Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Azimio la Bunge la Kuridhia Ubadilishaji Hadhi Mapori ya Akiba ya Biharamulo, Burigi, Kimisi, Ibanda na Rumanyika – Orugundu kuwa Hifadhi za Taifa

Hon. Dr. Hamisi Andrea Kigwangalla

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nzega Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Azimio la Bunge la Kuridhia Ubadilishaji Hadhi Mapori ya Akiba ya Biharamulo, Burigi, Kimisi, Ibanda na Rumanyika – Orugundu kuwa Hifadhi za Taifa

WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, Mhifadhi, ahsante kwa fursa hii, Nashukuru kwanza kwa kukubali hoja hii iletwe hapa kwenye Bunge lako Tukufu, lakini pili kwa mchango ambao umeutoa hapa. Japokuwa umenirushia nondo kwelikweli ukijua kabisa ni Daktari Bingwa wa Afya ya Jamii, lakini najifunza haraka.

Mheshimiwa Spika, awali ya yote kwanza nianze kumshukuru na kumpongeza Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Awamu ya Tano kwa kukubali ushauri wetu mbalimbali ambao tumekuwa tukiupeleka kwake, hususan jambo moja kubwa ambalo mwezi Januari, tarehe 15 alilifanyia uamuzi, kwamba, uhifadhi katika Awamu ya Tano ubadilike kidogo tutoke katika misingi ya uhifadhi ya zamani ambayo ilikuwa inajikita kwenye dhana ya command and control zaidi kwa maana ya kutumia law enforcement zaidi tuhamie kwenye uhifadhi ambao unahusisha maendeleo ya jamii, unafaidisha watu, kwa maana fupi community based conservation.

Mheshimiwa Spika, imefika mahali Mheshimiwa Rais ametoa ridhaa yake, lakini pia ametoa mwongozo ambao sasa unatupa dira ya kuweza kutekeleza azma pana tuliyonayo ya kuichora upya tasnia ya uhifadhi hapa nchini.

Mheshimiwa Spika, mambo mengi yamekuwa yakizungumziwa katika nchi yetu kuhusu uhifadhi, lakini mengi yamekuwa yakikwama kwa sababu, wewe bahati nzuri ni Mhifadhi unafahamu ni jinsi gani sheria za uhifadhi zilivyo rigid, sheria hizi ni ngumu sana. Ukiwa Waziri wa Maliasili na Utalii unataka kufanya ubunifu kwenye maeneo haya utapata tabu sana kwa sababu, ni lazima upate ridhaa ya

Mheshimiwa Rais, Baraza la Mawaziri limshauri, akupe ridhaa yake, uje upate ridhaa ya Bunge, halafu mrudishie tena Mheshimiwa Rais ndio sasa kitu kitokee. Kwa hivyo, unaweza ukawa Waziri ambaye pengine unapata tabu sana kufanya innovation kwenye eneo ambalo umepewa kusimamia kwa sababu ya rigidity ambayo ipo kwenye sheria mbalimbali za uhifadhi.

Mheshimiwa Spika, kwa hatua tuliyofikia na mwongozo ambao Mheshimiwa Rais ameutoa sasa tunafarijika kwamba, tunaweza kusonga mbele na kufanya ubunifu katika maeneo mbalimbali ambayo tunakusudia kuyafanyia kazi. Mheshimiwa Rais ameturuhusu turekebishe mipaka ya maeneo ya uhifadhi na hii ni mojawapo ya jitihada ambazo tunafanya.

Mheshimiwa Spika, katika eneo hilo, kwa mfano, kuna baadhi ya misitu ya reserve, tutaikata tutarudisha kwa wananchi ili kupunguza pressure kwenye maeneo haya ya Hifadhi za Taifa, ndiyo ile dhana ya community based conservation itafanya kazi ipasavyo. Kwanza lazima tutatue changamoto za wananchi, wananchi wanahitaji maeneo kwa ajili ya kuchunga, makazi, kilimo na uchimbaji wa madini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, maeneo kwa kiasi kikubwa katika mikoa ile yalikuwa yamehifadhiwa, kama si Mapori ya Akiba basi ni misitu ambayo inaifadhiwa kwa mujibu wa sheria, Misitu ya Halmashauri ama misitu ya Serikali Kuu. Kwa hiyo, katika kuchora upya ramani ya uhifadhi katika mikoa ile, tutaweza kufikia azma ya kuwapa wananchi maeneo ambayo watayatumia kwa shughuli hizo mbalimbali ambazo wamekusudia. Jambo hilo tu peke yake lilihitaji kwa kweli ridhaa ya Mheshimiwa Rais mwenyewe wala siyo uamuzi wa Waziri wa Maliasili na Utalii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba ya kwako yote niyachukue kama ushauri na tutayafanyia kazi. Hili la kuhamisha wanyama tunalifahamu na tayari kazi hiyo imeshaanza kufanyika. Nikuhakikishie tu kwamba nimefanya ziara mara tatu katika Mapori haya ya BBK katika maandalizi ya kuleta hoja hii ya Azimio ya Kuyapandisha hadhi kwenda kuwa Hifadhi za Taifa, maeneo yale yame-recover kwa kiasi kikubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa Wabunge ambao tulifanya nao ziara mwaka jana ni mashahidi, tulikutana na makundi makubwa ya tembo yakihama kutoka Burigi na kuhamia upande pili wa barabara ambao ni upande wa Hifadhi wa Kimisi na pia kuna makundi makubwa ya nyati yapo katika maeneo haya. Vilevile wawekezaji ambao wamefika kufanya survey kwa ajili ya kuja kuwekeza pale ambapo tutatoa fursa ya kufanya hivyo wameanza kupigana vikumbo, kuwania maeneo mbalimbali kwa ajili ya kuwekeza. Hii ni dhahiri kwamba hata kama private sector nao wanafikiria kuwekeza mle ni dhahiri kwamba maeneo haya yana vivutio ambavyo vitaleta tija katika kukuza utalii katika eneo husika. Kwa hiyo, tutafanya kazi ndogo za kuhamishia wanyama kama ambavyo umetushauri ambao hawapatikani kwa sasa.

Mheshimiwa Spika, lakini kufafanua tu kidogo hili la Ngorongoro Conservation Area Authority tayari tumeshawapa maeneo mengi. Maeneo hayo ya Kolo, Miambani na Mapango ya Amboni. Wiki iliyopita nimesaini administrative directive ambayo sasa ni Waraka wa kisheria kuyahamisha kutoka taasisi moja kuyapeleka taasisi nyingine. Ngorongoro ana maeneo kadhaa ambayo yana urithi wa kiutamaduni ama yana hadhi ya kuwa Geopark kwa sababu ana maeneo mawili ambayo yana hadhi hiyo na yametambuliwa na UNESCO. Kwa hiyo, tumeona tumuongeze pia Mapango ya Amboni, Michoro ya Miambani na Irrigation Scheme ya jadi pale Engaruka, zote hizi atakuwa akizisimamia na kuziendeleza, kwa hiyo, naye Ngorongoro tumempa mzigo.

Mheshimiwa Spika, lakini pia taasisi zote za uhifadhi tumezipa mizigo mingine ya kuendesha maeneo mbalimbali ya mali kale. Maeneo ya Kalenga tumempa TANAPA kwa sababu yapo karibu na Hifadhi ya Taifa ya Ruaha, maeneo ya Isimila tumempa TANAPA, Nyumba ya Mwalimu Nyerere ile ya pale Magomeni tumempa TANAPA na Kilwa, Songo Mnazi tumewapa TAWA. Tumewagawia haya maeneo ili kukamilisha hizi circuit.

Mheshimiwa Spika, kwa hivyo, ndugu yangu Mheshimiwa Msingwa asiwe na wasiwasi, hiki kichwa kilichokalia hapa ikifika mwaka 2020 tufanye tathmini pamoja na utaona tofauti. Kwa sababu kuna mambo mengi tunayafanyia kazi na kwa hakika yataichora upya ramani ya uhifadhi wa nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuunganisha na hoja tu ya Mheshimiwa Nsanzugwanko katika eneo hilo, tunapoelekea kuichora upya ramani ya uhifadhi nchini, pamoja na kupandisha hadhi haya Mapori ya Akiba matano kwenda kuwa Hifadhi za Taifa pia tunakusudia kupandisha hadhi kiini cha mapori ya akiba mengine matatu katika ikolojia hiyo hiyo moja. Pori la Akiba la Kigosi tunachukua kiini tunapandisha kinakuwa national park, tunaacha eneo la nje linabaki kuwa game reserve. Pori la Akiba Moyowosi tunapandisha hadhi kiini pamoja na ile Ramsar site inakuwa national park, pembezoni tunaacha inabaki kuwa game reserve. Pori la Akiba Ugala tunapandisha hadhi eneo la kiini ile satellite area tunaiacha inaendelea kuwa game reserve, tunaunganisha na misitu ya hifadhi ambayo ipo katika maeneo hayo ambayo tunaipandisha hadhi pia inakuwa natural reserves.

Mheshimiwa Spika, malengo yetu ni kuichora upya ramani ya uhifadhi. Pembezoni kabisa mwa misitu ya hifadhi tunarekebisha maeneo ya vijiji, tunakata ardhi ya misitu tunawarudishia wananchi ili wawe na ardhi ya kutosha. Tunaweka alama za kudumu na baada ya kuweka alama za kudumu sasa tunasisitiza na kuimarisha ulinzi wa maliasili hizo kwamba zisivamiwe. Pamoja na kupunguza maeneo hayo lakini pia kuna maeneo mengine ambayo tutayapandisha hadhi na maeneo mengi mapya tutayaazisha kwa sababu ya umuhimu wake kiuhifadhi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa mfano, eneo la Wembele na Nyahua Mbuga ni the only connection kati ya hifadhi zilizoko Kusini; kwa maana ya ecosystem ya Ruaha, Rungwa kuja kuunga kwenye hifadhi zilizopo Kaskazini kupitia Nyahua, Wembele mpaka kutokea Maswa Game Reserve. That’s the only connection ambapo wanyama wanatoka Kusini wanakuja Kaskazini, wanatoka Kaskazini wanaenda Kusini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile maeneo muhimu kama hayo niliyosema connection kati ya Burigi, Biharamulo na Kimisi ukiunganisha na Kigosi Moyowosi kwenda mpaka Mahale, Katavi National Park mpaka Gombe, hiyo pia ni ikolojia moja. Kwa hivyo, kuna maeneo ambayo tunayapandisha hadhi, kwa mfano misitu iliyopo kule Uvinza, Masito East, Masito West, Misitu ya Tongwe East, Tongwe West tunaiunganisha na North East Mpanda yote tunaipandisha hadhi na tunahifadhi katika ngazi ya Kitaifa ama ngazi ya Halmashauri za Wilaya ili kuwe na uhakika wa corridor ambazo zinapitika mwaka wote. Kwa sasa hivi maeneo mengine hayo niliyoyataja ni general land, kwa hiyo, wanaweza kufanya lolote sasa tunaamua kuyahifadhi kwa mujibu wa sheria. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lengo letu ni kutimiza hilo nililolisema la kuichora upya ramani ya uhifadhi. Vijiji ambavyo kwa mfano vipo katikati ya kiini cha maeneo yaliyoifadhiwa tunavihamisha, tunavikatia maeneo pembezoni ili kuwa na uhakika kule ndani pako salama na maisha ya huko kwenye hifadhi yanabaki kuwa salama na wanyama hawatolewi katika njia yao ya kila siku na matokeo yake kuvamia vijiji vya watu na kusababisha migogoro ambayo ulikuwa unaizungumzia.

Mheshimiwa Spika, tunafanya hivi kwa msingi mmoja, sisi watoto wa Tanzania tukitembea nchi za nje huko tunajivuna sana kwamba tunatoka Tanzania. Katika mambo ambayo tunajivuna nayo ni urithi wa maliasili ambao tunao na urithi huu unatambulika kimataifa na sisi ni miongoni mwa nchi ambazo zimetenga eneo kubwa la ardhi yake kwa ajili ya kuhifadhi maliasili mbalimbali ambazo ni urithi kwa sisi tunaoishi leo na vinavyokuja hapo baadaye.

Mheshimiwa Spika, huu ni urithi wa kipekee, ni unique feature ya nchi ya Tanzania na ni urithi ambao unaweza kujizalishazalisha, unaweza kuji-renew haushi. Ni utajiri ambao haufilisiki kama tutaweza kuuhifadhi na kuutunza na ni utambulisho wa nchi yetu nje ya mipaka ya nchi yetu. Kwa hiyo, jukumu la uhifadhi kwa kweli tunalichukua katika viwango vya juu sana na katika umuhimu wa kipekee na ndiyo maana tumeona tuichore upya ramani ya hifadhi zetu hapa nchini.

Mheshimiwa Spika, ni kweli TANAPA inaongezewa mzigo lakini inategemea unalinganisha TANAPA na kitu gani. Uongozi wa Jenerali Waitara na Mkurugenzi wetu, Ndugu Kijazi ni dhabiti na imara. Mimi kama Waziri najiridhisha katika taasisi ambazo nimepewa kuzisimamia TANAPA ina viwango vya juu sana vya utendaji na ndiyo maana kila mtu hapa anawamwagia sifa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, TANAPA wana hifadhi 16 tu, kati ya hizo tano (5) kweli zinajiendesha na zinatoa faida ambayo inasaidia kuendesha hifadhi nyingine. Ukitaka kulinganisha sasa TANAPA ambaye ana hifadhi 16 na TAWA ambaye ana hifadhi zaidi ya 100, utaona migogoro kwa kiasi kikubwa na hizo operesheni zinazozungumziwa hapa zililazimika kufanyika si kwa sababu ya uzembe wa TANAPA, hapana, kwa sababu TANAPA analinda vizuri maeneo yake, ni kwa sababu kulikuwa na uzembe chini Wizara ya Maliasili na Utalii na mamlaka za Serikali za Mitaa na wakati huo TAWA ilikuwa haijaazishwa. Kwa hiyo, kuhamisha baadhi ya majukumu kutoka TAWA kuyapeleka TANAPA mbali na sababu ambazo tumezisema wakati tunatoa hoja yetu ya msingi ni jambo ambalo pia linapunguza mzigo kwa TAWA lakini pia linaimarisha ramani ya uhifadhi hapa nchini.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tunaona pengine ni vyema kwa maeneo ambayo yana umuhimu wa kipekee tukayapeleka TANAPA ili yakapata ulinzi wa kutosha. Kwa mfano, Moyowosi hatuchukui hifadhi yote, tunachukua kiini tu tunampa TANAPA, nje ya kiini tunamuacha TAWA aendele kusimamia. Lengo letu ni moja, kuongeza idadi ya men in the boots, ya askari ambao wako katika eneo husika.

Mheshimiwa Spika, tunafanya hivi siyo tu kwa sababu za ulinzi wa maliasili iliyoko pale lakini kwa sababu za ulinzi mpana wa nchi yetu. Kwa sababu mapori haya yamekaa katika eneo ambalo ni conflict zone; kuna wakimbizi na wahalifu wanaotoka katika nchi za jirani. Kwa hiyo, tunavyoongeza men in the boots kwenye maeneo haya maana yake pia tunaimarisha ulinzi katika nchi yetu, kwa sababu patrol na miundombinu itakuwa mingi na maeneo haya yatabaki kuwa salama. Linakuwa ni jambo la ajabu sisi tunazuia watu wetu wasitumie maeneo haya kwa shughuli zao za kila siku halafu watu wa nchi nyingine wanakuja kuyatumia, ni jambo ambalo halikubaliki kidogo. Kwa hiyo, tumeona bora tuyahifadhi na tuyalinde kwa nguvu zaidi kuliko ilivyokuwa hapo awali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hoja nyingi wamezizungumzia Mheshimiwa Mabula na Mheshimiwa Kanyasu naomba nisizirudie, labda niseme moja hii ya REGROW na Sungura Wawili. Mradi wa REGROW upo pale pale, fedha zimeshaingia ndani ya Serikali. Nilifafanua hapa siku tatu au nne zilizopita, tunachokifanya ni kuendelea kupatana na wenzetu ili mradi ule uwe na tija zaidi. Kuna haja gani ya kujengewa viwanja vya ndege vya changarawe kwa pesa ya mkopo ambayo nchi yetu italipa wakati tuna uwezo wa kuwataka wanaotukopesha watujengee kiwanja ambacho ni cha hard surface (sakafu ngumu) ili kiweze kudumu zaidi. Tunaona economically hai-make sense kuwa na project ambayo itakuwa ya muda mfupi kiasi hicho, halafu project yenyewe si rafiki kwa mazingira.

Mheshimiwa Spika, kwa sababu ukitaka kufanya ukarabati wa kiwanja cha changarawe maana yake ni lazima uchukue material humo humo ndani ya hifadhi, kwa hiyo, pia it is not environmental friendly. Kwa hiyo, tunaona bora tujenge kiwanja cha ndege ambacho ni cha sakafu ngumu na ndilo jambo pekee ambalo tumebaki tukizungumza na watu wa World Bank. Pesa wameshatoa, ruhusa ya kuendelea na mradi imeshatoka na Mradi wa Kukuza utalii Kusini unaendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sambamba na mradi huo, tumepata pesa pia baada ya kuonyesha nia ya kuyapandisha hadhi Mapori ya Akiba kuwa National Park kutoka Global Climate Facility ambao watatupa pia dola za Kimarekani milioni 100 ambazo zitatusadia kufanya maboresho katika Mapori haya ya Akiba kwa sababu na wao wameona kwamba sisi wenyewe tuna nia ya kufanya hivyo. Malengo yetu ni kutimiza azma ya Ilani ya Uchaguzi ambayo sasa imedumu takribani miaka 10 ikizungumzia jambo moja; Mpango wa Taifa wa Maendeleo wa Miaka Mitano sasa mwaka wa tisa huu wanazungumzia jambo moja kubwa nalo ni diversification ya kijiografia ya vivutio vya utalii hapa nchini, haiwezekani tuka-concentrate watalii kwenye kanda moja tu ya nchi yetu, tufungue kanda nyingine. Ndiyo maana tunafungua Circuit hii ya Kusini na Kaskazini Magharibi. Lengo letu ni ku-diversify geographical shughuli za utalii katika nchi yetu ukiacha Circuit ya Zanzibar.

Mheshimiwa Spika, pia tunafungua circuit ya utalii wa fukwe katika ukanda wa fukwe utakaoanzia Bagamoyo kwenda mpaka Tanga. Sasa hivi tuko katika mipango ya awali, tunachora ramani na ile water front yote tunaiwekea mkakati. Pia water front ya Kilwa sambamba na kutambua umuhimu wa kipekee wa magofu yaliyopo pale Kilwa Kisiwani pamoja na jitihada zinazoendelea za kuifungua Circuit ya Kusini pale kuunganisha la Selous National Park kwa upande ule wa nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, kwa hivyo, tunaichora upya ramani ya utalii na uhifadhi katika nchi yetu na hii ni moja ya jitihada.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Waziri.

WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa fursa hii, naunga mkono hoja na naomba kutoa hoja.

WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Spika, naafiki.