwisho wa siku wataweza kuchangia kwenye pato la Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile kuna suala la ruzuku kwa wachimbaji wadogo, niombe Serikali suala hili ni muhimu sana. Siku za nyuma Serikali ilikuwa inatoa ruzuku, lakini hivi karibuni hatuoni tana wachimbaji wadogo kupewa ruzuku. Niiombe sasa Serikali iangalie siri kwa macho mawili, ile benki kama vile wakulima wanavyopewa ruzuku hata wachimbaji wadogo tuangalie namna ya kuwapa ruzuku ili hatimaye waweze kuwekeza zaidi katika shughuli zao za uchimbaji wa madini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile kuna suala muhimu kabisa ambalo wamelizungumzia, ni suala la tozo na ada mbalimbali kwa wachimbaji wadogo wa madini ambazo wamekuwa wakilipa kwa dola. Kwa hiyo, niombe pia hata mimi nashauri kwamba Serikali iangalie tozo hizi zilipo kwa shilingi ya Tanzania, kama ambavyo tunasisitiza hata watu wengine wageni wakiingia ndani ya nchi walipwe kwa shilingi hata katika wachimbaji wa madini pia tuangalie namna ya tozo hizi kulipwa kwa shilingi za Kitanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile napenda pia kusisitiza kuna baadhi ya maeneo ambayo yalichukuliwa kwa ajili ya uanzishaji wa shughuli mbalimbali za madini likiwemo lile eneo la Lwamgasa ambapo wamechukua kwa ajili ya kuanzisha shughuli mbalimbali za uchimbaji lakini kwa ubia na watu wengine. Watu hawa kwa muda mrefu sana eneo hili limechukuliwa lakini hawajapewa fidia. Kwa hiyo niiombe Serikali pia iangalie namna watu hawa wapewe fidia, miezi sita imepita hakuna chochote, ni mwaka sasa hakuna chochote kinachoendelea na sheria tunavyoijua ni kwamba kwa muda wa miezi sita kama wameshafanyiwa tathmini hawajalipwa Serikali inatakiwa kufanya tathmini upya tena ili waweze kulipwa haki zao za msingi. Kwa hiyo, niombe Serikali iangalie sasa namna ya kuweza kuhakikisha hawa ambao wanahitaji kulipwa fidia wanalipwa kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi hawa hawarusiwi kufanya shughuli zozote za kiuchumi katika maeneo yale. Sasa kwa sababu mtu hatumruhusu kufanya shughuli yoyote anapataje uchumi wake kama humruhusu kulima, haruhusiwi kufanya kitu chochote katika eneo lake. Kwa hiyo, naomba sana katika Sekta ya Madini Serikali iangalie namna zaidi ya kuangalia mapendekezo ambayo wachimbaji wa madini na wadau mbalimbali wa madini wameweza kuyapendekeza na kuweza kuiomba Serikali iweze kuyafanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile katika Sekta ya Umeme, Sekta ya Nishati nianze kipekee kabisa kupongeza Serikali hasa Wizara ya Nishati kupitia Mheshimiwa Waziri wa Nishati pamoja na Naibu wake kwa kazi kubwa hakika wanafanya kazi kubwa sana kwenye hii Wizara, kila wakati Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri wanapita sehemu mbalimbali kukagua miradi mbalimbali ya umeme hata kwenye Jimbo langu wamefika, niwapongeze sana kwa kazi kubwa wanayoifanya kwa ajili ya kupeleka umeme kwa Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hii REA III, katika awamu ya kwanza yake, ni kweli wamefanya kazi kubwa kuhakikisha kwamba wananchi wanapata umeme. Niombe sasa zile nguzo ambazo pengine tunapopeleka umeme labda kwenye kijiji fulani, unakuta nguzo zinakuwa chache sana wanaoweza kupata huo umeme ni wachache ukilinganisha na mahitaji. Watanzania sasa hivi wanahitaji kupata umeme kwa sababu umeme ndio maendeleo kupitia umeme watakuwa na uwezo wa kufanya shughuli mbalimbali za kiuchumi, wengine watatumia kwa ajili ya viwanda. Kwa hiyo, nitumie fursa hii kuiomba Wizara kupitia Mheshimiwa Waziri hebu tuangalie kuongezea nguzo za umeme hasa kwenye maeneo ambako wanapeleka umeme huu wa REA, watu wanahitaji umeme sana . (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitatolea mfano tu kwenye Jimbo langu, pale Nyakagomba wamepeleka kweli umeme wa REA III, katika awamu ya kwanza, lakini kila siku hata hivi leo natumiwa meseji sasa Mbunge mbona nguzo hazitoshi, watu wengi tunahitaji umeme? Kwa hiyo, nitumie fursa hii kuomba kabisa kwamba hebu tuangalie kuongeza nguzo kwa sababu wananchi wanapenda umeme kwa ajili ya maendeleo yao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile niishukuru Serikali kwa mradi mkubwa sana wa Rufiji ule wa Stiegler’s Gorge, ni mradi wa kimkakati, naipongeza sana Serikali kwa kufanya maamuzi hayo. Tuna uhakika kwamba baada ya muda mfupi Tanzania itaondokana na tatizo la upungufu wa umeme. Kwa hiyo, niombe tu Serikali iendeleze huo mradi kwa sababu ni mradi mkubwa wa kimkakati ili tuweze kufikia azma ya Serikali ya viwanda. Hakika umeme wa Stieglers Gorge utatusaidia kuweza kufikia hiyo azma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile kuna miradi mingine ya umeme, kwa mfano katika Mkoa wetu wa Geita kuna ule mradi wa 220 KV. Ni kweli Mheshimiwa Waziri amezindua huu umeme lakini hatujaona kinachoendelea. Tuombe hii miradi Serikali iendelee kuwekeza nguvu ili iweze kufanya kazi kwa wakati. Wananchi kama ambavyo nimetangulia kusema wanahitaji umeme… (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa, kengele ya pili imeshagonga. (Makofi)

MHE. LOLESIA J. BUKWIMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. Ahsante sana.